Wawakilishi wa Caritas wakutana Tz, watoa neno kwa maaskofu


Na Dalphina Rubyema
WAKATI  wafanyakazi wa  Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki (Caritas) wakitakiwa kujitathimini kuona kama utendaji wao unabeba utambulisho wa chombo hicho, Maaskofu nchini wameombwa  kulichukulia shirika hilo kama nyenzo yao ya  kuhudumia jamii kiroho na kimwili, hivyo kuhakikisha wanazifuatilia kwa karibu shughuli za utendaji wake.
Ombi  hilo limetolewa na Katibu Mtendaji Msaidizi wa Caritas Internationalis, Roma, Monsinyori Pierre Cibambo, wakati wa mkutano baina ya timu ya wawakilishi wa Caritas ilipomtembelea Mwenyekiti wa Idara ya Caritas- Tanzania,  Askofu Mkuu Yuda Thaddeus Ruwa’ichi, uliofanyika nyumbani kwake, Kurasini jijini Dar es Salaam mwanzoni mwa juma.
Monsinyori Pierre ambaye katika ziara hiyo aliongozana na Makatibu Watendaji  wa Caritas Afrika, AMECEA na watendaji  wa Caritas- Tanzania ngazi ya taifa, amesema kuwa  tangu kuanzishwa kwake, Caritas ni chombo cha maaskofu lengo lake likiwa ni kufanya matendo ya huruma kwa makundi mbalimbali ndani ya jamii hususan maskini,  hivyo ili kiweze kutimiza majuku yake ipasavyo, hakina budi kupata ushirikiano kutoka kwa viongozi hao wa kiroho.
“CARITAS- Tanzania ni kioo cha maaskofu wote wa TEC na Kanisa la Tanzania kwa ujumla, hivyo kufanya kwake vizuri ni taswira nzuri pia kwa baraza ambalo maaskofu wake walioshiriki kwa namna ya pekee kuanzishwa kwa shirika hili la hisani, “ amesema.
Sanjari na hilo, Monsinyori Pierre alisema, ukaribu wa Maaskofu kwa Caritas kutawafanya hata watendaji wa shirika hilo kufanya kazi zake katika uwajibikaji wa hali ya juu , wakitambua kuwa juu yao kipo chombo kinachowasimamia na kuwafuatilia kwa karibu.
“Hata kama utapata misaada lakini kama hauna chombo ama mtu wa kusimamia kwa karibu, bila shaka huwezi kufika mbali katika kutimiza lengo lililokusudiwa, kwani mtekelezaji wa shughuli utakuwa ni wewe mwenyewe, unajifanyia tathmini mwenyewe na hata ukaguzi wa mahesabu ni mwenyewe… ukifanya kazi namna hii bila shaka hauwezi kufika mbali,” alisema.
Hata hivyo Monsinyori Pierre alisema, katika utafiti wao sehemu mbalimbali duniani, wamebaini kuwa kuna baadhi ya nchi ambako  Caritas inafanya kazi kama baadhi ya NGO, ambapo watendaji wake wanajali  zaidi maslahi yao binafsi ikiwemo  mishahara mkubwa na stahiki nyingine, hivyo kupoteza utambulisho wa kuanzishwa kwake kama chombo cha kueneza upendo na kufanya matendo ya huruma kwa masikini.
 “Caritas haitakiwi kufanya  kazi yake  kwa ushindani kama zilivyo baadhi ya NGOs, bali utekelezaji wa majukumu yake lazima uendane na utume wa Kanisa wa kumuhudumia mtu kimwili na kiroho na hasa suala la ujenzi wa amani, kutoa misaada ya kiutu kwa watu wanaopata majanga na matatizo mbalimbali na huduma nyinginezo, hivyo kutekeleza tunu ya  viongozi wa Kanisa ya kuwa sauti ya wasiyokuwa na sauti,” alisisitiza.
Aliongeza “Ni kutokakana na  sintofahamu   iliyojitokeza ndani ya Caritas hasa ya kupoteza utambulisho wake, kulikopelekea hata Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani, kuliagiza shirika hili kujitathmini ili kuona kama utendaji wa shughuli zake unaendana na madhumuni ya uanzishwaji wake ama vinginevyo,” alisema.
Alitoa wito kwa wafanyakazi wote wa Caritasi kutambua utendaji wa shughuli zao upo chini ya askofu wa eneo husika iwe ngazi ya Taifa ama Jimbo, hivyo hawanabudi kufanya kazi zao kwa uwazi na kuwajibika vilivyo kwa viongozi wa maeneo husika.
“ Pia mapdri na watawa wa kike na kiume washirikishwe ili waweze kuitambua Caritas na shughuli zake…jambo hili pia ni vyema likaendana na kuwafundisha waamini katika ngazi zote kuanzia kwenye jumuiya Ndogondogo za Kikristo, juu ya kufanya matendo ya huruma, hivyo kuwahamasisha kutoa kwa ajili ya wahitaji wakiwemo masikini na watu wenye kupata majanga mbalimbali,” alisisitiza.
Katika hili aliongeza kuwa hata Ulaya wanaotoa misaada siyo matajiri bali ni watu wenye kipato cha kawaida ambao wanaupendo na hofu ya Kimungu ya kuwasaidia wengine, hivyo akatoa wito pia kwa ofisi ya Caritas Taifa kuendelea kutekeleza majukumu yake hasa ya kuratibu kazi za majimbo pamoja na kusimamia miradi inayofadhiliwa na Caritas Internatiolis, badala ya kutekeleza moja kwa moja miradi hiyo.
Hata hivyo hakusita kutoa pongezi zake kwa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania(TEC), Padri Charles Kitima, ambapo alisema baada ya kuzungumza naye, alionyesha kulifahamu vilivyo lengo la Caritas na zaidi, Katibu Mkuu huyo aliahidi kuwa TEC katika mipango yake, itaweka vipaumbele vya kulifanya Shirika hili kutekeleza kazi zake kama ilivyokusudiwa.
Upande wake Mwenyekiti wa Caritas-Tanzania, Askofu Mkuu  Yuda Thaddeus Ruwa’ichi alisema Kanisa la Tanzania linaheshimu kazi nzuri inayofanywa na shirika hilo na kwamba kama kuna mapungufu, basi sula hilo litajadiliwa kwenye vikao mbalimbali vya maaskofu ili yaweze kufanyiwa kazi, hivyo kuendeleza ustawi mzuri kwa manufaa ya jamii, Kanisa na Taifa kwa ujumla.
“Kama maaskofu tupo bega kwa bega na Caritas, tunaitambua na kuthamini kama chombo chetu cha kuihudumia jamii… ni kweli changamoto zipo, lakini hili ni jambo linaloendelea kufanyiwa kazi na masuala mengine yatajadiliwa kwenye mikutano mbalimbali  ya maaskofu,” alisema.
Katibu Mtendaji Caritas- Afrika, Bw. Albert Mashika, ametoa wito kwa shirika hilo upande wa Tanzania kuwa na mpango mkakati  wenye kulenga kutekeleza shughuli mbalimbali za kijamii, ambapo hata hivyo mkakati huo  usitofautiane sana na ule wa CARITAS Afrika uliopangwa kutekelezwa ndani ya kipindi cha miaka mitano , kuanzia 2019-2023. “Kwenye mkakati wenu pia lazima muwe na vipaumbele na kuvifanyia kazi kwa wakati,” alisema.
Katibu Mtendaji wa  Caritas- AMECEA, Padri Paul Igweta, kwa upande wake alisema, kama chombo cha Kanisa, shughuli za Caritas zinategemeana, hivyo kufanya vizuri kwa Caritas Tanzania si tu ni mafanikio ya TEC, bali pia ni mafanikio ya AMECEA, Caritas Afrika na hata Caritas Internationalis, hivyo akaomba ushirikiano  ili lengo hili litimie.
Timu hii ya Caritas Internationalis, Afrika na AMECEA ilifanikiwa kukutana na watendaji wa Caritas Tanzania, ambapo  ambapo pamoja na mambo mengine walifanikiwa kubadilishana uzoefu wa kiutendaji, kujua maendeleo ya Catitas Tanzania na changamoto zake pamoja na kuweka mkakati  wa kuzitatua.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU