Vyombo vya habari vya Katoliki vyaaswa kufahamisha umma juu ya miaka 150 ya uinjilishaji

Na Julieth Muunga Dadi, Dar es Salaam
Wanamawasiliano wa Vyombo vya Habari vya Kanisa Katoliki wametakiwa kuweka mikakati madhubuti kupitia njia za mawasiliano ikiwemo Televisheni, Radio na Magazeti ili kurahisisha na kuendeleza utume wa Kanisa.
Aidha Vyombo hivyo vya habari viweke mikakati madhubuti ili kuelimisha na kufahamisha uma kuhusu Jubilei ya  Miaka 150 ya Ukristo Tanzania.
Wito huo umetolewa hivi karibuni na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Raymond Saba wakati akifungua Mkutano  Mkuu wa  Mwaka wa Wakurugenzi wa Mawasiliano Majimboni na wa Vyombo vya Habari vya Kanisa uliofanyika hivi karibuni Kurasini, Jijini Dar es salaam.
Padri Saba amesema kuwa,  kama wanamawasiliano hawana budi kuweka mikakati ya kuhamasisha waamini juu ya matukio mbalimbali katika Kanisa ikiwemo Maadhimisho ya Jubilei ya Miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara.
“Ni wajibu wa Vyombo vyetu vya Habari vya Kanisa Katoliki kuhakikisha waaamini wanajua, wanashiriki na kuyaishi yale yote mazuri yaliyokuwepo ndani ya Miaka 150 ya uinjilishaji ili waweze kuimarisha Imani yao,” amesema.
Aidha ameongeza kuwa ni vyema wakajenga utamaduni wa kusoma na kujifunza  masuala mbalimbali muhimu katika Kanisa ili yawasaidie katika kazi zao za kila siku sambamba na kuzingatia matumizi fasaha ya lugha.
Kwa Upande wake Mkurugenzi wa Mawasiliano Jimbo Kuu Katoliki  Dar es Salaam, Padri Joseph Masenge wakati akiwasilisha mada ya  weledi katika Uandishi wa habari na uandaaji wa vipindi amesema uandishi ni wito , hivyo kama wanamawasiliano wanapaswa kufanya kazi kwa weledi na haki sambamba na kuzingatia maadili ya Uandishi wa Habari.
“Si sahihi kuongeza maneno ama kumlisha mtu maneno ili kuuza gazeti. Si sahihi kupindisha ama kukuza vichwa vya habari kwa ajili ya soko la gazeti. Maadili ya uandishi ndiyo ninayosisitiza.
Andikeni kwa ufasaha, ubunifu na weledi ili kuhabarisha umma na kujiaminisha katika jamii,” amesisitiza Padri Masenge.

Mkutano huo wa Mwaka wa Wanamawasiliano uliwakutanisha Wakurugenzi  wa Majimbo nane wakiwemo wasimamizi  wa vipindi  kutoka katika Redio zinazomilikiwa  na Kanisa Katoliki majimboni ikiwemo Tumaini Media, Redio Ukweli ya Morogoro, Redio Mwangaza ya Dodoma, Redio Fadhila ya Tunduru Masasi, Redio Faraja ya Shinyanga, Redio Chemchem ya Sumbawanga, Redio Huruma ya Tanga, Redio Mbiu ya Bukoba iliyopo kwenye majaribio na Redio Maria Tanzania.
Kanisa Katoliki Tanzania lina jumla ya Majimbo 34 kati ya hayo Majimbo Makuu ni sita ambayo ni Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Arusha, Tabora, Mwanza, Dodoma na Songea.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU