‘Kiongozi mwadilifu na mchaMungu aepuke ubinafsi na chuki’

Na Rodrick Minja, Dodoma
WAZIRI Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda amesema kuwa viongozi wanatakiwa kuwa waadilifu na wacha Mungu badala ya kufanya kazi kwa ubinafsi, chuki na kula rushwa. Ametoa kauli hiyo alipokuwa akifunga Kongamano la Maombi ya kuliombea taifa pamoja na viongozi lililofanyika mjini Dodoma.
Pinda amesema kuwa ili uweze kuwa na taifa lenye viongozi wazuri wasiojihusisha katika vitendo vya rushwa na kuwa na utawala bora ni lazima kupata viongozi ambao ni wacha Mungu na wenye hofu ya kimungu.
Amesema kuwa viongozi wote ndani ya serikali, kwenye vyama vya siasa pamoja na kwenye taasisi mbalimbali lazima wafanye kazi zao kwa hofu ya Mungu kutoka moyoni na siyo maigizo, ili kuweza kuwapatia wananchi maendeleo.
“Maombi ambayo yamekuwa yakifanyika kwa ajili ya kuliombea taifa pamoja na viongozi mbalimbali yawe chachu ya kuwaletea maendeleo wananchi na viongozi wanatakiwa kutambua wazi kuwa ili nchi iweze kuwa na maendeleo ni lazima kuwepo na utawala bora. Kama viongozi watafanya kazi zao kwa uadilifu ni wazi kuwa kila Mtanzania ataweza kujivunia na kujiongezea kipato kutokana na rasilima zinazotokana na vyanzo mbalimbali ambavyo Mungu ameviweka katika nchi yetu” amesema Pinda.
Mbali na hayo Pinda ameongeza kuwa kuna haja ya kuanzishwa kwa vikundi vya maombi kuanzia ngazi ya shule za msingi hadi vyuo vikuu ili kuwekeza njia bora ambayo watoto watakiwa waaminifu katika utendaji wao wa kazi kwa misingi ya kujitenga na ufisadi, rushwa pamoja na wizi wa mali ya umma.
Kwa upande wake aliyekuwa Makamu Rais wa Benki ya Dunia Kanda ya Afrika, Dk.Oby Ezekwesili kutoka nchini Nigeria akitoa mada katika kongamano la maombi juu ya utawala bora, uwazi na uwajibikaji amesema kuwa ili nchi iweze kusonga mbele ni lazima kuwa na viongozi ambao wanazingatia misingi ya utawala bora.
Mbali na kuwepo kwa utawala bora pia Dk. Ezekwesili amehimiza uongozi ambao unazingatia masuala ya utekelezaji wa demokrasia, uwazi, uwajibikaji pamoja na utawala bora ili kila mmoja aweze kujivunia rasilimali za nchi.
Katika hatua nyingine kiongozi huyo amehimiza utoaji wa elimu juu ya kutunza maliasili za nchi huku suala zima la uzalishaji likipewa kipaumbele kwa njia ya kutunza vyanzo vyote vya mapato ikiwa ni pamoja na kujiepusha na masuala ya rushwa, ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU