Kanisa halitadhoofishwa-Ask Ndimbo

n Na Pascal Mwanache
ASKOFU wa Jimbo Katoliki Mbinga na Mwenyekiti wa Huduma za Jamii kwa upande wa Elimu, katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Mhashamu John Ndimbo amesema kuwa, licha ya vikwazo na changamoto wanazokutana nazo katika jitihada za kumkomboa mtanzania dhidi ya ujinga, Kanisa Katoliki halitarudi nyuma wala kudhoofishwa kwa kuwa utoaji wa elimu ni sehemu ya kazi ya uinjilishaji ya Kanisa.
Ameeleza hayo hivi karibuni wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Makatibu wa Elimu kutoka Majimbo Katoliki Tanzania, uliofanyika TEC Kurasini jijini Dar es salaam. Askofu Ndimbo amesema kuwa siku zote uwepo wa Kanisa Katoliki unatambulishwa kwa uwepo wa huduma za kijamii na kusema kuwa hakuna uinjilishaji pasipo makuzi ya kitaaluma.
“Elimu ndiyo inayomfanya mwanadamu kwanza ayajue mazingira yake, ajitambue yeye ni nani na kisha imfahamishe uhusiano wake na Mungu. Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara inapata maana zaidi kwa jinsi sekta ya elimu ilivyokua katika taasisi zetu. Taasisi zetu za elimu ni wakala mashuhuri wa uinjilishaji” amesema Askofu Ndimbo.
Pia amewakumbusha makatibu hao kusisitiza malezi ya vijana kutoka moyoni, kwa kuwarithisha tunu za maisha kimwili na kiroho. Amesema kuwa mabadiliko ya mfumo wa elimu hasa kwa wanafunzi wanaotoka sekondari kwenda Vyuo Vikuu ambao wanalazimika kuomba moja kwa moja katika vyuo husika, hayapaswi kudhoofisha Vyuo Vikuu vya Kanisa Katoliki bali iwe fursa kwao katika kuwalea watoto wafaulu vizuri na kuwahamasisha waendelee na masomo katika vyuo vya Kanisa.
Awali akiwakaribisha wajumbe wa mkutano huo, Naibu Katibu Mkuu wa TEC Padri Damian Dulle amesema kuwa Kanisa linapoadhimisha jubilee ya miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara, linajivunia mchango wake katika utoaji wa elimu, hasa kuongezeka kwa shule na ufaulu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU