Trilioni 1 kulipa madeni 2017/2018

Na Lilian Lundo, Dodoma
SERIKALI imetenga jumla ya shilingi Trilioni 1 kwa mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya kulipa madeni mbalimbali ya watoa huduma, wazabuni na watumishi wa Umma.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO) Dkt. Hassan Abbasi ameeleza hayo Mjini Dodoma alipokuwa akiongea na waandishi wa habari juu ya utekelezaji wa miradi na ahadi mbalimbali za Serikali.
“Kati ya shilingi Trilioni 1 zilizotengwa kulipia madeni kwa mwaka huu wa fedha, shilingi Bilioni 896.3 zimeshalipwa kwa watoa huduma, wazabuni na watumishi wa Serikali,” amesema Dkt. Abbasi.
Amesema hesabu hiyo inajumuisha shilingi Bilioni 43 ambazo zimelipwa Februari, 2018 ikiwa ni malimbikizo ya wafanyakazi  wa sekta ya Umma. “Madeni mengine uhakiki unaendelea na yataendelea kulipwa siku zijazo na tutawajulisha,” amefafanua Dkt. Abbasi.
Vile vile amesema kuwa Serikali ina mkakati wa kuwaondoleaa adha ya usafiri wananchi wa maziwa makuu likiwemo Ziwa Nyasa, Tanganyika na Viktoria ambapo kwa upande wa Ziwa Viktoria,  mkandarasi amepatikana na majadiliano ya mwisho na kusaini mkataba na kampuni ya STX ya Jamhuri ya Korea vitafanyika mwezi huu kwa ajili utengenezaji wa meli mpya itakayokuwa na uwezo wa kubeba abiria 1,200 na mizigo tani 400.
Kwa upande wa Ziwa Tanganyika zabuni kwa ajili ya utengenezaji wa meli mpya ya abiria na mizigo itatangazwa mwezi huu. Meli hiyo mpya itakuwa na uwezo wa kubeba abiria 600 na tani 400 za mizigo na italeta mapinduzi makubwa katika usafiri ziwani hilo.
Aidha Dkt. Abbasi amesema Julai mwaka huu nchi itapokea ndege kadhaa mpya ikiwemo Boeing Dreamliner na ukarabati wa viwanja vya ndege vya Kitaifa, Kimataifa na Kimkoa unaendelea kwa kasi kote nchini.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU