WAOMBEENI WATUMISHI WA MUNGU-ASKOFU MSONGANZILA



n Na Veronica Modest, Musoma.
WAKAtoliki jimboni Musoma wameaswa kuhakikisha wanawaombea  mashemasi, mapadri na watawa, ili waweze  kudumu  na kuziishi nadhiri zao, kama walivyotoa ahadi kwa Mwenyezi Mungu na mbele ya Kanisa Katoliki.
Hayo yamesemwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila wakati wa ibada Takatifu ya kutoa daraja ya Ushemasi kwa Flateri Thomas Nsabamusabe Samwel na Flateri Gabriel Boli Wadan, iliyofanyika hivi karibuni katika Parokia ya Mtakatifu Yohane Mbatizaji Nyamiongo jimboni hapa.
Askofu Msonganzila amesema kuwa   ni wajibu wa waamini wakatoliki kuhakikisha wanaweka muda wa kuwaombea wahudumu wa Kanisa ambao wanajitoa kwa Mungu kwa ajili ya kulitumikia Kanisa na jamii kwa ujumla, ili waweze  kuziishi na kudumu katika nadhiri zao, kwa kuwa bila maombi  hawawezi kufanya chochote.
“Niwaombe wakristo wa jimboni Musoma, tusisahau kuwaweka katika maombi mashemasi wetu, mapadri, watawa na wanovisi, ili wazidi kuimarika kiroho na kimwili katika kumtumikia Mungu, kwani hii ni zawadi ya wito kwa vijana wetu na pia tunamshukuru Mungu kwa kutupatia nafasi hii ya walelewa na vijana kuonja miito hii ndani ya Kanisa letu,” amesema Askofu Msonganzila.
Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Yohane Mbatizaji Nyamiongo Padri Bosco Kiyuga amesema kuwa  wanamshukuru Mungu ndani ya shirika lao la Wana wa Moyo Safi wa Bikira Maria (WAKLARETI) kwa karama ya Utumishi wa neno la Mungu katika kueneza neno hilo kwa njia mbalimbali ikiwemo uchapishaji wa vitabu na majarida.
Padri Kiyuga amesema kuwa  kwa sasa shirika hilo limeadhimisha miaka 25 ya uwepo wake katika nchi tatu za AfrikaMashariki yaani Kenya,Uganda na Tanzania ambapo kwa Tanzania shirika hilo lina jumuiya jimboni Musoma, Mwanza, Dar es Salaam, Morogoro na Moshi, na tangu lianzishwe linaadhimisha miaka 168, hivyo wanamshukuru Mungu kwa Neema na Baraka nyingi alizowajalia, baada ya kuanzishwa na Mtakatifu Antoni Maria Claret na mapadri wengine watano huko Vic nchini Hispania mwaka 1849.
Kwa upande wake shemasi Gabriel Wadan amesema kuwa safari yake ya wito shirikani ilianza  mwaka 2007 alipoanza malezi ya kwanza huko Kupang Indonesia na aliweka nadhiri zake za kwanza Julai 16, 2011 ambapo amepokea daraja ya Ushemasi Julai 27, 2017 kutoka kwa Askofu Michael Msonganzila wa Jimbo Katoliki Musoma katika Parokia ya Mtakatifu Yohane Mbatizaji Nyamiongo, ambapo anamshukuru Mungu kwa zawadi hiyo huku akiahidi kuitumikia hadi kufa kwake.
Naye Shemasi  Thomas  Nsabamusabe amesema kuwa safari yake ya wito shirikani ilianza  Septemba 2007 alipojiunga  na malezi ya kwanza  Makoko Centre jimboni Musoma na aliweka nadhiri zake za daima Julai 26 mwaka 2017, na amepokea daraja ya Ushemasi Julai 27, 2017 katika parokia ya Mtakatifu Yohane Mbatizaji Nyamiongo kutoka kwa Mhashamu Michael Msonganzila  wa Jimbo Katoliki Musoma ambapo amewaomba waamini wa Jimbo hilo kuendelea kuwaombea kwa Mungu ili waendelee kuziishi na kudumu katika wito wao kama walivyoahidi mbele ya Mungu na mbele ya Kanisa Katoliki.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU