Kardinali Pengo afanya ziara ya kichungaji Shinyanga

Na Natoly Salawa ±Shinyanga

ASkofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amewataka mapadri kuambatana daima na Kristo katika utume wao badala ya kujiambatanisha na malimwengu.
Kadinali Pengo ameyabainisha hayo katika Kanisa Kuu Mama Mwenyehuruma Ngokolo Shinyanga wakati wa mahubiri yake katika adhimisho la Ekaristi Takatifu na utowaji wa Daraja Takatifu la Upadri kwa mashemasi sita katika sherehe ya Kupalizwa Mbinguni Bikira Maria iliyofanyika 15 Agosti, 2019.
Katika ujumbe wake,Kadinali Pengo amewataka mapadri hao wapya kwenda kufanya utume wao kwa uaminifu huku wakitambua kuwa upadri ni  kujitoa sadaka kwa Mungu, hivyo wasifanye  utume wao kinyume na matarajio ya Wakristo ambao wanamategemeo makubwa juu yao na badala yake wamtangulize Kristo  katika huduma yao kwa Kristo na Kanisa lake.
Aidha Kadinali Pengo ametoa wito kwa  waamini wa jimbo Katoliki Shinyanga kuendelea kuwaombea mapadri wapya na mapadri wote kwa kuwa utume wa mapadri hauwezi kufanikiwa bila sala za waamini.
Mashemasi waliopewa Daraja Takatifu la Upadri ni Richard Masunga wa Parokia ya Malili, Gregory Samike wa parokia ya Salawe, Peter Mkunya wa parokia ya Malampaka na Peter Tungu wa parokia ya Mwanhuzi. Wengine ni Martine Masanja na Martine Jilala wote wa parokia ya Mipa.
Akitoa neno la Shukrani kwa niaba ya wanajimbo la Shinyanga kwa Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu wa Jimbo Katoliki Shinyanga Mhashamu Liberatus Sangu amesema kuwa ziara ya siku nne ya Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam Mwadhama Polcarp Kadinali Pengo imekuwa kichocheo kikubwa cha miito ya upadri jimboni hapa baada ya kuwapa Daraja Takatifu la Upadri mashemasi sita wa jimbo kwa mpingo,  tukio ambalo lilitokea  miaka 25 iliyopita katika historia ya jimbo “tangu mwaka 1994 jimbo halijawahi kupata mapadri sita kwa mkupuo na leo wewe Mwadhama umewapa Daraja hilo Takatifu la Upadri kupitia mikono yako mashemasi sita wa jimbo” .
 Askofu Sangu pia amemwelezea Kardinali Pengo kuwa amekuwa chachu ya kujenga umoja, upendo na mshikamano katika taifa la Tanzania na  nje ya Tanzania kutokana na kazi mbalimbali alizozifanya za kuwaunganisha watu wakati wote wa utume wake katika Kanisa.
Askofu Sangu pia alitumia nafasi hiyo  kutoa shukrani zake kwa jinsi serikali ya mkoa wa Shinyanga inavyoshirikiana na viongozi wa dini na ameahidi kuendeleza ushirikiano huo ili kuhakikisha hali ya umoja, upendo na mshikamano vinatawala katika jamii  hatua ambayo itasawaidia watu kujiletea maendeleo.
Kwa upande Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Bi Zainab Telack amelezea namna ambavyo viongozi wa dini likiwemo Kanisa Katoliki wanavyotoa mchango katika kudumisha amani miongoni mwa jamii.
Ametolea mfano jinsi ambavyo wamesaidia kukomesha mauaji ya vikongwe katika mkoa wa Shinyanga  pamoja na kujenga misingi ya utulivu ambayo imewasaidia viongozi wa serikali kuwaongoza watu bila migongano na kwa unafuu mkubwa.
Mwadhama Polcarp Kadinali Pengo aliwasili jimboni Shinyanga kupitia uwanja wa ndege wa Kahama siku ya Jumatano Agost 14 mwaka huu na kupokelewa na Askofu wa Jimbo la Shinyanga Mhashamu Liberatus aliyekuwa ameambatana na Askofu wa Jimbo Katoliki Kahama Mhashamu Ludovick Joseph Minde, mapadri, watawa, waamini pamoja na viongozi wa serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Zainab Telack.
Akiwa Kahama Kadinali Pengo  amebariki mawe ya msingi ambayo yatatumika katika miradi mbalimbali ya Jimbo Katoliki Kahama na kutoa Baraka kwa waamini wa jimbo hilo na baadaye alifanya mazungumzo mafupi na askofu Minde.
Aidha akiwa jimboni Shinyanga Kadinali Pengo ametumia siku ya pili ya mapumziko yake kubariki jengo la nyumba ya mapadri linaloendelea kujengwa katika parokia teule ya Lubaga mjini Shinyanga na kupanda mti wa kumbukumbu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU