KALENDA YA LITURUJIA NI KWA AJILI YA WAKRISTO WOTE


Kalenda ya Liturujia ni kwa ajili ya Mapadri na watawa? La, hasha! Hiyo siyo kweli. Kalenda ya Liturujia inaandaliwa ili kila Mkristo aweze kuitumia. Kalenda ya Liturujia ni kwa ajili ya kutumia Wakristo wote wakatoliki.
Kalenda ya Liturujia
Kalenda ya Liturujia ni mwongozo wa kiliturujia ambao hutolewa na Idara ya Baba Mtakatifu huko Vatikano – Roma, Idara inayosimamia Liturujia Takatifu; mwongozo huo unawekwa katika lugha ya Kiswahili na Idara ya Liturujia ili kuwawezesha Wakristo wakatoliki nchini waweze kutumia. Kalenda hiyo   huandaliwa kila mwaka kwa ajili ya Maadhimisho ya Misa na kwa ajili ya kusali Sala ya Kanisa.
Kalenda ya Liturujia siyo ya kutundikwa ukutani, bali inaandikwa kwa mtindo wa kijitabu kidogo chenye kurasa takriban 150 ili kwamba Mkristo akishajipatia anaweza kuiweka mfukoni na kusafiri nayo kwa urahisi. Kwa kuwa inatoa mwongozo wa kuadhimisha Misa na kusali Sala ya Kanisa, baadhi ya waamini wamekuwa na fikra kwamba inatengenezwa kwa ajili ya Mapadri ambao wanaadhimisha Misa na kwa ajili ya watawa kwa ajili ya kusali Sala ya Kanisa. Hizo si fikra sahihi; siyo Mapadri na watawa peke yao wanaosali Misa.
Siku ya Dominika kila Mkristo anawajibika kwenda kanisani kumwabudu Mungu kwa kushiriki Misa na wenzake. Miaka ya nyuma Wakristo wengi walifikiri kusali Masifu yaani Sala ya Kanisa ilikuwa wajibu wa Mapadri na watawa peke yao. Wakati huo Sala hiyo iliitwa na wengine eti ni sala ya watawa. Polepole mawazo hayo yamesahihishwa, na waamini wengi wanatambua kwamba hiyo ni Sala rasmi ya Kanisa zima.  Katika parokia nyingi sasa Wakristo husali Masifu ya Asubuhi pamoja kabla ya kuanza kuadhimisha Misa. Ili waweze kujiandaa vizuri kwa kushiriki kusali Masifu ya Asubuhi na kushiriki Misa, Kalenda ya Liturujia ni msaada mkubwa.
Yaliyomo ndani
Ukiwa na Kalenda ya Liturujia mwanzoni kabisa kuna Maelezo ya msingi kuhusu Sherehe na Sikukuu ambazo tarehe zake hubadilika kila mwaka. Tofauti na Sherehe ambazo tarehe zake zimepangwa, hazibadiliki, kama Noeli(25.12), Bikira Maria Mama wa Mungu (1.1), Mtakatifu Yosefu mume wa Mama Bikira Maria(19.3), Kutangazwa kuzaliwa kwa Bwana 25.3), na nyinginezo,  Kalenda ya Liturujia inatoa orodha ya  Sherehe na Sikukuu ambazo tarehe zake hubadilika kila mwaka  kama Dominika ya I ya Majilio, Familia Takatifu, Jumatano ya Majivu, Pasaka, Pentekoste na Sikukuu nyingine. Hapana budi kila Mkristo afahamu tarehe za Sikukuu hizo ambazo tarehe zake hubadilika mwaka hata mwaka.
Kalenda ya Liturujia hukuletea tofauti kati ya Sherehe, Sikukuu na Kumbukumbu. Baada ya maelezo kuhusu ya Maadhimisho hayo mbalimbali, hufuata Kanuni za jumla mintarafu Mwaka wa Kanisa na Kalenda. Mkristo anapata pia maelezo kuhusu aina mbalimbali za kuadhimisha Ekaristi Takatifu. Katika sehemu hiyo kuna maelezo ya Misa anapoongoza Askofu, Misa ya Parokia, Misa katika Shirika au Jumuiya ya waamini, Misa ambayo Mapadri wengi hushirikiana pamoja na maelezo mengine muhimu. Mkristo akijisomea hayo yote huelimika vizuri kuhusu Liturujia.
Baada ya maelezo kuhusu Misa mbalimbali, Kalenda ya Liturujia hutoa maelezo kuhusu Sala ya Kanisa.  Jambo linaloulizwa mara nyingi na baadhi ya waamini kuhusu kufunga, Kalenda hutoa pia maelezo ya Siku hizo za kufunga.
Baada ya maelezo hayo ndipo hutoa maelezo ya kiliturujia ya siku kwa siku kuanzia Dominika ya kwanza ya Majilio mpaka Jumamosi ya Juma la Mwisho katika Dominika za Mwaka. Kila siku Mkristo hupata vifupisho vya Masomo ya siku hiyo. Anachotakiwa ni kuwa na Biblia na kutoka Kalenda ya Liturujia atasoma Masomo ya kila siku. Isitoshe, Mkristo hufahamishwa kuhusu rangi ya mavazi ya Misa ya siku, iwapo siku hiyo huadhimishwa Misa ya Dominika iliyopita, au Kumbukumbu, au Sikukuu.
Muhimu kwa kila Mkristo
Licha ya kuwajuza mambo muhimu katika ujumla wake, Kalenda ya Liturujia inaongeza taarifa muhimu sana kwa ajili ya Kanisa Katoliki la               Tanzania katika kila Jimbo. Hapana shaka taarifa hizo  ni muhimu kwa kila Mkristo.
Kumbukumbu muhimu ya kwanza ni tarehe ya kutabaruku Kanisa kuu la Jimbo. Tarehe ya kutabaruku Kanisa kuu ni muhimu kwa kila Mkristo jimboni kukumbuka kwani Kanisa kuu la Jimbo ni ishara ya umoja wa Jimbo, ni kanisa  la Askofu na ndipo aishipo. Siku hiyo, katika Kanisa kuu inaadhimishwa Misa kuu ya Kutabaruku Kanisa, Misa ambayo  ina hadhi ya Sherehe. Kwa ngazi ya Sikukuu, kila parokia jimboni huadhimisha Misa ya kutabaruku Kanisa, wakimwombea Askofu, Mapadri na wasaidizi wengine wa Askofu. Wakristo wakiifahamu tarehe hiyo wataweza kujiandaa kushiriki Misa hiyo kwa ajili ya kuwaombea wachungaji wao ngazi ya Jimbo. Wakristo wajue kwamba siku hiyo ni sikukuu ya Jimbo lao.
Tarehe muhimu ya pili ni ile ya kuwekwa wakfu Askofu – jimbo na Askofu msaidizi. Kila Askosfu huikumbuka tarehe ya kuwekwa kwake wakfu akimshukuru Mungu. Hapana budi Wakristo jimboni kuifahamu tarehe hiyo ili waweze kuadhimisha Ekaristi kwa nia ya kumwombea Askofu wao. Wale wanaoweza kufika Uaskofuni huweza kuungana na Askofu wao katika Adhimisho hilo la kumshukuru Mungu likiongozwa na Askofu mwenyewe.  Hata hivi Mkristo popote anapokuwa, akiwa na Kalenda yake ya Liturujia, ataweza kumwombea Askofu katika siku hiyo. Pamoja na kumwombea, ataweza pia kumtumia kadi ya pongezi.
Pengine tarehe ya kuwekwa wakfu Askofu hutofautianana na tarehe ya kusimikwa na kukabidhiwa Jimbo. Tarehe ya kusimikwa Askofu ni  muhimu pia; huandikwa katika Kalenda ya Liturujia. Hapana shaka Wakristo watapenda kumshukuru Mungu kwa kumpata mchungaji wanapokumbuka siku aliposimikwa na kukabidhiwa Jimbo.
Tarehe  nyingine ambayo ni muhimu kwa Wakristo kuikumbuka ni tarehe ya kufariki Askofu katika jimbo. Hapana budi waamini kukumbuka tarehe aliyofariki mchungaji wao ili waweze kumwombea kwa Misa siku hiyo. Kila parokia wanatakiwa kuadhimisha Ekaristi kwa ajili kumwombea Askofu wao  hasa tarehe ile  aliyofariki.
Hatima
Kila Mkristo mwenye Kalenda ya Liturujia akifuatia kalenda yake siku kwa siku atafahamu tarehe hizo muhimu na kujiweka tayari kushiriki Misa siku hizo muhimu. Wakristo wasisubiri kutangaziwa kila kitu na uongozi wa parokia, lakini wakiwa na Kalenda ya Liturujia, na kuitumia siku kwa siku wataweza kujiandaa kushiriki Misa vizuri.

Mahali pengine Mkristo aliweza kumkumbusha padri kuhusu tarehe muhimu alipoangalia Kalenda yake. Tunawahimiza Wakristo kujinunulia Kalenda ya Liturujia. Tena ni muhimu sana   kila jumuiya, na uongozi wa Vikundi mbalimbali vya kitume kuwa na Kalenda ya Liturujia . Piga simu kwa mwandishi wa makala hayo.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU