UTOAJI MIMBA, VIDHIBITI MIMBA TISHIO NCHINI

n Na Pascal Mwanache, Dar

IMEELEZWA kuwa utoaji wa mimba na matumizi ya vidhibiti mimba ni dhana zinazolenga kuharibu taifa na kushambulia maadili, utamaduni na imani ya taifa huku dhana hizo zikiwa ni itikadi ovu za magharibi za kudhibiti ukuaji wa idadi ya watu.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa Shirika la Kutetea Uhai nchini (Pro life) Emil Hagamu katika tathmini yake ambapo amesema kuwa utoaji wa mimba na matumizi ya vidhibiti mimba ni vitu vigeni kwa waafrika na ili vikubalike hutumika kampeni na propaganda yenye maneno mazuri ili kuficha uovu uliomo ndani yake.
“Taifa lolote linaweza kuangamizwa njia ya vita. Vita kubwa tunayopigwa watanzania ni mashambulizi dhidi ya maadili ya Taifa ambayo ndiyo yanayotafsiri jamii ilivyo. Ukiua utamaduni unaojenga misingi ya maadili na imani utakua umeua taifa. Na ukitaka kuua vizuri Taifa basi lenga kwa vijana, ukibomoa misingi ya hawa lazima utamomonyoa taifa”
Aidha amesema kuwa fikra za kuzaa, idadi ya watoto, na namna ya kupishana kwa watoto ni sehemu ya mila na desturi za watu husika, ambapo tangu mwanzo mwanadamu amekuwa na uelekeo wa kupenda kuzaa watoto wengi.
Ameongeza kuwa Afrika inaongoza kwa kuwa na desturi ya kupenda na kuthamini uhai wa mwanadamu ndiyo maana watoto ni kitu cha thamani sana katika jamii zao.
“Watu wa Ulaya wamepita katika miongo mbalimbali, imefikia mahali wameharibikiwa. Hivyo mawazo na itikadi zao ovu ndizo zinazoletwa kwetu Afrika hasa Tanzania. Wanaleta kampeni za kudhibiti ukuaji wa idadi ya watu kwa kuweka matumizi ya vidhibiti mimba na utoaji mimba. Wanatumia maneno mazuri kama afya ya uzazi, yaani wanaangalia uzazi kama kitu kinachoharibu afya” amesisitiza.
Amesema kuwa ni uongo mkubwa kusema uzazi wa mpango unapunguza mimba zisizotarajiwa, na kusema kuwa uzazi wa mpango unachochea mimba zisizotarajiwa, akitolea mfano wa nchi ya Marekani ambako kuna kiwango cha udhibiti mimba kwa asilimia 80 lakini bado kuna sheria za utoaji mimba zimetungwa.
“Wanasema vidhibiti mimba vinasaidia kupunguza vifo vya kina mama na watoto, hii siyo kweli. Kinachosaidia kupunguza vifo vya kina mama na watoto ni mipango mizuri, utashi wa kisiasa na huduma bora za afya. Ni kuelimisha wahudumu, kuwa na vifaa vya kutosha na wataalamu, kutoa huduma kwa uzalendo ili mhudumiwa aone kuwa sehemu ya huduma ni sehemu salama na siyo sehemu ya kifo” ameongeza.
Ameeleza kuwa dawa zinazotumika kudhibiti mimba zinageuza uzazi kuwa ugonjwa na mtoto anayepatikana na uzazi kuwa balaa, huku akitahadharisha kuwa kiwango cha wanawake wanaoshindwa kupata mimba kinaongezeka ikiwa ni madhara ya matumizi ya dawa hizo. 
Pia amesema hiyo inaashiria kuwa kwa sasa uwezekano wa wasichana kuolewa ni mdogo kuliko ilivyokuwa zamani, na kubainisha kuwa asilimia 25 ya wasichana wanaotumia vidhibiti mimba chini ya umri wa miaka 25 wanapata saratani ya matiti.
Katika hatua nyingine Ndugu Hagamu ametahadharisha kuwa kuna sera zinazotekelezwa na serikali na washirika wengine juu ya afya ya uzazi ambazo zinaweza kuliangamiza taifa, kwani walengwa wa sera hizo ni vijana kuanzia miaka 15, ambapo amesema kuwa umri huo siyo sahihi kuwachanganyia mitaala ya mahusiano.
“Mtoto hastahili kuzaa wala kupanga uzazi kwani kwa umri huu anastahili kuwa shuleni. Huu ni umri wa makuzi na malezi na kwa kuwa hajafikisha miaka 18 anakuwa yupo chini ya uangalizi wa wazazi. Sasa inastaajabisha, eti watoto wa miaka 15 wanawekwa kwenye kampeni za kuwafundisha afya ya uzazi ikiwa ni pamoja na haki ya kuwa huru katika kufanya maamuzi ya mahusiano na jinsia. Wanafundishwa shuleni na vyuoni mambo haya, na wanayaita afya ya uzazi kwa vijana. Hili taifa linakwenda wapi?” amehoji.


Comments

  1. Ameeleza kuwa dawa zinazotumika kudhibiti mimba zinageuza uzazi https://digg.com/u/tuvanphathai kwani walengwa wa sera hizo ni vijana kuanzia miaka 15, ambapo amesema kuwa umri huo siyo sahihi kuwachanganyia mitaala

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU