KUELEKEA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA ASK. MKUDE ATAHADHARISHA

‘Haki itendeke kwa wote’
Na Pascal Mwanache, Morogoro
NCHI inapojiandaa kutekeleza haki ya msingi ya kidemokrasia ya raia wote kuchagua viongozi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji hapo 2019 wito umetolewa kwa vyombo husika kuwa walinzi wa watanzania wote kwa haki bila kuminya haki za watu wengine.
Wito huo umetolewa na Askofu wa Jimbo Katoliki Morogoro Mhashamu Telesphor Mkude katika Misa Takatifu ya Jumatano ya Majivu iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Mt. Patriki Morogoro. Askofu Mkude amesema kuwa kila mmoja anapaswa kujitathmini iwapo amekuwa mlinzi wa mwingine au amewatendea mema wale tu waliokuwa upande wake.
“Tunapojiandaa na uchaguzi mdogo katika serikali za mitaa tujiulize, mtazamo wetu juu ya jirani upoje? Tumekuwa walinzi kweli. Tumekuwa walinzi wa watanzania wote? au tunakwenda na mawazo gani, kwamba ndugu kwangu mimi ni yule ninayetoka naye mtaa mmoja, au familia moja tu? Mwingine siyo ndugu yangu?  Kama mkiwapenda wale wanaowapenda tu basi hamna mastahili, maana hata wapagani hufanya hivyo” amesema.
Akifafanua juu ya ujumbe wa kwaresima uliotolewa na Maaskofu, Askofu Mkude amesema kuwa mmaskofu wanataka kila muumini ajibu swali aliloulizwa Kaini kuwa ‘ndugu yako yuko wapi na ana hali gani.
“Maaskofu wanataka kuona kuwa kila mmoja ajione mlinzi kwa ndugu yake, hususani ndugu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Tunapowaona ndugu zetu wakiwa kwenye mahangaiko je tunaridhika au tunaumia na kutusumbua ili tufanye kitu kwa ajili yao?” amehoji.
Pia Askofu Mkude amewataka waamini kujikubali kuwa wao ni wamisionari, ambapo Kanisa linapoadhimisha Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara, kila muumini anapaswa ajitathmini.
“Maaskofu katika umoja wetu tumewaandikia barua ya pekee katika kipindi hiki cha kwaresima. Barua inatuelekeza kuwa, Kanisa lote la Tanzania linatafakari upendo wa Mungu ulivyokuja na kutua Bagamoyo kwa njia ya Shirika la Roho Mtakatifu mwaka 1868.  Zamu yetu imefika kushika na kuendeleza mwanga wa upendo wa Yesu ulioletwa nchini miaka 150 iliyopita” ameeleza.
Aidha ameongeza kuwa mwanga huo hautakiwi kuzimika na kufia mikononi mwa waamini, hivyo ni lazima wawe wamisionari, wawaendee watu na kuwafikishia mwanga huu. 
“Wale wakatoliki waliolegea katika imani yao, na wale wanaotafsiri vibaya Biblia wakawapotosha watu wanahitaji nao kujua mwanga halisi na Bwana halisi Yesu Kristo. Umisionari haukuisha katika kipindi hiki cha miaka 150, ni lazima uendelee” amesema.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU