WANANCHI WATAHADHARISHWA KUTOVAMIA MAENEO YA KANISA

n Na Veronica Modest, Musoma

WAnanchi wanaoishi jirani na maeneo yanayomilikiwa na Kanisa Katoliki kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali zikiwemo za kiroho, na kijamii wametakiwa kutoingilia mipaka ya maeneo hayo kwa kuwa maeneo hayo yalitolewa kwa mujibu wa kanuni, sheria na taratibu.
 Baadhi ya maeneo ya Kanisa yamekuwa yakiingia katika migogoro mikubwa na wananchi wanaoishi kuzunguka maeneo hayo, kutokana na watu kuvamia na kujenga pasipo kujua au wakijua kuwa eneo hilo tayari lilishanunuliwa na Kanisa kwa ajili ya kutoa huduma katika jamii na hatimiliki zikiwepo zinazoonyesha ukubwa wa eneo, lakini viongozi wa vijiji husika wamekuwa wakigeuka na kusema kuwa Kanisa ndio linalochukua maeneo ya wananchi.
 Hayo yamesemwa hivi karibuni na Askofu wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila wakati wa Misa Takatifu ya Kumshukuru Mungu kwa shirika la Marist Brother kutimiza miaka 200 tangu lilipoanzishwa mwaka 1817, miaka 25 ya uwepo wa shirika hilo hapa nchini Tanzania katika kijiji cha Masonga na miaka 25 ya shule ya Sekondari ya Masonga pamoja na parokia ya Masonga tangu zianzishwe, Misa iliyofanyika katika shule ya Masonga jimboni hapa.
 Askofu Msonganzila amesema kuwa  mashirika ya kitume yanapokuja nchini hayaji kunyang’anya wananchi maeneo yao, bali lengo lao linakuwa kuwahudumia wananchi ambao ndio kusudio lao kubwa, hivyo  kwa vile  Kanisa linakuwa na maeneo makubwa ambayo wanakuwa wameshayanunua mapema ndio maana wanawaruhusu kujenga kwa  ajili ya kutoa huduma kwa jamii na hasa katika maeneo yaliyoachwa nyuma kimaendeleo na ndio maana shirika la Marist Brother walipofika Masonga walianza kutoa huduma ya kiroho na elimu dunia kwa maana kuwa ndio walioanzisha shule ya Sekondari ya Masonga na eneo hilo lilikuwa nyuma kielimu.
 “Hivi karibuni nilikuwa huku kwa masuala ya migogoro ya ardhi, wananchi wanasema kijiji kililiuzia Kanisa eneo hili kinyemela wakati kwenye hati ya eneo hili inaonyesha mwanzo wa eneo hadi mwisho, na niwaambie kabisa huduma wanazozitoa hawa mabruda zitakuwa nzuri kama mahusiano yenu baina ya wananchi na viongozi wa vijiji vinavyozunguka shule hii yatakuwa mazuri.
“Ombi langu kwa viongozi wa vijiji na Wilaya hii ya Rorya naombeni sana tuache mizozo ya viwanja, ambayo inasababisha huduma zisiendelee au zicheleweshwe na sisi hapa Masonga tupo pembezoni kabisa, na Marist hawa wametoka mbali kuja kutusaidia kimaendeleo, naomba tuwape nafasi  jaza ujazwe, tuwajaze maeneo ili tufaidike zaidi, viongozi wa Serikali toeni  mwanya ili huduma za jamii zinazoletwa na hawa watu wa mbali ziweze kutuletea maendeleo,” amesema Askofu Msonganzila.
Reman Osca mwakilishi wa shirika hilo kutoka nchini Mexico amesema kuwa wao walikuja kusaidia jamii ya Masonga ambayo ipo pembezoni kabisa na ilikuwa imeachwa nyuma kimaendeleo hususani kielimu, na kwa sasa jamii iko vizuri kielimu na kiroho.
Kwa upande wake mkuu wa shule hiyo ya Masonga Br Valerian Stephen Kalendelo ambaye ndiye mwafrika wa kwanza tangu kuanzishwa kwa shirika hilo hapa nchini Tanzania, amesema kuwa shule hiyo kwa sasa ina wanafunzi 470 na mwaka huu wanaotarajia kufanya mtihani wa kidato cha nne wapo 67 na  kuna shule maalum ambayo ina watoto 21 viziwi, ambapo hadi sasa wanahitaji kujenga majengo mengine kwa ajili ya kupanua huduma wanazozitoa lakini wananchi wamezuia kwa madai kuwa eneo wanalotaka kujenga ni la wananchi, kwa madai kuwa Serikali ya kijiji ililiuzia Kanisa eneo hilo kinyume na taratibu.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU