Kanisa Katoliki lawa msaada mkubwa kwa wakazi Mtwara

n Na Doreen Aloyce, Mtwara

IMEELEZWA kuwa uwepo kwa Kanisa Katoliki katika Jimbo Katoliki Mtwara umekuwa msaada mkubwa wa maelfu ya waamini kutokana na wengi wao kumjua Kristo na kupata huduma za Kiroho ndani ya maisha yao.
Kauli hiyo imetolewa kwa nyakati tofauti  na baadhi ya mapadri wa Jimbo hilo wakati wakizungumza na gazeti la Kiongozi lilipotaka kujua Historia mbalimbali juu ya Imani Katoliki kwa waamini.
Padri Nixon Mbila ambaye ni Paroko wa Parokia ya Watakatifu Wote Jimbo Katoliki Mtwara pamoja na Padri Silvanus Chikuyu Paroko wa Parokia ya Watakatifu Petrol na Paulo Mitume  wamesema kuwa Parokia ya Watakatifu Wote  ilianzishwa mwaka 1957 na Parokia ya Watakatifu Petrol na Paulo Mitume ilianzishwa mwaka 2006 ambapo kumekuwepo na mafanikio makubwa kwani waamini wengi na wengine kutoka madhehebu tofauti wamekuwa wakifika parokiani hapo kupata huduma za kiroho na kimwili tofauti na hapo awali.
Wamesema kuwa wapo waamini ambao hapo awali walikuwa wakipata matatizo na wengine walipofariki hawakupata huduma za Sakramenti lakini kwa sasa wanajivunia kwa jinsi mapadri ambavyo wamekuwa nao bega kwa bega kuwapa msaada.
Wamesema kuna idadi kubwa ya waamini wanaotoka Dini zingine kuja kupata huduma za kikanisa, kuongezeka kwa uandikishwaji wa Sakramenti ya Ndoa, kuwepo kwa Sakramenti ya Kipaimara, kuanzishwa shule za Chekechea pamoja na kupanua makanisa.
Vile vile Kanisa Katoliki limefanya kazi kubwa ya kutatua migogoro mbalimbali ya kifamilia katika jamii, hivyo kila parokia kuwa na Kamati imara ambayo inashughulikia mambo hayo.
Aidha kwa ushirikiano wa waamini wamekuwa wakifanya kazi za kijamii hususani kutoa misaada ya chakula, mavazi na fedha kwa watoto yatima, wajane, wafungwa, na wote wasiojiweza huku wakitoa huduma ya kuwaombea wagonjwa hospitalini jambo ambalo limekuwa msaada mkubwa kwa jamii.
Mbali na mafanikio hayo kumekuwa kukijitokeza changamoto mbalimbali za kutaka kurudisha nyuma imani Katoliki kwa madai kwamba baadhi ya vijana wakatoliki husahau imani zao.
Hata hivyo mbali na changamoto hizo kumekuwepo mipango mizuri ya kuhakikisha waamini hawapotei kwani wamekuwa wakiimarisha Jumuiya ndogondogo, kuimarisha utume wa  vijana wadogo kwa kuwapa Semina mbalimbali na makongamano ambayo yanawafundisha kukaa katika imani zao na kwa kiwango kikubwa vijana na waamini wamekuwa na uelewa juu ya imani yao.
Padri Silvanus Chikuyu Paroko parokia ya Watakatifu Petrol na Paulo amesema kuwa parokia yake wana miradi ya shamba la ndizi, minazi na machungwa huku wakiwa na malengo makubwa ya kuanzisha miradi ya vibanda vya biashara.
Hata hivyo amewataka waamini kuwa karibu mbele za Mungu kwa kumtolea sadaka inayompendeza kutokana na parokia hiyo kutokuwa na msaada kutoka nje huku akiwasihi baadhi ya wakristo kuacha kasumba ya kuvaa Rozali kama pambo bila kusali kwani kumekuwepo na vijana wengi ambao hawajui kuitumia.
Naye Paroko Nixon Mbilla wa parokia ya Watakatifu Wote amesema kuwa parokia ina miradi mbalimbali ikiwemo ya kukarabati nyumba ya mapadri ambayo wanaendelea nayo kutokana na kuchakaa kwani tangu mwaka 1957 haijawahi kufanyiwa ukarabati na kwamba mpaka sasa kumalizika kunahitajika kiasi cha shilingi milioni thelathini na sita, mpaka sasa wametumia  milioni kumi na moja.
Pia amesema wana mradi wa kujenga uzio na mageti ya kisasa, kuanzisha kiwanda cha kuzalisha maji, kuanzisha duka la vitabu, ukumbi wa mikutano pamoja na shamba la mahindi na mihogo.
Hata hivyo ametoa wito kwa wakristo kuwanyenyekea na kujishusha mbele ya viongozi wao hata kama wakichukizwa bali wanapaswa kuwa na busara ya kukaa pamoja kumaliza tofauti zao.
“Wapo wakristo hawataki kujishusha mbele ya mapadri, na viongozi wao wanakuwa na kiburi ambacho matokeo yake sio mazuri, hivyo nawasihi onyesheni upendo na mshikamano kwa viongozi wenu,” amesema padri Nixon.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU