Dodoma yapewa hadhi ya kuwa jiji

Na Dotto Kwilasa,Dodoma.
KATIKA maadhimisho ya miaka 54 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, iliyokuwa halmashauri ya Manispaa ya Dodoma imepandishwa hadhi na kuwa jiji.
Akihutubia wananchi katika sherehe hizo za muungano katika uwanja wa Jamhuri Dodoma hivi karibuni,Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli amesema kutokana na mamlaka aliyo nayo anatangaza rasmi kuupa hadhi ya jiji mji wa Dodoma.
Pamoja na hayo amesema, kutokana na kuupadisha  mji wa Dodoma kuwa na hadhi ya jiji , hivyo aliyekuwa Mkurugenzi wa Manispaa ataitwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma hatua  ambayo imeungwa mkono na wananchi waliokuwa uwanjani kusherehekea muungano .
Sambamba na hayo amesema dhamira ya serikali kuhamishia makao yake makuu bado ipo pale pale na kwamba zaidi ya watumishi wa serikali 3800 tayari wamehamia Jijini Dodoma.
Wakizungumzia hatua hiyo, baadhi ya wananchi mkoani humo wamesema  kutokana na Dodoma kutangazwa kuwa jiji mzunguko wa kibiashara utakuwa mkubwa na hivyo kuwa fursa kwa wawekezaji na wafanyabiashara wengine.
“Dodoma kuwa jiji ni fursa kubwa kwetu wafanyabiashara kwani itaongeza tija na uhamasishaji wa shughuli za maendeleo kupitia miradi mbali mbali iliyopo,” amesema mfanyabiashara mmoja .
 Wakati huo huo Rais Magufuli amesema serikali itaendelea kuulinda ,kuutunza na kuuimarisha muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa gharama yoyote ile na kamwe haitomwonea haya mtu yeyote atakaye diriki kuuvunja muungano uliopo.
“Mimi na Dkt Shein tutaendelea kuulindà muungano  kwa gharama yoyote kwani tunaamini muungano wetu ndiyo nguvu yetu na ninawahakikishia kuwa tupo imara ,” amesisitiza.
Hata hivyo Rais amewatoa hofu wananchi kwa kusema kuwa, licha ya kwamba muungano  huo unakabiliwa na changamoto ndogo ndogo za kimuungano, serikali za pande mbili yaani Tanzania bara na visiwani zimejipanga kutatua na kuondoa mizozo.
Pamoja na hayo amezitaja faida ambazo Tanzania inanufaika kwa muungano  huo kuwa ni pamoja na nchi kuheshimika, kuwa na nguvu ya pamoja,mafanikio katika nyanja za kiuchumi,kisiasa na kijamii pamoja na kutoa mchango wa harakati za kusuruhisha migogoro katika nchi nyingine.
Tanganyika na Zanzibar ziliungana kutokana na ukaribu wa kijiografia ,muingiliano wa masuala ya utamaduni na urafiki baina ya viongozi waasisi .
Sherehe za muungano mwaka huu zimehudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwemo Rais msaafu wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Benjamin Mkapa, Rais wa Zanzibar Dkt.Shein, Mawaziri Wakuu  Wastaafu ,wabunge na na viongozi mbalimbali wa nchi.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU