Gumzo kuhusu Kanisa kumzika Hayati Kingunge latolewa ufafanuzi

n Na Sarah Pelaji, Dar es Salaam
Baada ya Taifa la Tanzania kumpoteza mwanasiasa mkongwe Mzee Kingunge Ngombale Mwiru Febriari 2 mwaka huu katika  Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, jijini Dar es Salaam kumekuwepo na gumzo la jamii kulishutumu Kanisa Katoliki kumzika kwa madai kuwa Hayati Kingunge  aliikana imani Katoliki katika enzi za uhai wake.
Akizungumza na Gazeti kiongozi, Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam Mhashamu Euzebius Nzigilwa amesema kuwa, Kanisa lipo wazi kutoa huduma zote za kiroho kwa mtu yeyote aliye tayari kushika mafundisho ya imani Katoliki.
“Ni kweli Mzee Kingunge enzi za uhai wake kuna masuala mbalimbali ambayo yalimsababisha aasi imani Katoliki lakini wakati akiwa mgonjwa alijirudi na kuonesha nia na utayari wa kumrudia Mungu wake.
Mda wa kumrudia Mungu wakati mwingine hautabiriki na yeye alikuwa na viashiria vya imani na kwamba alitaka kurudi kwenye imani Katoliki.
Viashiria hivyo ni kutubu na kuomba Sakramenti ya Upako wa wagonjwa na  Kanisa lipo kwa ajili ya mtu anayetubu.
Kanisa halihukumu ila  Kanisa lipo kwa ajili ya kumpatia mwanadamu huduma za kiroho katika safari yake ya kwenda Mbinguni.
Mzee Kingunge mwishoni kabisa mwa maisha yake ameonesha nia yake na heshima kwa Kanisa ingawa kuonesha nia ni kitu kingine  na kutekeleza mashari ni kitu kingine,” ameeleza Askofu Nzigilwa.
Amesema kuwa, Upako wa wagojwa ni Sakramenti inayomsaidia mwanadamu kuendelea na safari ya maisha na kumpa nguvu. Padri humuombea neema ya Mungu na kumpaka Mafuta Matakatifu mgonjwa aliye katika hatari ya kifo kwa ajili ya neema ya roho na mwili. (Yak 5:14-15, Mk 6:13).
Kuhusu kuzikwa, Askofu Nzigilwa amesema kuwa, kwa upande wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam si kawaida Katekista kuendesha ibada ya mazishi kutokana na mazingira na uwepo wa mapadri ingawa kwa mazingira ya watu wanaoishi vijijini ni kawaida.
“Mtu aliyeasi imani akionesha nia ya kurudi Kanisa linafungua milango na kumpokea ingawa lazima apewe masharti kwa kuzingatia kanuni na taratibu za Kanisa Katoliki.
Mzee Kingunge alionesha nia lakini kuna baadhi ya vipengele alikuwa hajakamilisha akafariki. Ndiyo maana nimeeleza kuwa, kuwa na nia ni kitu kingine na kutimiza masharti kulingana na taratibu za Kanisa ni kitu kingine.
Kwasababu hakupata nafasi ya kutekeleza kanuni na taratibu  mbalimbali kwa kufariki, basi ilibidi azikwe na Katekista kuonesha kuwa bado ana pungufu flani hivyo hapati ile huduma kamili ya Kanisa anapata huduma ndogo (minimum service) .
Angekuwa ametimiza kila kitu angezikwa kwa Ibada ya Misa Takatifu na maadhimisho yote anayopaswa kupatiwa Mkristo kamili wa Kanisa Katoliki,” ameeleza Askofu Nzigilwa.
Amewaasa waamini wote wa Kanisa Katoliki kujitahidi kishika imani kwa  nia na matendo kulingana na taratibu za Kanisa.
Kifo cha hayati Mzee Kingunge kitupe fundisho la kuwa tayari kwa ujio wa Bwana.
Mzee angefariki ghafla na kukosa nafasi ya kuonesha nia asingepata hata hiyo huduma ndogo ya Kanisa (minimum service) ingekuwa kitu kingine kabisa,” amesisitiza Askofu Nzigilwa.
Akizungumza na Gazeti Kiongozi Monsinyori Deogratius mbiku ambaye ni ndugu yake Hayati Kingunge na ndiye aliyempatia huduma ya kiroho kwa mara ya mwisho na kuzungumza naye ameliambia gazeti hili kuwa, Hayati Kingunge alikuwa anasumbuliwa na falsafa ya wakomunisti.

Mahojiano kati ya Gazeti Kiongozi na Monsinyori mbiku 
Je, Hayati Kingunge alikuwa Mkristo?
Monsinyori Mbiku: Kingunge Ngombale Mwiru alikuwa mkristo Mkatoliki aliyebatizwa akapata Sakramenti ya komunio ya Kwanza na Kipaimara , akasoma kwenye shule ya misheni  pale Msimbazi alikaa bweni  na baadaye shule ya middle school Ilala lakini alikuwa anarudi kukaa pale msimbazi.Alikuwa pia mtumishi wa Misa.

Inasemekana alishawahi kutengwa na Kanisa akiwa mdogo. Sababu zake ni zipi?
Tangu utoto wake mzee Kingunge alikuwa na akili nyingi na akili hizo zilimsababisha kuhoji masuala mbalimbali ya imani.Alikuwa anauliza, Dini ni nini? Mungu yupo wapi? Alisoma mafundisho ya Katekisimu lakini alikuwa mdadisi sana na kile alichokuwa anakiamini.
Yeye mwenyewe Kingunge alisimulia kuwa, wakati fulani Padri mmoja Mkapuchini kwa jina Clementi M. alimuona anadadisi mno masuala ya Imani na kumtilia shaka. Ndipo akamtenga na Kanisa akiwa darasa la sita. 
Huyo Padri alimuuliza wewe ni mkomunisti? (asiyeamini Mungu)  na kama ni umkomunisti ninakutenga na Kanisa.

Je, kama hakuamini Mungu alifungaje ndoa Takatifu?
Mons. Mbiku:  Alipopata mchumba ambaye ni mkatoliki na kutaka kufunga ndoa ya kikatoliki, Kingunge alikataa akaamuru kufunga ndoa bomani.
Kweli wakafunga ndoa ya bomani lakini mke wake akaenda kwa Kardinali Lauriani Rugambwa wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam akamueleza kuwa mume wake (kwa ndoa ya bomani) amekataa kufunga ndoa ya Kikristo kwenye Kanisa Katoliki naye anaogopa kutengwa na Kanisa.
Kard. Rugambwa akamuambia amuite wazungumze. Kingunge alipofika Kardinali akamuuliza wewe si mkrito? Ukifunga ndoa bomani tu huyu mkeo tunamtenga na Kanisa lakini Kingunge akabaki na msimamo wake akisema mimi siamini Mungu kwanini nifunge ndoa Kanisani?
Kard.Rugambwa akamwambia  kama unampenda mkeo fanya lolote litakalowezekana kumsababisha mkeo arudishwe kwenye imani kwa Sakramenti ya Ndoa Takatifu lakini itakuwa ndoa  ya mseto. 
Kingunge akakataa akasema hawezi kushuhudiwa na umati wa watu akifunga ndoa Kanisani. 
Kard. Rugambwa akamueleza kuwa, tutaenda mahali ambapo hakuna watu wengi. Utakuwa  wewe na mkeo na wasimamizi wawili, msimamizi wako mmoja na wa mkeo mmoja hivyo watu wanne na mimi wa tano. Tutafanya misa ya private. Ilimradi muweke maagano mbele ya Mungu.
 Hiyo Misa itasababisha mke wako aitwe mkatoliki kamili na hatatengwa. Kingunge akakubali wakaenda Kurasini kwa Benediktini procuria wakafunga  ndoa. Baada tu ya Misa hiyo Kingunge akamshukuru Kardinali akaenda kazini kwake na mkewe nyumbani.
Jioni wakakutana kusherehekea kidogo. Kuanzia hapo mkewe akawa Mkatoliki kabisa na yeye akaendelea na maisha yake.
Tangu enzi hizo mkewe alikuwa akimuombea mumewe abadilike kwakuwa familia yake ilikuwa ya kikatoliki ingawa Kingunge pia hakuwahi kuwazuiya wala kulidhihaki Kanisa Katoliki. Alikuwa nasumbuliwa na Falsafa ya ‘kwemi Mungu yupo?’

Ameshiriki maendeleo ya Kanisa?
Monsinyori Mbiku: Ndiyo wala alikuwa hana tatizo na Kanisa. Kule Goba kwenye kigango cha Bikira Maria  Mama wa Huruma tanki bovu kuna shamba la Kingunge ambalo alilitoa kama zawadi lijengwe Kanisa. Na ninakumbuka alisema, “Mtakapomaliza kujenga Kanisa nitakuwa mkristo wa kwanza kuingia katika hilo Kanisa.’ Baadaye walipoanza harakati za ujenzi eneo lilionekana dogo wakataka kuongeza nafasi wakanitumia mimi, nikamwombe awaongezee. Akakubali kuwapatia hekari mbili kwa kuwauzia kwa bei ya chini sana akishirikiana na mtoto wake mmoja aitwaye Kinje.

Kama alikuwa hamwamini Mungu kwanini ulimpatia Sakramenti ya Upako wa wagonjwa?

Baada ya kumzika mke wake alizidiwa na kurudishwa hospitali. Alipokuwa hospitali alizidiwa akazimia. Ndipo wakaniita nikaenda kumwona na kweli akawa anapumulia mashine na hawezi kuzungumza. 
Nikasema mimi nitampatia Sakramenti ya upako wa wagonjwa kwasababu yeye ni Mkristo maana miaka kadhaa iliyopita nilizungumza naye nikamuuliza wewe si mkristo? Akasema, ‘Mimi ni mkristo lakini bado ninajiuliza kama kuna Mungu kweli. Hilo tu ndilo nagombana nalo maana falsafa yangu inataka kuhakikisha kama kweli kuna Mungu.’
Katika mazungumzo hayo nilimuliza huwezi kurudia ukristo wako akasema ninaweza lakini siyo sasa. Nilipoona amezimia nikakumbuka maneno yake, ‘nitaamini lakini  siyo sasa.’ Ndipo nikampatia Upako wa wagonjwa nikiamini ndiyo muda wake sasa.
Nilipomaliza nikawambia wauguzi kuwa naondoka lakini akizinduka naomba mniite. alipozinduka akawa yupo kawaida wauguzi wakamueleza nilichofanya. 
Akauliza niko wapi akaamuru niitwe. Wakaja kwangu kunichukua saa tano asubuhi.
Nikamwambia una lolote tuzungumze? Akawasihi wahudumu wote watoke abaki na mimi na nesi mmoja maana naumwa hivyo lazima awepo mmoja kwa dharura.
Nikamueleza nilichokifanya, akaniambia, ‘Monsinyori umefanya vizuri sana na ninakushukuru kwa ulichofanya. Asante sana. Nikamwambia sasa tumalize kabisa urudi kwenye imani.
Akasema Monsinyori ngoja nikueleze kilichonifanya hivi. Mimi nilikwenda Urusi, kule nilikaa miaka mingi nikisoma nikakutana na wakomunisti nikajifunza falsafa kuhusu Mungu yupo au hayupo. 
Wakomunist wakasema hakuna Mungu. Mimi niliwakatalia nikawaambia nihakikishieni kuwa Mungu hayupo. Wakashindwa kunihakikishia. Nao wakanilazimisha kuwahakikishia kuwa Mungu yupo? Nami nikashindwa kuwahakikishia. 
Ndiyo falsafa yangu na nikarudi katika hilo hadi sasa. Wala sisemi kuwa hakuna Mungu lakini falsafa yangu haijanipa jibu kwamba kuna Mungu. Ndiyo hiyo nahangaika nayo.
Kama kuna yeyote anaweza kunihakikishia (kuprove) anisaidie kwaba kuna Mungu niko tayari hadi sasa kuwa Mkatoliki.
 Katika falsafa yangu hiyo, ndipo nikakutana na maandishi ya Mtakatifu Anselmo, alitamka ‘Naelewa akilini mwangu ili niamini,’  nami (Monsinyori) nikamwambia amini ili uelewe. Nikamwambia sasa kama una Imani jaribu kuelewa uamini. Akasema hapana huko siko. 
Tena nilipata sakramenti zote za Kanisa kasoro upadri. Kama unaweza kunihakikishia niambie ili akili ijue. Akili haijui ndiyo maana nahangaika.
Kwabahati mbaya katika mazungumzo akaanza kuchoka Muuguzi akasema huyu amechoka. 
Monsinyori kwa sasa tumuchane . Lakini yeye Kingunge akasema amefurahia upako wa wagonjwa yuko radhi kurudi kwenye Imani Katoliki ananiomba nije tena nimuelezee nielewe. Sina shaka na imani Katoliki. Falsafa tu inanisumbua.
Maneno yake ya mwisho kwangu alisema, Monsinyori mimi nakushukuru ulimzika mama yangu mzazi 1973 mwaka mmoja wa padri wako pale Msimbazi, tena umezika mke wangu . “Nilitamani kumwambia nitakuzika nawewe.” Nikaondoka.
Baada ya siku tatu akazimia tena. Nikawaambia waniite akizinduka lakini wauguzi wakasema amezidiwa sana na baadaye wakanitaarifu kuwa amefariki.  Hapo ndo ikawa kazi na changamoto.
Nikamuambia Askofu wangu Euzebius Nzigilwa kuwa mazungumzo yetu na Kingunge na kwamba alipata baadhi ya sakramenti. 
Askofu Nzigilwa akasema nisubiri azungumze na maaskofu wengine.
Ndipo baadaye ikaamuliwa kuwa kwa heshima ya mkewe na watoto wake waliokuwa wanamuombea abadilike, kwa heshima aliyokuwa anaonesha kwa Kanisa maana hakuwa mpinzani wa Imani tusimtupe tu maana hakuwa mpinzani.
Pia hatuwezi kumpeleka Kanisani kwa Misa ya mazishi maana alikuwa haendi Kanisani na hatuwezi kumtupa kama mpagani kabisa.
Tutamtuma Katekista afanye ibada kwenye maziko. Nikamchukua Katekista wangu nikamueleza, aende nyumbani na baadaye makaburini akafanye ibada.

Kama ndugu yake wa nini hukushiriki kama mtu wa kawaida?
 Nilijihadhari kwa maswali mengi. na hata nilipewa ushauri na askofu maana nikienda kama padri kwenye ibada wangeweza kuzusha mengi.

Na Sarah Pelaji


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU