Waliosoma Chanjale seminari wamuunga mkono Askofu Kimaryo kuendeleza jimbo



Na Philipo Josephat Same Kilimanjaro
Wanamalezi wote waliosoma katika seminari ya Chanjale tokea ilipoanzishwa wameungana na Askofu wa Jimbo Katoliki Same Mkoani Kilimanjaro Mhasham Rogathy Kimario kuendeleza utume katika jimbo hilo.
Awali walianza kujumuika katika hija ya kusali njia ya msalaba siku ya Ijumaa Kuu kwa kupandisha mlima kuanzia Njoro hadi Chuo cha Malezi Dido ambapo wanafunzi wanapata elimu ya awali ya sekondari (pre-form one) kabla ya kuingia kidato cha Kwanza huko Chanjale Seminari wilaya ya Mwanga Kilimanjaro.
 Kwenye hija wanamalezi hao waliosoma katika Seminari hiyo miaka ya 1983 hadi 2015 wameahidi kumuunga mkono Askofu Kimaryo  katika kulipeleka mbele jimbo Katoliki Same.
Wanamalezi hao wakiongozwa na Ndg Karol Kadeghe na Goodluck Kavugha  walimkabidhi Askofu Kimaryo Television moja kama zawadi kwa watoto wanaosoma katika Chuo cha Malezi Dido, vazi la Askofu la kuendeshea ibada na kumuonesha ujenzi wa vyoo na mabafu  ya kisasa ambao wanaujenga kwaajili ya wanafunzi hao na yatakabidhiwa mara tu baada ya kukamilika hivi karibuni.
Akipokea zawadi hizo Askofu Rogathy kwa kuonesha uso wa  furaha mbele ya waamini amesema kuwa, hakosi kutoa machozi ya furaha kila anapoona mambo mazuri yanafanyika. Amewashukuru kwa kujitolea kuendeleza seminari hiyo na kuwa wazalendo wa Seminari ya Chanjale iliyowafanya wawe kama walivyo leo.
“Hii ni imani na moyo wa ukarimu kwa wadogo zenu. Ninawashukuru sana,” amesema Askofu Kimaryo.
Pia amewaomba wanamalezi hao kumsaidia kujenga ukumbi wa Seminari ya Chanjale kwa ajili ya mahitaji mbalimbali ombi ambalo lililopokelewa kwa mikono miwili na wanamalezi hao.
                   Aidha, wanamalezi hao wamewekeana mikakati mbalimbali ambayo wataifanya ili kutimiza majukumu la kulipeleka Jimbo la Same Mbele kwa kushirikiana na Askofu wa jimbo hilo, mapadri, watawa na waamini.
Mratibu Mkuu wa Kikundi hicho Gudluck Kavunga amewaasa wote waliosoma katika Seminari ya Chanjale kuunga mkono jitihada za kundi hilo ili kuendeleza elimu jimboni Same na kuwasaidia wanafunzi wanaosoma Dido na Chanjale seminari kutimiza ndoto zao kama wao walivyofanikiwa.
“Kutoa ni kupokea, kutoa ni moyo si utajiri. Yule mwenye ujuzi wowote, kipaji, fedha, mali yoyote itakayofaa kuiendeleza Chanjale na Dido anakaribishwa kushirikiana na kikundi hiki cha Chanjale Alumni kwa ajili ya maendeleo ya jimbo letu.
Zamani tulikuwa na wafadhili kutoka ndani na n je ya nchi lakini sasa hatuna wafadhili wa nje. Wafadhili wa maendeleo ya Same ni sisi wenyewe. Tuwe wamisionari kweli kwa vitendo kwa ajili ya uinjilishaji wa nyakati zetu hasa wakati huu Kanisa Katoliki nchini linaposherehekea Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji. Tutimize wajibu wetu kama wakristo wa Kanisa Katoliki,” amesisitiza.
Kwasasa kikundi hicho cha wanamalezi kina watu 200 ambapo awali walikuwa wakiwasiliana na kupanga mambo yao kupitia mitandao ya kijamii na mikutano mbalimbali.Wamewataka wanamalezi wazawa na wasio wazawa ambao hawajajiunga nao wajiunge ili washirikiane kwenye shughuli mbalimbali kwaajili ya maendeleo ya jimbo la Same na kwaajili ya maendeleo ya Kanisa la Mungu  kwa ujumla (uinjilishaji wa kina).


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU