‘Bila ushirikiano wa Serikali na Kanisa hakuna maendeleo’


Na Izack Mwacha Singida
ASKOFU wa Jimbo Katoliki Singida Mhashamu Edward Mapunda, ameipongeza serikali ya Mkoa wa Singida, kwa kutoa ushirikiano na Kanisa katoliki katika shughuli za maendeleo.
Askofu Mapunda ameyasema hivi karibuni katika uzinduzi wa miaka 22 ya Radio Maria Tanzania iliyofanyika Parokia ya moyo Mtakatifu wa Yesu Jimbo Katoliki  Singida.
Katika homilia yake Askofu Mapunda amesema kuwa ushirikiano ukidumishwa Kati ya serikali na Kanisa ni lazima maendeleo yawepo,kwani miongoni mwa mambo ambayo yanaleta chachu ya Nguvu, umoja na mshikamano ni ushirikiano ambao kwa kiasi kikubwa unaleta hali ya kujaliana, hivyo anategemea maendeleo makubwa zaidi katika Jimbo la singida
Askofu mapunda amesisitiza kuwa, ili imani ya Kanisa Katoliki iendelee kudumu zaidi ni lazima kwa kila mkristo mkatoliki mmbatizwa afahamu umuhimu wake wa kuchangia vyombo vinavyoweza kuisambaza injili hiyo kwa kasi zaidi ulimwenguni kote ikiwemo Radio Maria, kwani hiyo ni njia pekee ambayo ina uwezo mkubwa zaidi wa kuhubiri neno la Mungu haraka zaidi na kwa kasi kubwa.
“Kuna mtu alijitokeza wakati nikiwa Ulaya akataka kunipa Radio, nami nikamwambia sidhani kama ninahitaji Radio maana nchini Tanzania kuna RAadio Maria na Redio ya mama inatosha’’ amesema Askofu Mapunda.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Singida Dr Rehema Nchimbi ambaye alikuwa ni mgeni rasmi katika uzinduzi huo, amewataka wakristo kote ulimwenguni kujiwekea Utaratibu maalum wa kusali Rozari Takatifu, huku akisisitiza kuwa, Pamoja na mambo mengi ambayo yanafanyika hapa duniani, ni lazima yasindikizwe na nguvu ya sala kwani sala pekee ndiyo silaha ya kukuweka mbali na muovu shetani.
“Waamini wenzangu naomba mtambue ya kuwa  Salamu Maria moja Ina nguvu kuliko bomu la nyuklia.
Kama unataka kuwa mkandarasi mzuri ambaye hakuna hata mtu mmoja anayeweza kukuondoa katika kazi yako basi ni lazima kwanza uwe mkandarasi wa Yesu,” amesema Dr Nchimbi huku akisema ya kwamba kujitoa katika matukio mbalimbali ya Kanisa pamoja na kusali ndiyo mahusiano pekee yanayodumu milele kwani yanakuwa yameunganishwa na Mungu ambayo hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kuyavunja kamwe.
Sanjari na hayo Dr Nchimbi ametoa zawadi ya Rozari  elfu mbili kwa Radio Maria Tanzania huku akisema kuwa itakuwa chachu ya kuwajengea mazingira mazuri zaidi waamini katika sala, kwani kupitia Rozari Takatifu miujiza mingi zaidi inawatokea wanaosali kwa imani.
Naye Mkurugenzi wa Matangazo Radio Maria Tanzania Padri John Maendeleo, amewashukuru viongozi wote wa Kanisa waamini, pamoja na viongozi wa Serikali ambao walijitokeza kwa furaha kubwa katika uzinduzi huo na kusema kuwa kuwezesha habari njema kufikia watu wengi zaidi kupitia Radio Maria ni sawa na Kupanda mbegu katika udongo mzuri, jambo ambalo linakupa uhakika wa kujipatia mazao mengi na  ya kutosha siku za usoni.
Uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 22 ya Radio Maria Tanzania umefanyika Jimboni Singida, huku kilele chake kikiwa ni Tarehe 1/7/2018 Jimboni humo.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU