Paroko: Wakeketeni watoto kiimani siyo kimwili

Na Veronica Modest, Sirari


PAROKO wa Parokia ya Sirari katika Jimbo Katoliki la Musoma, Padri Erenest Kamugisha amesema umefika wakati sasa jamii ikawakeketa watoto na vijana kiimani ili wawe waamini na raia wema, badala ya kuwakeketa kimwili hali inayowapa mateso.
Kwa msingi huo amesema, mabadailiko ya waamini kuachana na sherehe zinazohusu ukeketaji na kuhamia katika sherehe za kikanisa kama Ubatizo, yatasaidia kuondoa uhalifu na ukatili kama mauaji katikajamii na kuwaongezea uhusiano na Mungu.
Aidha, amewasisitiza Wakristo kuacha vitu na mambo ya anasa kwa kuwa yanawafanya watu kumchukiza Mungu kwa mambo mbalimbali ya hatari kimwili na kiroho kama mauaji, utoaji mimba, utekaji watoto, wizi, ushoga na usagaji.
Ukeketaji wa kimwili ni ukatili ambao wamekuwa wakifanyiwa baadhi ya wanawake na watoto wa kike katika jamii kadhaa nchini huku ukitajwa kama hatari kwa afya na kisaikolojia kwa wahusika.
Padri Kamugisha alisema hayo hivi karibuni wakati akitoa Sakramenti za Ubatizo na Komunio ya Kwanza kwa waamini zaidi ya 70, katika Misa Takatifu iliyofanyika katika Senta za Sirari na Pemba za Kigango cha Nyabitocho parokiani Sirari.
“Tumefikia hatua hatuwezi kumaliza wiki bila kusikia tukio mojawapo kati ya hayo, hivyo inatubidi tusali kumuomba Mungu aweze kuingilia kati maana zamani watu ndio walikuwa wanaogopa fisi na samba, lakini sasa mwanadamu amegeuka kuwa chui na simba na anaogopwa sana; ni heri  kupita ndani ya hifadhi ukakutana na wanyama wakali kuliko mwanadamu  maana amekuwa mwovu zaidi,” alisema.
Hata hivyo, paroko huyo aliwapongeza waamini wa eneo hilo kwa kuanza kubadili mtazamo mintarafu suala la kuwafanyia sherehe watoto wao wanapopokea sakramenti mbalimbali ndani ya Kanisa kama Ubatizo, Komuniyo na Kipaimara badala ya kuwafanyia sherehe wakati wa ukeketaji ambao ni ukatili wa kijinsia.
“Niniwapongeza kwa moyo wa dhati kabisa kutokana na mabadiliko ninayoyaona maana zile sherehe mlizokuwa mnazifanya wakati wa ‘salo’ (ukeketaji) sasa zihamishieni kanisani wakeketeni watoto kiimani kama mlivyofanya sasa,” amesema Padri Kamugisha.
Mmoja wa waamini waliopokea sakramenti katika tukio hilo, Anastazia Joseph alisema anamshukuru Mungu kwa kumfikisha katika hatua hiyo aliyoitamani kwa muda mrefu.
Alimshukuru pia Padri Kamugisha kwa kukubali kuwapatia sakramenti katika misa iliyofanyika katika kigangoni Nyabitocho katika Parokia ya Sirari.
Nao wasimamizi wa watoto hao na viaana waliopata sakramenti wameahidi kuwalea watoto katika misingi inayompendeza Mungu ikiwa ni pamoja na kuwatembelea mara kwa mara na kushirikiana nao katika shughuli mbalimbali za kiimani.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU