DUMISHENI AMANI-RAIS MAGUFULI

n Na Dotto Kwilasa,Dodoma.
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Magufuli, amewataka watanzania wote kutunza amani ya nchi ambayo ndio tunu ya Taifa ikiwa ni pamoja na kuiunga mkono Serikali ya awamu ya tano katika utendaji wake.
Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni  Mjini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za mitaa, George Simbachawene kwa niaba ya Rais katika ibada ya kusheherekea  Jubilei ya Miaka 100 ya Upadri Tanzania Bara iliyofanyika katika eneo la Hija Kata ya Miyuji Manispaa ya Dodoma.
 Aidha Waziri Simbachawene amesema kuwa Serikali inaendelea kuuenzi mchango wa taasisi za kidini ambao umekuwa ukitolewa kwa jamii hususani katika masuala ya elimu, afya na maendeleo ya jamii kwa ujumla.
Hata hivyo amezitaka taasisi mbalimbali za kidini nchini kuwekeza katika viwanda ili kufikia uchumi wa kati wa viwanda kwa kutoa ajira kwa vijana.
Mbali na hayo amewataka watanzania kuwa waadilifu na waaminifu kwa Serikali yao kwa yale mema ya kimaendeleo ambayo yanafanywa.
Kwa upande wake Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Burundi Askofu Mkuu Joakim  Kambanda amewataka mapadri nchini kujali umuhimu wa nafasi yao katika jamii.
Amebainisha kuwa mapadri wa kwanza katika nchi za Burundi na Rwanda walilelewa Tanzania na hivyo kuwahamasisha kujali umuhimu wa ukuhani wakati wote.
“Tukio hili ni la kihistoria, hata sisi tumehamasika kuiga hasa kwa kuwa mapadri wa mwanzoni kabisa nchini mwetu wamelelewa Tanzania,” amesema Askofu Joakim wa Burundi.
 Sherehe hizo za Jubilei ya Miaka 100 ya Upadri Tanzania Bara zimehudhuriwa na waamini mbalimbali wakiwemo viongozi wa kisiasa na Serikali.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU