Wizara ya Elimu yatahadharishwa mabadiliko ya mara kwa mara

Na Eliya Mbonea, Kilimanjaro
ASKOFU wa Kanisa la Anglikan Tanzania, Dayosisi ya Mount Kilimanjaro (DMK), Dk. Stanley Hotay ameishauri Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kutofanya mabadiliko ya mara kwa mara katika Sera ya elimu nchini.
Kauli hiyo ameitoa mjini Moshi hivi karibuni wakati wa Ibada ya kuweka wakfu jina la Shule ya Bishop Alpha Memorial High School iliyohudhuriwa na mgeni rasmi Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia William Ole Nasha.
Ibada hiyo ilifuatiwa na changizo la kuchangia fedha kwa ajili ya ujenzi wa Bwalo la chakula shuleni hapo ambapo kiasi cha Sh milioni 56.3 zilikusanywa huku Naibu Waziri Ole Nasha akichangia Sh milioni 8.
Akizungumza baada ya kumalizika kwa ibada ambayo mahubiri yake yalitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Singida Dk. Rehema Nchimbi, Askofu Dk. Hotay amesema mabadiliko ya mara kwa mara yamekuwa yakiyumbisha elimu.
“Wizara ya elimu fikirini kwa upya sera ya elimu mnawezaje kumsaidia mtoto wa Tanzania, mabadiliko haya ya kila wakati hayamsaidii mwanafunzi,” amesema Askofu Dk. Hotay.
Kwa upande wake Naibu Waziri Ole Nasha akizungumza kwenye uzinduzi wa jina jipya la sekondari hiyo amesema kuwa, serikali inatambua mchango unaotolewa na shule binafsi na za Taasisi za dini katika maendeleo ya sekya ya elimu.
“Sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 inasema serikali itaweka mazingira bora na kuhakikisha kuwa sekta ya elimu na mafunzo inatoa rasilimaliwatu ya kutosha na mahiri ili kukidhi mahitaji ya sekta mbalimbali kwa maendeleo ya taifa.
“Ili kufikia azma hiyo ushiriki wa wadau wengine kama shule binafsi na taasisi za dini ni muhimu, hivyo Serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa shule hizi ili ziweze kufikia malengo ya kuanzishwa kwake,” amesema Naibu Waziri Nasha.
Akifafanua kuhusu kupanua kwa fursa za elimu nchini, Naibu Waziri Ole Nasha alisema mpango wa ElimuMsingi bila malipo umewezesha zaidi ya wanafunzi 462,530 kuingia darani kutoka mwaka 2015 hadi 2017.
“Serikali inatoa kila mwezi Sh Bilioni 23 kwa ajili ya kutekeleza mpango ElimuMsingi bila malipo. Na mpango huu umeongeza wanafunzi walioandikishwa darasa la kwanza kutoka 1,386,592 mwaka 2015 hadi 1,849,122 mwaka 2017,” amesema Naibu Waziri Nasha.
Aidha serikali imefanya pia ukarabati na ujenzi wa miundombinu ya shule za msingi na sekondari kupitia mpango wa lipa kulingana na matokeo (P4R), ikiwa ni pamoja na ukarabati wa shule zote kongwe 88 nchini.
Kupitia Ibada hiyo Naibu Waziri Ole Nasha ametolea pia ufafanuzi suala la wazazi na walezi kuchangia katika maendeleo ya elimu akisema kwamba serikali hajiakataza.
Amesema ni muhimu kuzingatia maelekezo ya Waraka wa Elimu namba 3 wa mwaka 2016 katika uchangiaji kwa kuhakikisha kuwa michango yote inaratibiwa na Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri kama ilivyo kwenye michango mingine ya maendeleo.
Wanafunzi wasifungamanishwe na mchango wa aina yeyote kwa maana ya kumzuia kuhudhuria masomo au kumnyima cheti kwa kigezo cha mzazi au mlezi kushindwa kuchangia,” amesisitiza.
Akisoma taarifa ya shule hiyo Afisa wa uongozi shuleni hapo, Fadhili Chibago aliyataja malengo ya shule hiyo iliyojulikana awali kama Pasua Sekondari, kuwa ni kurudisha matumaini mapya kwa wanafunzi waliokosa nafasi za kidato cha kwanza kwenye shule mbalimbali za serikali.
“Shule yetu imekuwa ikijitahidi katika ufaulu kitaaluma na ukilinganisha na aina ya wanafunzi tunawapokea kama shule ya kanisa.
“Mfano mwaka 2015 kidato cha nne shule ilishika nafasi ya 79 katik ya shule 292 kimkoa na 906 kati ya shule 3,452 kitaifa. Pia jumla ya wanafunzi 23 walichaguliwa kwenda kidato cha tano kati ya wanafunzi 70 waliofaulu,” alisema Chibago.
Awali Mkuu wa Mkoa Dk. Nchimbi alisema kuwa  Kanisa la Anglika kumiliki na kuendesha shule hiyo ni moja ya dhamana kubwa waliyokabidhiwa ya kuandaa taifa lijalo.
“Elimu inayotolewa hapa itawapatia vijana wetu uelewa mpana wa kuelewa dunia inakwendaje wao kuwa na uhakika wa kuishi mahali popote,’ amesema Dk. Nchimbi.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU