WAZAZI IRINGA WATAKIWA KUWASOMESHA WATOTO WA KIKE

n Na Getrude Madembwe, Iringa

WITO umetolewa kwa wazazi na walezi kuona umuhimu wa Elimu kwa kuwasomesha watoto wa kike ili waweze kutimiza ndoto zao na kulisaidia Taifa katika nyanja mbalimbali.
Wito huo umetolewa hivi karibuni na mgeni rasmi kwenye mahafali ya pili ya shule ya sekondari ya wasichana ya Regina Pacis, Josephat Mwagala inayomilikiwa na Jimbo Katoliki Iringa parokia ya Kibao, yaliyofanyika shuleni hapo.
Mwagala amesema kuwa kumekuwa na fikra potofu kuwa kumsomesha mtoto wa kike ni kupoteza rasilimali fedha kitu ambacho amesema siyo kweli kwani maisha ya sasa bila elimu ni changamoto kubwa hasa kwa mtoto wa kike.
Mwagala amesema kuwa mtoto wa kike akipatiwa elimu kuna uwezekano mkubwa kwa taifa kuwa na maendeleo kutokana na kuwajibika kwao katika maisha ya kila siku, hivyo wazazi na walezi ni muhimu kuwasomesha watoto wa kike kwa lengo la kuendeleza ndoto walizonazo.
Wakati akijibu risala ya shule, mgeni huyo rasmi ametoa kiasi cha Tsh.300, 000 kwa ajili ya walimu ikiwa ni pongezi kwa kazi nzuri wanayoifanya na ameahidi kukabidhi mifuko 100 ya saruji, kuchimba visima viwili vya maji vyenye thamani ya Tsh. Milioni 3 kwa ajili ya matumizi ya wanafunzi.
Aidha katika mahafali hayo ameongoza harambee ya ununuzi wa keki ambapo kiasi cha Tsh.700, 000 kimepatikana.
Ameipongeza shule hiyo kwa kuwa moja ya shule zinazofanya vizuri mkoani Iringa kielimu na kitabia kwani ni moja ya shule ambazo idara ya elimu haipati malalamiko ya mara kwa mara kutoka shuleni hapo.
Amewataka wahitimu hao kuyasoma vyema mazingira ya maisha popote watakapokuwa na kuamua namna ya kujiajiri ili mradi isiwe shughuli zinazopingana na sheria na maadili ya kijamii, kama vile kuuza dawa za kulevya, ukahaba, unyang’anyi na mambo mengine yanayofanana na hayo ambayo watajiingiza matatani na kuonekana wabaya.
‘Ninawaomba mkirudi nyumbani kwa muda huu mfupi wa kusubiri matokeo, zingatieni maadili mliyofundishwa mkiwa hapa shuleni, bado nyie ni wanafunzi, hakikisheni mnajiepusha na mambo yasiyofaa ambayo yanaweza kukatisha ndoto zenu za kuendelea na masomo ya juu,” Ameasa  Bw. Mwagala.
Awali Mkuu wa shule ya wasichana Regina Pacis, Marco Shayo akimkaribisha mgeni rasmi amesema kuwa uongozi wa shule umeweka mikakati mbalimbali inayoendelea kutekelezwa ikiwa ni pamoja na ujenzi wa jengo la shule linaloendelea kujengwa, kuchimba visima vya maji ili maji yaweze kukidhi mahitaji ya wanafunzi.
Shayo amewasihi wahitimu hao kuyazingatia maadili waliyoyapata wakiwa shuleni hapo ili waweze kuepukana na vishawishi vitakavyoweza kukatiza ndoto zao na hatimaye kuwaingiza katika mambo yasiyofaa katika jamii na Taifa kwa ujumla.  
Pamoja na mafanikio mengi, lakini shule inakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo upungufu wa nyumba za walimu, uhaba wa vyumba cha maktaba na upungufu wa visima vya maji.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU