SEMINARI ARUSHA YAFANYA JUBILEI YA MIAKA 50 

ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha Mhashamu Josaphat Lebulu amesema kuwa Shule za Seminari hapa Nchini zimekuwa mfano bora katika kukuza maadili kwenye jamii kutokana na malezi bora ya kiroho na kimwili.
Askofu Mkuu Lebulu ameyasema hivi karibuni alipokuwa akiongoza Misa ya Jubilee ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Seminari ya Arusha iliyopo Oldonyo Sambu Jimbo Kuu Katoliki Arusha.
Amesema kuwa tangu kuanzishwa kwa seminari hiyo iliyoanzishwa mwaka 1967 lengo likiwa ni kulea vijana wa kiume kuwa mapadri na kupata wakristo wenye maadili mema katika jamii, kumekuwa na mafanikio makubwa ambayo yameisaidia Serikali na jamii kwa ujumla kubadilisha mienendo ya vijana ambao walikuwa na tabia mbaya.
“Seminari zimekuwa zikifundisha vijana wote bila kujali itikadi za Dini mambo ya kiroho na kimwili na kujua mpango wa Mungu katika maisha yao huku wakifundishwa kutambua kwamba binadamu wote ni sawa kwa kuheshimu utu wa mtu,” Amesema.
Kutokana na Elimu inayotolewa na Shule za Seminari, Serikali na jamii imekuwa na watu wenye maadili na hofu ya Mungu wanaofanya kazi katika sekta mbalimbali ambao wanafuata Sera za Taifa kutokana na maadili waliyonayo.
“Tunamshukuru Mungu kufikia hatua hii tangu kuanzishwa kwa seminari hii tumekuwa na mafanikio makubwa hususani kuelimisha maadili ya Kiafrika wapo vijana wanakuja wakiwa na tabia mbaya lakini wakifika hapa tunawabadilisha na hatimaye wengine ni viongozi wazuri sana katika Kanisa na Serikali,” amesema Askofu Mkuu Lebulu.
Seminari zimekuwa zikifundisha vijana wote bila kujali itikadi za Dini mambo ya kiroho na kimwili na kujua mpango wa Mungu katika maisha yao huku wakifundishwa kutambua kwamba binadamu wote ni sawa kwa kuheshimu utu wa mtu.
Amewataka vijana wenye wito kutokata tamaa mbali na changamoto wanazokumbana nazo ambapo wengi wao wameishia njiani, bali wanapaswa kuzingatia yale wanayofundishwa ili waweze kutimiza malengo yao.
Ameongeza kuwa wapo baadhi ya viongozi wa Kanisa na Serikali ambao wamekuwa hawasemi ukweli pale mtu anapokosea wanaficha ukweli hivyo kuwa na ukosefu wa maadili.
“Kama kiongozi wa Kanisa na Serikali mnapaswa kuwa wakweli mbele za Mungu mtu akikosa mkosoeni na kumwambia ukweli kwani ukweli bila maadili hupoteza malengo,” amesema Askofu Mkuu Lebulu.
Naye Gombera wa Seminari ambaye ndiye msimamizi Mkuu Padri Edwin Kiromo amesema kuwa mbali na elimu ya kiroho wamekuwa wakitoa elimu ya kilimo na ufugaji, afya, uhifadhi wa mazingira kwa kujenga miundombinu jambo ambalo limesaidia wanafunzi kujitambua na kufanya kazi za mikono.
Mbali na mafanikio waliyoyapata ya kuwa na hospitali, shule na vituo vya watoto yatima bado wamekumbana na changamoto nyingi zikiwemo kuchakaa kwa miundombinu ya Seminari hiyo, uchakavu wa Kanisa wanalotumia kusali, mabweni hayatoshi ikiwa ni pamoja na fedha za kuendesha seminari hiyo.
Hata hivyo seminari hiyo ina mipango endelevu ya kudumisha umoja uliopo, kurudisha kidato cha tano na sita, kuongeza wanafunzi, kuwezesha kupata viongozi wenye kiwango cha juu ,kuwapata wataalamu wa Kanisa wazuri na viongozi wa walei, kuongeza mabweni pamoja na nyumba za walimu.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa wanaseminari waliosoma Seminari ya Arusha, Oldonyo Sambu, George Stephen wameamua kuanzisha umoja wao ili kuendeleza yake mema waliyoyakuta kwa kurudisha shule hiyo kuleta maendeleo ambapo wamezindua madarasa matatu ambayo ni matunda yao kwa nia ya kutoa shukrani kwa elimu na maadili waliyoyapata shuleni hapo.
Amewataka wale wote wanaomaliza shule walizotoka kuwa na kasumba ya kurudisha fadhila kwa kujenga miundombinu ikiwa ni manufaa kwa vizazi vijavyo.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU