Vijana wasitumike kama vibaraka wa wanasiasa

Na Pascal Mwanache

KUELEKEA maadhimisho ya Jumapili ya matawi ambayo ni sikukuu ya vijana, wito umetolewa kwa vijana nchini kuielewa siasa kwa undani badala ya kutumika na watu wachache wenye nia ya kujinufaisha wenyewe.
Wito huo umetolewa na Mratibu wa Vijana Taifa katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Padri Liberatus Kadio huku akiakisi ujumbe wa Baba Mtakatifu Fransisko kwa maadhimisho ya siku ya 33 ya vijana ulimwenguni, na kuwataka vijana nchini kuwa makini na namna wanavyojikita katika shughuli mbalimbali za kisiasa.
“Elimu yetu haiwaandai vijana kuwa wanasiasa wazuri, na hii inasababisha vijana wengi kujiingiza katika siasa wakiwa na dhana kwamba kuwa mwanasiasa ni njia ya kuwa tajiri. Wanasahau kuwa siasa ni njia ya kuwatumikia watu yaani kutumika. Shida hutokea pale ambapo wengi hawapati kile walichokitarajia, matokeo yake kwa shauku hiyo ya utajiri wanajikuta wakitumika kama vyombo vinavyowafaidisha wengine” amesema. 
Aidha ametahadharisha kuwa vijana wanaporuhusu kutumika na wanasiasa, wao ndiyo wanakuwa waathirika wakubwa, kwa kuwa wanaowatumia wengi hawana nia njema ya kuwafanya wawe wazalendo kwa taifa bali vibaraka wao.

Vijana na hofu ya maisha
Akiuelezea ujumbe wa Papa kwa vijana mwaka 2018 unaoongozwa na maneno ya Mwinjili Luka “Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu”, Padri Kadio amesema kuwa vijana nchini wanakabiliwa na hofu ya maisha inayochangiwa na mfumo wa elimu ambao haumuandai kijana ajiamini na ajitegemee katika kukabiliana na maisha, na badala yake unamfanya awe tegemezi.
“Mfumo wa elimu unamfanya kijana asubiri kuajiriwa, huku akiwa na matarajio lukuki kama vile kuishi maisha bora, kumiliki mali na kupata kazi nzuri. Sasa inapotokea kijana amekosa fursa ya kuajiriwa licha ya kuwa na elimu ya kutosha hapo ni lazima awe na hofu ya maisha” ameongeza.
Pia ametaja hofu nyingine zinazowakabili vijana kuwa ni pamoja na hofu ya imani inayosababisha vijana kuhama makanisa wakitafuta utajiri, hofu ya kutopendwa kwa sababu ya kukosa fedha, mali au nafasi na hofu ya kukataliwa.
Akitoa ushauri wa namna ya kukabiliana na hofu hizo Padri Kadio amewataka vijana kuwa na ujasiri wa kuyaweka mambo yote mikononi mwa Mungu, huku wakiwa na uthubutu wa kutumia elimu, ujuzi na nguvu walizonazo katika kukabiliana na changamoto za maisha.
“Wao ni kanisa la leo na kesho, hivyo uthubutu wao ndiyo utasababisha tuwe na mapadri wazuri, watawa wazuri, wazazi wazuri na waamini imara. Yote wayaweke mikononi mwa Mungu na wawe tayari kujifunza kupitia maandiko matakatifu” ameongeza.

Vijana na kitubio
Akitoa tathmini kuelekea kilele cha Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara Padri Kadio amesema kuwa vijana wanapaswa wahimizwe juu ya umuhimu wa kukaa karibu na sakramenti ya kitubio na sakramenti ya Ekaristi Takatifu na kuachana na dhana kwamba sakramenti hizo ni kwa ajili ya wazee.
Amesema kuwa kitubio ni sakramenti inayompa kijana ujasiri na uthubutu wa kutenda yaliyo mema hivyo hawana budi kuijongea na kuachana na dhana potofu kuwa hakuna haja ya kuungama kwa padri au dhana ya kujiungamisha.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU