Ask.Nzigilwa aonya kuhusu kulipiza kisasi, kinyongo

Na Agens Shayo, Dar es Salaam
Waamini wakatoliki nchini, wameshauriwa kutenda mambo yale wanayoyaona kuwa ni madogomadogo katika maisha yao ya kila siku, kwa kuwa hayo yanayoonekana madogo ndiyo yanamfikisha mtu mbinguni.
Wito huo umetolewa hivi karibuni na Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki  Dar es Salaam, Mhasham Eusebius Nzigilwa, wakati wa Ibada ya Misa Takatifu ya Maziko ya Emmanuel Muunga, Mmisionari wa Shirika la Utoto Mtakatifu jimboni humo iliyofanyika katika Parokia ya Hananasifu.
Askofu Nzigilwa amesema kuwa watu walio wengi wana kawaida ya kudharau mambo madogo madogo, huku wakiamini kuwa hayana uhusiano katika maisha yao ya hapa duniani na mbinguni, hali ambayo amesema haifai katika maisha ya mwamini mkatoliki.
Akimzungumzia Emmanuel Muunga, Askofu Nzigilwa amesema kuwa, marehemu enzi za uhai wake alijitahidi sana katika kuziishi vyema sakramenti  za Kanisa Katoliki, ambazo alijaliwa kuzipata ikiwa ni Ubatizo, Kipaimara na Ndoa Takatifu, ambapo katika maisha yake yeye kwa kushirikiana na  mke wake na watoto wake, walijitoa kiaminifu katika umsionari wa uinjilishaji kupitia Shirika la Kipapa la Kimisionari Jimbo Kuu Dar es Salaam.
Aidha, ameongeza kwa kuwakumbusha waamini suala zima la msamaha, huku akihusisha na kipindi hiki cha kwaresma kinachosimamia toba na msamaha akisema;
 “Hakika nawaambieni msipowasamehe watu makosa yao, hakika baba yenu wa mbinguni hatawasamehe milele, pia tusiwe na tabia ya kuweka vinyongo wala kulipiza kisasi, tunapaswa kutambua kuwa sisi sote tunahitaji msamaha na huruma ya Mwenyezi Mungu,”Askofu Nzigilwa.
Akiwasilisha salamu za Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinal Pengo Askofu Nzigilwa amesema kuwa, Mwadhama amepokea taarifa za msiba huo kwa masikitiko makubwa sana na hivyo ametoa pole zake za dhati kwa familia ya Mzee Gerald na Mama Muunga, pamoja na mke na kwa watoto wa marehemu kwa kifo cha mpendwa wao Emmanuel Muunga.
“Hii familia huwa inamfurahisha sana, katika matukio ya kijimbo familia hii imekuwa mstari wa mbele daima, kila anapoiona huwa inambariki sana, na amewataka kupitia tukio hili wasitetereke bali waendelee kudumu katika Ibada na kujitoa zaidi kwenye mambo ya Mungu”, Askofu Nzigilwa alipowasilisha salamu za Baba Mwadhama.
Kwa Upande wake Paroko wa Parokia ya  Kimara Mtoni, alikokuwa anasali marehemu enzi za uhai wake, Padri Patrick Msumba mmisioanari wa shirika la Marianhill amesema kuwa, kila mwamini anapaswa kujifunza kuwa hata akiwa na nguvu kiasi gani, itafika wakati atahitaji tuu japo kuinuliwa juu au kushikwa mkono na mtu mwingine ili usonge mbele, hivyo amewataka watu kuishi kwa upendo na ushirikiano.
Amezungumzia namna alivyomfahamu Emmanuel na familia yake yote, anaamini kabisa kwamba marehemu alijitahidi sana katika kutimiza wajibu wake katika kutenda yale yote aliyopaswa kuyatenda, na kwa wakati, hali ambayo amedai kuwa imeacha alama ndani ya Kanisa la Kimara, na wameahidi kuienzi hiyo hali pamoja na familia ya marehemu kwa muda wote.
Padri Timoth Maganga Nyasulu ambaye yeye ni Mkurugenzi wa Mashirika ya Kipapa Jimbo Kuu katoliki Dar es salaam, na Paroko wa Kanisa la Bikira Maria Mama wa Huruma Mbezi Beach, amesema kila Mwamini mbatizwa anapaswa kukitazama kifo na kisha kujitafakari upya katika mwenendo wa maisha yake ya kila siku, huku akisisitiza kuwa ni vyema kila mmoja akatimiza wajibu wake kwa Umma, kwa Kanisa na kwa ulimwengu mzima.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mashirika ya Kipapa Taifa, Padri Jovitus Mwijage, katika salamu zake za rambirambi amesema kuwa, kila mmoja anapaswa kutambua kuwa uwepo wake hapa duniani anamtafuta Mungu, hivyo hana budi kuishi kadiri ya maongozi ya Mwenyezi Mungu.
“Hata Emmanuel  alikuwa akimtafuta Mungu, na leo tunapomsindikiza tunaamini kuwa anakwenda kupata zawadi yake  kwenye maisha ya milele”.
Emmanuel Gerald Mokiwa Muunga, aliyekuwa Mmisionari wa Shirika la Kipapa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, alizaliwa 05.12.1981, na kufariki tarehe 24.02.2018, katika Taasisi ya Mifupa ya Hospitali Ya Taifa Muhimbili, ameacha mke mmoja Bi Maria Muunga na watoto wawili wakike Precious na Princess Emmanuel Muunga, ambao wote ni Wamisionari wa Shirika la Utoto Mtakatifu Jimboni humo


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU