Kanisa lafungua kitengo cha Magonjwa ya Mfumo wa Chakula Dodoma

Minja-DODOMA.
Kanisa Katoliki hivi karibuni limefungua kitengo cha Magonjwa ya Mfumo wa Chakula (ENDOSCOPY) katika Hospitali ya Mtakatifu Gemma iliyoko Miyuji Dodoma.
Wakati wa ufunguzi wa jengo hilo, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaiya ameiasa jamii kuwa na mwamko wa haraka kuchangia huduma za afya pale zinapohitajika ili kunusuru maisha ya watanzania.
Pia iwe na mipango ya kudumu ya huduma za afya kwa maendeleo.
Pamoja na hayo Askofu Mkuu Kinyaiya amesema ufunguzi wa kitengo hicho ni muhimu kwa wananchi wa Dodoma kwani wamekuwa wakisumbuka kwa muda mrefu na kuwataka madaktari katika Hospitali hiyo kuwa na moyo wa huruma katika kuwahudumia wagonjwa.
Aidha amewasisitiza kulinda vifaa tiba katika kitengo hicho.
Kwa upande wake Mganga Mkuu Msaidizi katika Hospitali hiyo Sista Dkt. Theodora Mwasu amesema kuwa,wazo la kuanzisha Hospitali hiyo lilikuwa ni kwa ajili ya kuwatibu masista wagonjwa na wazee ambapo kwa sasa hospitali hiyo inatoa huduma kwa jamii nzima.
Hata hivyo Sista Theodora ametaja baadhi ya changamoto zinazoikabili Hospitali hiyo ikiwa ni pamoja na uhaba wa wafanyakazi, chumba cha kuhifadhia maiti, ubovu wa barabara inayoingia hospitalini hapo na uhaba wa vifaa tiba kutoka bohari kuu ya dawa.
Kutokana na hayo Mgeni Rasmi katika ufunguzi huo kwa niaba ya Waziri wa Kazi, Ajira na Vijana Anthony Mavunde, Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Deo Ndenjembi amesema kuwa, serikali iko mbioni kumaliza tatizo la uhaba wa wafanyakazi katika hospitali zote na kuwataka wananchi wa Dodoma kuwa na mwamko wa kuitumia Hospitali ya Mtakatifu Gemma kwani inajitosheleza katika kutoa huduma za afya.
Pamoja na hayo amesema kuwa, mwamko mdogo wa wakazi wa mji wa Dodoma unachangia kudidimiza maendeleo ya hospitali hiyo na    kuwataka wananchi kuwa kichocheo cha maendeleo hospitalini hapo kwa maendeleo ya Taifa kwa ujumla.
Wazo la kuanzishwa kwa kitengo cha magonjwa ya mfumo wa chakula hospitalini hapo lilibuniwa na Sista Gemma Mkondoo kutokana na msukumo alioupata kwa kusafirisha wagonjwa mara kwa mara kwenda kutibiwa Dar Es Salaam huku wakiwa wadhaifu kiafya.
Hali hiyo ilimlazimu kuomba msaada kwa rafiki zake waitaliano ambao wamesaidia kufanikisha huduma hiyo kwa karibu zaidi na jamii.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU