JPM: Kipaumbele ni kuhuisha teknolojia ya viwanda SADC

Na Paschal Dotto-MAELEZO
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.John Pombe Magufuli amefungua maonesho ya wiki ya viwanda kwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Africa (SADC).
Akizungumza katika hafla hiyo ya Wiki ya Viwanda ya SADC, Jijini Dar es Salaam, Rais Magufuli amesema kuwa ili kufikia uchumi wa kati viwanda ni kichochea muhimu katika sekta nyingi kwani uwepo wa viwanda utasababisha uhakika wa uzalishaji na uchakataji wa bidhaa na kufanya biashara kwa nchi wananchama.
Rais Magufuli amezitaka nchi wanachama wa SADC kuweka kipaumbele kwenye kuhuisha teknolojia katika viwanda vilivyoko ndani ya jumuiya ya Maendelea kusini mwa afrika (SADC) pamoja na kushughulikia kwa haraka zaidi vikwazo vinavyochelewesha ukuaji wa viwanda.
“Viwanda ni Sekta muhimu katika kukuza uchumi wa nchi yeyote, kuondoa umasikini, kuongeza ajira na Sekta hii imeziletea maendeleo makubwa nchi zilizoendelea, kwa hiyo mkutano huu ni dhahiri kuwa sasa nchi za SADC zimeanza kuchukua hatua madhubuti za kukuza sekta hii na ikiwa mkakati huu utatekelezwa utasaidia kukuza uchumi wa nchi zetu”, Rais Magufuli.
Akielezea suala la teknolojia Rais Magufuli amesema kuwa ukuzaji wa teknolojia na ubunifu kwenye sekta ya viwanda ni silaha muhimu kwa nchi za SADC kuendelea na kutegemeana kwani utazalisha ajira, biashara kubwa, na kuepuka kuuza malighafi  kwa wingi nje ya Afrika kama ilivyosasa.
Aidha Rais Magufuli amezitaka nchi wanachama wa SADC kujikita zaidi katika kukuza ubunifu na teknolojia rahisi kwenye sekta ya viwanda kwa kuwaendeleza vijana na kuimarisha viwanda vidogo vidogo vilivyoko kwenye jumuiya, kwa hiyo wiki ya viwanda ni fursa muhimu kwa nchi  zote wananchama.
“Wiki ya Viwanda ya SADC ni fursa ya kubadilishana uzoefu miongoni mwa wadau kuhusu utekelezaji wa mikakati ya miaka 49 ya uendelezaji wa viwanda katika jumuiya yetu, bado tuna safari ndefu kuhakikisha sekta ya viwanda inazidi kukua na kuleta mageuzi ya kiuchumi katika nchi zetu”, amesema Rais Magufuli.
Kwa upande wake Waziri wa Viwanda na Biashara wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Innocent Bashungwa amesema kuwa uthubutu wa Rais Magufuli kuipeleka Tanzania katika uchumi wa kati wenye viwanda ni mkubwa na  matokea yake  yanaonekana sasa. Hivyo, maonesho haya ni moja ya njia muhimu ya kuimarisha sekta ya viwanda nchini.
“Maonesho haya ya wiki ya viwanda yanawawezesha wanachama wa SADC kuona namna nchi wenyeji inavyotekeleza uwekezaji kwenye sekta ya Viwanda. Aidha,  tunaamini wazalishaji, wafanyabiashara, na wananchi kwa ujumla watachangamkia fursa mbalimbali zitazotokana na mkutano huu wa SADC.”, Waziri Bashungwa.
Waziri Bashungwa amesema kuwa Tanzania inafanya vizuri kwenye biashara ndani ya SADC  kwani takwimu zinaonyesha kuwa mauzo ya Tanzania kwenda SADC mwaka 2018 yalikuwa dola za kimarekani milioni 999 ikilinganishwa na dola za kimarekani milioni 875 mwaka 2017 ikiwa na ongezeko la asilimia 12.16.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt.Stagomena Tax, amesema kuwa juhudi za Serikali ya Tanzania kutekeleza mradi mkubwa wa kufua na kuzalisha umeme mto Rufiji ni moja ya njia madhubuti katika kuimarisha na kukuza sekta ya viwanda kwa Jumuiya ya SADC.
“Kutekelezwa kwa Mradi wa umeme mto rufiji tunaamini kuwa Tanzania itazalisha umeme wa kutosha, tunaomba ziada iweze kwenda kwenye nchi wanachama wa SADC kwani kumekuwa na changamoto ya kubwa mgawo wa umeme na uendeshwaji wa viwanda unahitaji mambo mengi ikiwemo umeme huwezi kuwa na viwanda bila kuwa na umeme unaozalishwa kwa urahisi, kwa hiyo Tanzania imechukuia maamuzi mazuri kuzalisha umeme mto Rufiji.”, Stagomena Tax, Katibu Mtendaji, SADC.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU