Vijana ni utajiri wa Kanisa-Padri asisitiza

Na Stanslaus Likomawagi, Dodoma
Vijana ndiyo utajiri wa Kanisa hivyo wajitume kulitegemeza Kanisa hasa kuiishi miito mitakatifu.
Vijana Wakatoliki wametakiwa kuitikia miito mitakatifu wanayoitiwa na Mungu kwani Kanisa bado lina mahitaji makubwa katika kuitangaza Injili.
Aidha wametakiwa kuepuka tamaa za dunia ambazo zinawapumbaza na kukataa kuitikia sauti ya Mungu, badala yake kuomba ushauri kwa Mapadri na maaskofu ili kupata msaada wa kufikia safari yao ya miito.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Miito wa Shirika la Mateso ya Yesu (PASSIONIST FATHERS) Padri Erasto Kamugisha alipokuwa akizungumza na Gazeti Kiongozi katika  mahojiano maalumu kuhusu changamoto ya miito ya Upadri kwa vijana katika karne hii.
Padri Kamugisha amesema kuwa, Vijana wanaitwa na Mungu na wengi wana wito wa Upadri  lakini wapo wanaopata vikwazo kufikia safari yao kutokana na mazingira wanayoishi.
Hao wasipokuwa na msaada ama kukosa nidhamu ya kiimani hawawezi kujiunga na seminari ama hata wakijiunga na seminari wataacha katikati.
“Kanisa bado linahitaji watenda kazi ,ni maamuzi ya Vijana kukubali wito wa Upadri waliotiwa na Mungu na jambo kubwa wajikite katika sala na kuomba ushauri kwani hata mimi nilisaidiwa katika kufikia wito wangu,” amesema Padri huyo.
Kuhusu changamoto zinazowakabili Vijana Padri Kamugisha amefafanua kuwa Jimbo kuu Katoliki Dodoma kupitia Shirika la Mapdari wa Mateso ya Yesu limeendelea kuwasaidia Vijana kwa kuwapa elimu ya kujitambua na kuachana na mambo ya kishetani kama vile matumizi ya dawa za kulevya, uasherati na mambo mengine ambayo ni dhambi kwa Mungu.
Amesema,  wamekuwa wakiandaa makongamano mbalimbali ya vijana na kuwafundisha Ujasiriamali,lengo likiwa ni kuwapa ufahamu Vijana katika kukabiliana na tatizo la ukosefu wa ajira.
“Mpaka sasa Vijana zaidi ya 200 walikuja katika semina ambayo tuliiandaa na tumeona matokeo kwani wengi wao mara baada ya semina hiyo walionesha mabadiliko na wengine kuanza kuonesha nia ya kupenda miito ya upadri na utawa na wengine kuachana na mazingira waliyokuwa wakiishi zamani,” amesema.
Amewasihi Vijana kuendelea kutambua thamani yao ndani ya Kanisa na taifa kwa ujumla na kujituma katika kufanikisha malengo yao ili Kanisa na jamii iweze kunufaika na mchango wao kwa siku za baadae.

Pia amewataka Mapadri na Watawa wa kike na kiume kuendelea kuwalea na kuwatia moyo Vijana wanapowafuata  kuomba ushauri pale wanapokumbana na vikwazo ili wawe imara na kuendelea na safari yao ya wito.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU