Ask. Ngalalekumtwa aongoza maelfu ya waamini kumzika Padri Mahimbi Iringa


Askofu wa Jimbo Katoliki Iringa Mhashamu Tarcisius Ngalaekumtwa mwanzoni mwa juma ameongoza maelfu ya waombolezaji kumzika Padri Vedasto Mahimbi ambaye alifariki kwa ajali ya gari Januari 31 mwaka huu katika eneo la Lwangwa karibu  na Parokia ya Kifanya Jimbo Katoliki Njombe.
 Misa hiyo Takatifu imefanyika katika Kanisa la Moyo Mtakatifu wa Yesu Parokia ya Tosamaganga ikiongozwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Njombe Mhashamu Alfred Maluma  huku homilia ikitolewa na Mhashamu Ngalalekumtwa ambaye amewata waombolezaji hao wakumbuke kwamba maandiko Matakatifu yanaagiza na kuonya wanadamu wasilale kwenye usingizi wa dhambi.
 “Siri ya Mungu ni agizo tukae katika mazingira ya kukesha. Kila mmoja wetu lazima atambue hilo na kukaa tayari.
Tunapaswa kuwa na hekima yenye utambuzi na uadilifu, hekima ambayo huratibu mwenendo na mahusiano yetu yawe ya haki na upendo,”ameasa  Askofu Ngalalekumtwa. 
Mwenyekiti wa Umoja wa Madri Jimboni humo , Padri Leonard Maliva amemuelezea marehemu Padri Vedasto kuwa ni mtu mchangamfu na hata tabasamu lake lilionyesha kwamba alikuwa ni mtu wa watu na aliupenda upadri wake.
 “Daima tutamkumbuka Padri Vedasto, alikuwa na karama ya pekee hata waliosoma naye, waliohudumiwa naye kamwe hawataweza kumsahau kwa upendo wake kwa watu wote.
 Padri Maliva ambaye pia ni paroko wa Parokia ya Isimani amewataka wombolezaji hao kumuenzi Padri Vedasto kwa kutenda mema na kuyafuata yale mema yote ambayo yeye (Padri Veda) alikuwa akiyatenda.
 Akisoma wasifu wa Marehemu Padri Mahimbi, Paroko wa Parokia ya Mbarali Padri  Romanus Mihali, Padri Mahimbi alizaliwa tarehe 24.10.1971 Kihesa Iringa kwa Wazazi Evaristo na Mama Ferdinanda Sekibabage, alibatizwa 27.11.1977 katika Parokia ya Itengule na Padri Benedict Nganung’a.
 Alipata Sakramenti Takatifu ya Komunio ya Kwanza na Kipaimara 21.09.1980 na Mhashamu Baba askofu Mario A. Mgulunde.

ELIMU.
Padri Mahimbi alipata elimu ya Msingi katika shule Kichangani- Kihesa Iringa mwaka 1980 hadi 1986. Mwaka 1987 alijiunga na masomo katika Seminari ndogo ya maandalizi Tosamaganga. 
Mwaka 1988 hadi 1991 alipata elimu ya sekondari kidato cha kwanza hadi cha nne katika Seminari Ndogo ya Mafinga. 
Mwaka 1992 hadi 1994 alisoma kidato cha tano hadi sita katika shule ya wavulana Songea. Na mwaka 1994 hadi 1995 alifanya mwaka mmoja wa kichungaji katika parokia ya Kihesa. 
Mwaka 1995 – 1997 alipata elimu ya Falsafa katika Seminari Kuu ya Peramiho. Mwaka 1997  hadi 2000 alipata elimu ya Teolojia katika Seminari Kuu ya Peramiho. Mwaka 2010 alitunukiwa Shahada ya Uzamili ya Falsafa Chuo Kikuu cha Urbaniana Roma Italia. 
Mwaka 2012 alitunukiwa shahada ya Uzamivu ya Falsafa katika  Chuo Kikuu cha Urbaniana Roma Italia.

DARAJA
Daraja Takatifu la Ushemasi alipata 28.12.2001 na Mhashamu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa katika Kanisa Kuu la Kiaskofu Kihesa Iringa na Daraja Takatifu la Upadri  03.07. 2002 na Mhashamu Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa katika Kanisa Kuu la Kiaskofu Kihesa Iringa.

UTUME.

Septemba 2002- 2004 Paroko Msaidizi katika Parokia ya Mgololo. Julai 2004 – Julai 2007 Jalimu na Mlezi katika Seminari Kuu ya Peramiho. Mwaka 2012 -2018 alirudi tena Seminari Kuu ya Peramiho kuwa Jalimu na Mlezi.

KIFO.
Padre Vedasto Mahimbi amefariki Januari 31, 2018 kwa ajali ya gari katika eneo la Lwangwa karibu na parokia ya Kifanya Jimbo Katoliki Njombe.
Raha ya Milele Umpe Ee Bwana na Mwanga wa Milele umwangazie, apumzike kwa amani, amina.

Na Getrude Madembwe, Iringa.


Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU