Kardinali Pengo atimiza miaka 75, atoa neno kuhusu kustaafu


Nictor Shonga na Geofrey Wella
WAAMINI nchini wametakiwa kutambua kuwa kutimiza umri wa miaka 75 ya kuzaliwa siyo kigezo pekee cha kustaafu nafasi ya uaskofu kwa maaskofu wa Kanisa Katoliki, bali mwenye ruhusa ya kutoa kibali cha kufanya hivyo ni Baba Mtakatifu pekee.
Angalizo hilo limetolewa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, wakati  wa Misa Takatifu ya Kutabaruku Kanisa na Altare, katika Parokia ya Mtakatifu Augustino Salasala jimboni humo.
Kardinali Pengo ambaye alitoa kauli hiyo siku moja kabla ya kutimiza umri wa miaka 75 ya kuzaliwa, alisema askofu yeyote hawezi kujiamria kustaafu kwa kigezo kwamba ametimiza wa umri, bali atafanya hivyo kwa kuruhusa ya Baba Mtakatifu ambaye ndiye kiongozi Mkuu wa Kanisa Katoliki Duniani.
“Lakini askofu anaweza kuomba kwa Baba Mtakatifu ampumzishe kusimamia kazi za jimbo anapotimiza umri wa miaka 75 na kama yeye (Papa) hajakwambia ustaafu basi utaendelea na majukumu yako kama kawaida,” alisisitiza.
Aliongeza “ Mimi binafsi nimetumikia nafasi ya uaskofu kwa kipindi cha miaka 35… ni kipindi kirefu na tayari nimeishamjulisha Baba Mtakatifu kuwa kesho (Agosti  5, 2019) natimiza miaka 75 ya kuzaliwa… hivyo niendelee  ama nisiendelee kulitumikia Kanisa katika nafasi yangu, hilo ni jukumu la Baba Mtakatifu mwenyewe.”
Sanjari na hilo, Kardinali Pengo aliwapongeza waamini wa Parokia hiyo ya Mtakatifu Augustino, Salasala, kwa moyo wa majitoleo ambapo wamefanikisha ujenzi wa Kanisa kwa nguvu zao wenyewe, jambo linalotakiwa kuigwa na waamini wa Parokia nyingine.
“Kujitolea kwa michango mbalimbali ikiwemo ya kifedha hadi kukamilisha ujenzi wa Kanisa hili ambalo ni kubwa  na zuri na ujenzi wake kuchukua muda mfupi, ni ishara ya nje ambayo inapaswa kudhihirisha roho iliyo ndani mwenu  ambayo imejaa upendo na  mshikamano,” alisema.
Aliongeza “Tungeweza kukaa hata chini ya mkorosho na kuabudu…lakini kwa vile mwanadamu ni mwili na roho, ndiyo maana tumeweza kufanya ujenzi kama huu… hii ni udhihirisho wa upendo mlionao kwa Mungu na si kwetu tu kama Wakristo Wakatoliki, lakini hata kwa wasiyo Wakatoliki,” alisema.
Hata hivyo alisema, kukamilika kwa kazi hiyo ya ujenzi wa Kanisa si mwisho wamejitoleo kwa waamini hao wa Salasala, bali ni mwanzo wa kuendelea kujitolea zaidi ili kazi ya Mungu iendelee kusonga mbele.
Akielezea maana halisi ya kutabaruku Kanisa na Altare, Kardinali Pengo alisema “ hii ni kwamba mahali hapa hata kama tunatamani pawe ukumbi wa kufanyia mkutano au biashara nyingine… kwa sasa baada ya kutabarukiwa, mahali hapa patatumika kwa ajili ya shughuli za Kiibada tu kuanzia leo na hata milele,si shughuli nyininezo,”.
Naye Paroko wa Parokia hiyo, Padri Peter Assenga, CSSp, aliwashukuru wanaparokia na timu ya wataalam, waliojitolewa kwa namna ya pekee kuhakikisha ujenzi huu unakamilika kwa ufanisi tena ndani ya muda mfupi, hivyo akwaomba waendelee na moyo huu wa majitoleo.
Ujenzi wa jengo hilo la Kanisa la Mtakatifu Augustino Salasla ulianza rasmi Novemba 2015 chini ya Padri Greogory Mallya, CSSp ,(aliyekuwa Paroko kwa kipindi hicho) na kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi, Bibi Frola Minja, sehemu kubwa ya ujenzi huu imechangiwa na waamini wenyewe.
Parokia ya Mtakatifu Aigustino Salasala ilitangazwa rasmi na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam,  Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, mnamo Agosti 15 mwaka 2004 na kabla ya hapo ilikuwa na moja ya vigango vya Parokia ya Mtakatifu Nicholaus Mtongani.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU