Waliovamia kiwanja cha Kanisa waitwa kwa Lukuvi

Na Mashauri Marwa
WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi ameagiza mmiliki wa Kituo cha mafuta cha Victoria Service Station kilichopo maeneo ya Msimbazi Center, Dar es salaam kuwasilisha kwake nyaraka zote kuthibitisha uhalali wa umiliki wake katika eneo hilo.
Waziri Lukuvi ametoa agizo hilo katikati ya juma alipofanya ziara katika kituo hicho cha mafuta kinachodaiwa kuendesha katika eneo halali la Kanisa katoliki Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, kupitia Parokia ya Msimbazi.
Akiwa katika eneo hilo pamoja na paroko wa parokia ya Msimbazi, Padri  Gregory Josephat, Mwenyekiti wa Kamati ya Ardhi ya Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Albert Singombe, amemwambia waziri kuwa, eneo kilipo kituo hicho cha biashara ya mafuta, ni mali ya Kanisa tangu mwaka 1965 na nyaraka halali za umiliki zipo.
Baada ya Padri Greogory na Bw Singomnbe kumwonesha nyaraka za umiliki wa eneo hilo na kusikiliza maelezo ya mwendeshaji wa kituo hicho, waziri Lukuvi amesema nyaraka hizo za Kanisa ikiwamo hati na zile zilizopo ofisini kwake zinabainisha kuwa, wamiliki wa kiwanja hicho ni Kanisa Katoliki kwa kuwa tangu mwaka 1965 Kanisa lilipopata hati hiyo, haikuwahi kufutwa.
Amesema ingawa anazitaka pande zote husika katika mgogoro huo wa ardhi kufika ijumaa hii ofisini kwake jijini Dar es Salaam na vielelezo husika, kwa kawaida na kisheria kama hati ya umiliki wa Kanisa Katoliki haikufutwa, basi kama kuna nyingine iliyotolewa katika kiwanja hicho hicho, hiyo nyingine ni batili.
“Kisheria ili kuhamisha umiliki, lazima ile ya kwanza ifutwe. Sasa kama haikufutwa, hii nyingine ni batili maana hakuna hati inayotolewa juu ya hati nyingine, wala mchoro wa kiwanja unaochorwa juu ya mchoro mwingine,” amesema Waziri Lukuvi.
Katika maelezo yake kwa waziri, mmiliki huyo wa Victoria services station, amesema eneo hilo aliuziwa na Hawel (Abdalla Thabit Hawel) mwenye asili ya Kiarabu, aliyempa nyaraka akimhakikishia kuwa kiwanja hicho ni mali yake.
Baada ya kusikia maelezo hayo waziri Lukuvi akasema: “Njoo Ijumaa pale ofisini kwangu na nyaraka zako zote; na hata Kanisa njooni na nyaraka zote na mtu yeyote anayejua vizuri aneo hili.”
Akaongeza; “Kwa mara ya kwanza leo ndipo nimesikia kuwa mwarabu anamuuzia mswahili eneo, badala ya mswahili kumuuzia mwarabu… halafu waarabu kwa biashara hii ya mafuta tena katika eneo hili la barabarani mpaka akuuzie, lazima  alijua kuna bomu hapo na nadhani ndugu yangu hapa kuna mchezo mchafu umefanyika umeingizwa mkenge.”
Aidha amesema nyaraka zilizowasilishwa na Kanisa sambamba na maelezo ya wawili, zinaonesha kuwa eno hilo ni mali ya Kanisa kwa kuwa hati ya Kanisa ni hai na haijafutwa.
“Askofu Nzigilwa (Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam) alikuja pale ofisini akanionesha hati zote na tumezichunguza na kuangalia nakala zetu , tumejiridhisha kuwa, bado eneo hili ni mali halali ya Kanisa maana hati bado ni hai,” ameeleza Lukuvi.
Awali katika ziara hiyo, waziri Lukuvi alimrudishia bw. Ramadhani Sood Bulenga jengo lake la ghorofa nne lililopo maeneo ya mzunguko wa kigogo wilayani Ilala baada ya jengo na eneo hilo kumilikishwa kinyume na taratibu kwa mtu aliyefahamika kwa jina la Hans Macha.
Lukuvi amesema kutokana na hali hiyo, amemwondoa kazini kamishina aliyehusika na ukiukaji huo wa taratibu na kumteua David Mshendwa kushika wadhifa huo.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU