KIONGOZI MKRISTO ASIYEWAJIBIKA AJITATHMINI NDANI YA KWARESIMA

Mwanasheria na Mhadhiri wa kimataifa kuhusu Afrika P.L.O Lumumba aliwahi kusema kuwa moja ya matatizo makubwa Afrika ni kwamba Viongozi wengi wa Afrika hawana sifa ya kuwa Viongozi. Kwa miaka miwili sasa anaisifia Tanzania kuwa ni kinara cha kuigwa Afrika.
Muda huu wa Kwaresima wale wote wenye nyadhifa za uongozi wa dini na serikalini wajihoji kuhusu majukumu waliyopokea. Musa alilelewa kwenye ikulu ya Farao, mfalme wa Misri kwa muda wa miaka 40. (Mdo 7: 20 -23) Kwa miaka 40 alifanya kazi ya kuchunga kondoo wa Baba Mkwe wake Yethro huko Midiani (Mdo 7:30).
Akiwa na umri wa karibu wa miaka 80 Mungu alimpa kazi mpya ya kuongoza watu na kuwatoa Utumwani (Mdo 7:30 - 34). Musa alimwambia Mungu ‘Kwanini umenitwisha mzigo wa watu hawa juu yangu’ (Hesabu 11:11-12).
Kiongozi anabeba Taifa lote kichwani mwake, Musa alihoji kila mara ‘nipate wapi nyama ya kuwapa watu wote hawa’ (Hes 11:13). Sehemu nyingine alihoji ‘nipate wapi maji ya kuwapa watu wote hawa wanywe’ Musa alikiri mbele ya Mungu ‘mimi siwezi kuwachukua watu wote hawa peke yangu’ (Hes 11:14). Kazi ya uongozi wa aina yeyote ile ni mzigo. Musa angelipendelea kuishi kwenye raha za ikulu ya Farao lakini ‘alipokuwa mtu mzima’ akatoka ikulu kwenda kuona ndugu zake ‘akatazama mateso na mizigo yao’(Kut 3:11).
Musa alipenda kubaki jangwani na kuchunga kondoo bila bugudha yeyote lakini ‘nitakutuma sasa uende kwa Farao, kuwatoa watu wangu’ (Kut 3:10). Mungu alimtuma Musa kwenda kutatua matatizo ya wananchi ‘kilio cha wana wa Israeli kimenifikia, nimeyaona mateso yao’ (Kut 3:9). Nenda ‘kawatoe watu wangu’. Kazi ya kiongozi ni kuwapeleka wananchi kwenye ‘nchi njema, pana na iliyojaa maziwa na asali’ (Kut 3:8). Kila mara kiongozi atafute maslahi mapana ya nchi yake. Kiongozi awafikishe wananchi kwenye nchi njema yenye neema na ustawi.
Tatizo kubwa kwetu kila mtu akipata nafasi ya uongozi anaanza kutafuta maslahi binafsi. Kiongozi anaanza kuwaneemeshe ndugu na jamaa zake. Kiongozi anaanza kuiba mali ya wananchi kujitajirisha. Hivi karibuni tumeona huko Zimbabwe na Afrika ya Kusini. Yesu alisema ‘Njoni kwangu mnaoteseka na kusumbuka nami nitawapumzisha’.  Tuliwahi kuona huko Filipini wakati wa Rais Markus na mke wake Imelda. Dhambi ya Mfalme Ahabu na mkewe Jezebel inaendelea mpaka leo.
Kinachosikitisha sana ni kwamba baadhi ya hawa viongozi wanaofanya haya ni wakristo wabatizwa. Hata Viongozi wa kanisa wameingia mtego wa dhambi ya Ahabu na Jezebel. Viongozi wengi wa kanisa hawana tena roho ya kinabii. Viongozi hawa wanajilimbikizia mali binafsi na kuwasahahu maskini na wanyonge.
Uongozi mbaya huliteketeza Taifa. Wimbi la wakimbizi toka Ethiopia kwenda Afrika Kusini ni kwa sababu wanakimbia hali mbaya ya nchini kwao. Sijasikia watanzania wanakimbia kwenda Ulaya. Ulaya na Amerika zilijengwa kwa jasho la watu wengi waliopita wakazifanya nchi zao ziwe za maziwa na asali. Kwa mantiki hiyo viongozi lazima wajenge nchi zao ziwe nchi za Maziwa na asali. Viongozi wa kanisa pia wajenge makanisa yao yawe ya Maziwa  na Asali. Kiongozi lazima atafute maslahi mapana ya nchi yake.
Kama kiongozi anatafuta maslahi mapana ya Taifa lake na kusikiliza kero za wananchi wake basi Mungu alisema ‘Mimi nitakuwa pamoja nawe’(Kut 3:12). Wote wanaopinga Uongozi kwa hila na wivu wanastahili adhabu. Aliwapa ukoma Miriamu na Haruni.(Kut 12: 1-9) Wana wa Kora pia walipewa adhabu( Kut 16: 1-35)
Wakati wa kwaresima kila mtu ajiulize Je mimi ni kiongozi bora? Au ni mfuasi wa Mfalme Ahabu na mkewe Jezebel?  Au tunataka kufanana na Musa?

Tuzinde Mgassa OSB Sakarani Tanga 0717312239

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU