Ask. Amani aagwa Moshi, awaachia ujumbe

·     

Kusimikwa kuwa Askofu Mkuu Arusha Aprili 8
Na Pascal Mwanache, Dar
ASKOFU Mkuu Mteule wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha Mhashamu Isaac Amani ameagwa rasmi na waamini wa Jimbo Katoliki Moshi katika Adhimisho la Misa Takatifu lililofanyika katika Kanisa Kuu la Kristo Mfalme Moshi, Aprili 4, 2018.
Akitoa homilia katika Misa hiyo Askofu Amani amewaasa waamini kuwa vyombo vya wokovu kwa kuwatetea wanyonge, kuwafariji, kupigania haki zao na kuwaonya wanaopotosha haki na kuwakosesha wengine amani. Amesema kuwa kila mkristo anapaswa kushiriki kazi ya Yesu ya kuwasaidia na kuwaimarisha wale wanaowahitaji, huku akitaka ukarimu wao uwe zaidi ya fedha na dhahabu.
“Ni lazima tuwashike mkono na tuwainue wale waliotengwa na wenye shida. Tunaowasaidia wanamshangilia Mungu kwa kuwa wameonja furaha ya uhai. Baada ya kufufuka Yesu hakufanya miujiza ya uponyaji, hivyo hilo ni jukumu letu kuwa vyombo vya wokovu” ameeleza.
Awali Askofu Amani ametoa salamu za Pasaka kwa waamini wa majimbo ya Moshi na Mbulu ambapo amesema kuwa Kanisa linapoadhimisha Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara inafaa kila muumini ajitathmini nafsi yake kwa kutafakari  jinsi anavyoelewa na kuishi maagano ya ubatizo.
Amesema kuwa baadhi ya waamini wanazo hali za kusikitisha hasa ushirikina, kutojali amri za Mungu na za Kanisa, kuishi usuria, kuendekeza chuki na kukataa kusameheana na kupatana. Amemtaka kila muumini atafakari changamoto hizo na kujiuliza anakwenda wapi na katika changamoto za kuishi maagano ya ubatizo.
“Wamisionari walituletea Injili ili ituangazie namna ya kuwa watoto wa Mungu na wa Kanisa. Chimbuko la ubatizo ni Pasaka; yaani mateso, kifo na ufufuko wa Mkombozi wetu Yesu Kristo. Ubatizo hutuingiza katika ushindi wa mkombozi. Je tunayo maisha ya ushindi? Je imani, matumaini na mapendo yetu yamejikita kwa Yesu mfufuka? Je ninajivunia kuwa mkristo na kuchangamkia ukristo?” amehoji Askofu Amani.
Aidha amesema kuwa tunda la ubatizo wa maji ni kufanya toba kwa kukataa maisha duni ya dhambi, chuki, uasi, mafarakano na hofu, hivyo amewataka waamini hao kukataa uasi na kila ubaya ili wawe safi.
“Ubatizo siyo ngonjera au maigizo; ubatizo huokoa; ubatizo ni kuzaliwa upya kwa maisha mapya. Uhai wa maisha mapya huonekana katika tabia za kusali, kupokea sakramenti, kusoma neno la Mungu, kujitahidi kushirikiana na wakristo wengine katika vyama vya kitume na kujitolea kuwasaidia wenye shida” amesema.

Askofu Amani anatarajiwa kusimikwa kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha hapo Aprili 8, kuanzia saa 3 asubuhi katika viwanja vya Kanisa Kuu la Mt. Theresia wa Mtoto Yesu.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU