Padri Mtui afariki kwa ajali Shinyanga

Na Joachim Mahona, Shinyanga
Waselesiani wa Mtakatifu Yohane Bosco na Jimbo Katoliki Shinyanga wamepata simanzi baada ya Padri Richard Stanslaus Mtui  kufariki dunia baada ya gari alilokuwa akisafiria kugongana uso kwa uso na Lori la mizigo huko mkoani  Singida.
Padri Mtui    alikuwa ni Gombera wa shule ya Sekondari ya Don Bosco Didia, inayomilikiwa na Waselesiani wa Mtakatifu Yohane Bosco  iliyopo Didia katika Wilaya ya Shinyanga.
Kwa mujibu wa taarifa za kipolisi na zile zilizotolewa na msaidizi wake Padri Mathias Isaka ambaye ni Mkuu wa seminari hiyo ndogo, Padri Mtui amefariki dunia majira ya saa saba usiku, kuamkia Ijumaa kuu  baada ya gari alilokuwa akisafiria aina ya  Toyota  Noah  lenye namba za usajili Z463 GH kugongana uso kwa uso na lori la mizingo  lenye namba T9992 DLN aina ya Scania mali ya kampuni ya BHANJI  lililokuwa likitokea Dar-es-salaam kuelekea Burundi katika eneo la Kyengege wilaya ya Iramba mkoani Singida barabara kuu ya Mwanza  Dar es salaam.
Taarifa zaidi zinaeleza kuwa dereva wa Noah aliyokuwa amepanda marehemu padre Mtui  kutoka Singida  alikuwa akiendesha kwa mwendo kasi, kiasi kwamba alipoteza uelekeo  baada ya kukuta gari aina ya fuso likiwa limeegeshwa kandokando ya barabara.  Wakati akijaribu kuikwepa alikutana na lori hilo ambalo aligongana nalo uso kwa uso na kusababisha kifo cha Padre Mtui papo hapo  na mtu mwingine aliyekuwa amepanda kwenye Noah  hiyo alijeruhiwa vibaya  ambapo amevunjika mikono na miguu yote. Dereva wa Noah alifanikiwa kukimbia baada ya ajali hiyo kutokea.
Padre Mathis amebainisha kuwa marehemu Padri Mtui aliwaaga siku ya Jumatatu yaani Machi 26, 2018 kuwa anakwenda Moshi Mkoani Kilimanjaro kwa ajili ya kuadhimisha misa ya maziko ya mama yake mkubwa ambayo ilikuwa ifanyika Jumanne yaani Machi 27, 2018.
Baada ya maziko, siku ya Alhamisi Machi  29, 2018  alikwenda mpaka Arusha akitokea Moshi. Akiwa Arusha siku hiyo aliondoka majira ya saa kumi  jioni  kwa gari binafsi ambalo lilimfikisha mpaka Singida ambapo alipanda gari hilo la Noah kuja Shinyanga  kwa lengo la kuwahi kuja kuadhimisha Ibada ya Ijumaa Kuu.  
Akizungumza huku akibubujikwa na machozi Padri Mathias amefafanaua kuwa  alipata taarifa kuwa Padre Mtui amefariki kwa ajali ya gari kutoka kwa Padri wa shirika lao aliyeko Iringa siku ya Ijumaa Kuu mchana wakati akijiaandaa kwenda Tinde kwa ajili ya adhimisho la Ibada ya Ijumaa Kuu.
Padri huyo alimweleza kuwa alipigiwa simu na askari aliyeangalia namba katika simu ya marehemu baada ya ajali kutokea. Aliendelea kusema kuwa, baada ya kupata taarifa hizo yeye pamoja na watu wengine kadhaa walifunga safari ya kwenda Singida. Walipofika walikwenda  moja kwa moja katika kituo cha polisi na baadaye Maaskari walimpeleka  katika hospitali ya Kiomboi ili kuutambua mwili wa marehemu  na kuthibitisha kuwa ndie yeye.
Misa ya kuuaga mwili wa marehemu Padre Mtui imefanyika Aprili 3, 2018 na ikiongozwa na Mhashamu Askofu Liberatus Sangu wa Jimbo Katoliki  Shinyanga.
Ibada hiyo ilifanyika katika Viunga vya shule ya Sekondari Don Bosco - Didia na kuhudhuriwa na Mapadri, Watawa, Viongozi wa Serikali, Viongozi wa vyama vya siasa, Wafanyakazi wa shule hiyo, Waamini, Wanafunzi  na watu wote wenye mapenzi mema.
Katika misa hiyo, Askofu Sangu amewataka watu wote waendelee kumwombea Padri Mtui ili aweze kuyafikia aliyokuwa akiyaadhimisha na kuyatumainia.
Askofu Sangu amesema kuwa, Kanisa limempoteza padri kijana ambaye alikuwa mahili wa kazi. Aliwasisitiza Wakristo daima kujiweka tayari wakati wote na  kutotetereka kiimani pale misiba au matatizo yoyote yanapotokea,  kwa kuwa kifo ni njia na mlango wa kwenda kule ambako Kristo ametuahidia sote.
Kwa upande wake Mkuu wa Shirika hilo katika Ukanda wa Afrika Mashariki Padri Simon Asira amewashukuru watu wote kwa namna walivyoshiriki tangu kutokea kwa kifo hicho.
Amewaomba kuendelea kumtumainia Mungu ambaye amependa kumwita kwake Padri Mtui  na kwamba  pamoja na kifo chake  Shirika hilo litaendelea kuwepo na kutoa huduma za kielimu na nyinginezo kama kawaida katika jamii.
Mwili wa marehemu Padre Richard Mtui ulisafirishwa kwenda  Moshi mkoani Kilimanjaro  April 4,  2018 kwa ajili ya maziko ambayo  yamefanyika Aprili 5, 2018 katika eneo la nyumba ya malezi ya Shirika iliyoko huko Moshi.
Marehemu Padri Richard Mtui amezaliwa Juni 19 mwaka 1977 katika kijiji cha Mbahe bondeni wilayani Marangu mkoani Kilimanjaro.
 Baada ya kumaliza malezi  katika nyumba za malezi za Shirika la Mtakatifu Yohane Bosco katika Novitiate huko Nairobi Kenya na Ethiopia. Baada ya masomo yake  ya Falsafa na Theolojia  alifunga nadhiri za daima  mnamo Agosti 16 mwaka 2009.
Alipewa Daraja Takatifu la Ushemasi Mei 8 mwaka 2010 na baadaye Julai 21 Mwaka 2011 alipewa Daraja Takatifu la Upadri.
Baada ya kupewa Daraja la Upadri alipangiwa kwenda kufanya kazi katika shule ya Sekondari Don Bosco iliyoko Embu nchini Kenya na baadaye Julai mwaka 2016 aliteuliwa kuwa Mkuu wa nyumba Jumuiya ya Shirika Didia na Gambera wa shule ya Sekondari Don Bosco - Didia jimboni Shinyanga mpaka mauti yalipomkuta.

Roho ya Marehemu Padri Richard Mtui ipate rehema kwa Mungu ipumzike kwa amani. Amina.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU