Pinda aongoza harambee ya ujenzi wa kituo cha hija Ifucha



Na Thomas Mambo- Tabora.
Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo  Pinda amewahimiza waamini wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora na wenyenji wa Kijiji cha Ifucha Nholo Tabora kutunza uoto wa asili na Mazingira ili kuenzi kazi ya Uumbaji wa Mwenyezi Mungu.
Rai hiyo ameitoa hivi karibuni alipotembelea eneo la Ifucha Tabora mahali ambapo Jimbo Kuu Katoliki Tabora linaendelea na ujenzi wa kituo cha Huruma ya Mungu .
Mh. Pinda alipokea taarifa iliyotolewa na Padri Mhandisi wa Jimbo Kuu Gosbert Kalaso iliyosema kuwa kituo hicho kutagharimu kiasi cha fedha kisichopungua shilingi milioni 717 za kitanzania.
Aidha Padri Kalaso amesema hadi ujenzi wa kituo ulipofikia , kituo kimeshagharimu shilingi milioni sitini na nne, laki mbili na ishirini na tano (64,225,000).
Baada ya kupokea maelezo hayo, Mh. Pinda aliwatoa hofu wanatabora hao na kusema kituo kitakamilika kwa wakati na akapendekeza mikakati iwekwe ikiwemo kuandaa na kupanga siku maaalumu ili kufanya harambee itakayoshirikisha watu ndani na nje ya mkoa wa Tabora.
Akielezea lengo la kituo hicho, Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora, Mhashamu Paul Ruzoka amesema kuwa, kituo hicho ni kwa ajili ya kupata eneo la kupata utulivu wa moyo kama jina lilivyo yaani “Ifucha nholo” watu watapata sehemu wanayoweza kusikia na kusikiliza sauti ya Mungu.
Sanjari na ujenzi wa kituo hicho cha kiroho, Jimbo Kuu Tabora limesaidia wenyeji wa eneo hilo kwa kuwagawia wanakijiji mbegu ya kisasa ya mihogo inayokinzana na magonjwa na kuvumilia hali ya hewa jambo lilisababisha  mbegu hiyo kuitwa,”Mkombozi.”
Aidha jimbo pia limesaidia kutoa elimu ya kilimo  na ufugaji kwa kaya zisizopungua 120, kwa kutumia kiasi cha milioni 400 pesa za kitanzania.
Jimbo Kuu Tabora limeanzisha kilimo cha korosho ili kuwasaidia wanatabora kubadili fikra na kuanzisha kilimo hicho cha biashara. 
Jimbo pia limepanda miti ili kuwa kielelezo cha utunzaji mazingira na kuhamasisha wananchi kuotesha miti na kuchana na tabia mbaya ya kukata miti hovyo.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mkuu wa Wilaya  ya Tabora mjini Mwl. Queen Mlozi alitanabaisha fursa zinazopatikana mkoani hapo ambazo kila mwanatabora anapaswa kuzichangamkia kwa wakati yaani;  ujenzi wa reli ya kisasa, uhakika wa usafiri wa ndege, ujio wa maji toka ziwa Victoria, ujenzi wa barabara za lami unaoendelea ili kuufungua mkoa wa Tabora na mikoa mingine jirani na uwepo wa makao makuu ya Serikali hapo Dodoma.
Katika hafla hiyo fupi, Mh. Pinda  aliendesha harambee na kupata kiasi cha shilingi milioni 12,920,000 zikiwa ahadi na pesa taslimu.
Pia ameomba utaratibu ufanyike haraka ili harambee nyingine ifanyike mwaka huu (2018) ili Kanisa la Tanzania litakapo adhimisha Kongamano la Ekaristi Takatifu kitaifa 2020 kituo kiwe katika hatua nzuri. 
Jimbo kuu Tabora linatarajia kujenga shule, zahanati, kumbi za mikutano, nyumba ya kulala wageni na nyumba ya utulivu au “rehabilitation centre.”


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU