Miaka 56 ya uhuru

Tanzania inahitaji awamu ya pili kupigania uhuru

Na Pascal Mwanache, Dar

IMEELEZWA kuwa Tanzania inapaswa iingie katika awamu ya pili ya kupigana vita vya uhuru wa kiuchumi ili kuondokana na hali ya kuwa koloni la mfumo wa kimataifa wa uchumi.
Hayo yameelezwa na Mkuu wa Idara ya Haki, Amani na Uadilifu wa uumbaji ambaye pia ni Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uchungaji Katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Dkt. Camilius Kassala, alipoangazia tathmini ya miaka 56 ya uhuru wa Tanganyika.
Dkt. Kassala ameeleza kuwa hakuna njia yoyote ya kuondokana na umaskini isipokuwa kupigana vita ya ukombozi wa kiuchumi, ili usimamizi wa kiuchumi na rasilimali uwe mikononi mwa watanzania.
“Ili kuweza kufika hapo kunahitaji awamu ya pili ya kupigania uhuru, kutoka kisiasa kwenda kiuchumi. Tafakari maswali haya: Vitu tunavyonunua madukani, asilimia ngapi vinatengenezwa hapa nchini? Asilimia ngapi ya wanataaluma wetu wanaomaliza vyuoni wanaingia katika sekta ya uchumi ili wausimamie? Bidhaa tunazouza nchi za nje, kwa kiwango gani tuna maamuzi kuhusu bei zake? Na ukilinganisha wawekezaji wa nje na wa ndani, upande upi ni wengi zaidi” amehoji Dkt. Kassala.
Pia amesema kuwa katika kipindi cha miaka 56 tangu ipate uhuru, nchi inajivunia mambo mengi ikiwa ni pamoja na kuthamini uelewano, kutojali tofauti za kidini na kikabila, kuwa na lugha moja ya kitaifa, kuwa na kiwango cha demokrasia, na kuwa na uchumi ambao unakidhi mahitaji ya lazima ya wananchi.
Kuhusu kiwango cha demokrasia nchini Dkt. Kassala amesema kuwa Tanzania inajivunia demokrasia kwa kiwango kinachozidi wastani wa demokrasia katika nchi nyingi za kiafrika. Pia amesema uelewa wa watanzania kuhusu haki zao ni wa kiwango cha juu, ambapo mara nyingi wanatafuta namna ya kupata haki zao bila kuvuruga amani.
Amesema kuwa ili kuimarisha demokrasia nchini serikali haina budi kutoa uhuru wa habari na uhuru wa shughuli za siasa ili watu wapewe fursa ya kuwa huru katika sekta ya habari.
“Hata hivyo tunahitaji demokrasia ipanuke zaidi ambapo elimu ya siasa inapaswa ifundishwe katika shule na vyuo, hii itasaidia kuepukana na upotoshaji wa maswala ya siasa kama ilivyo sasa” ameongeza.
Aidha amebainisha kuwa sera za uchumi zinapaswa ziangaliwe upya ili kukabiliana na mfumo wa ubepari unaoashiria kurudi hasa kuongezeka kwa matabaka ambapo wachache wa tabaka la juu wanachukua sehemu kubwa ya mapato ya taifa kuliko wengi, na hivyo kuwakosesha kufurahia matunda ya uhuru.
Kuhusu utoaji wa huduma za jamii, Dkt Kassala ametaka viwango vya ubora wa huduma za jamii kama vile matibabu, elimu, makazi na usafiri vifanyiwe kazi ili viongezeke. Kuhusu suala la ajira amesema linapaswa lihusishwe na mfumo wa elimu na mafunzo na lisibaki mikononi mwa sekta binafsi.
Wakati huo huo Dkt Kassala ametahadharisha kuwa vita dhidi ya rushwa na ufisadi haviwezi kushinda nje ya utaratibu wa maadili. Amesema kuwa badala ya kuwa na TAKUKURU, Tume ya Maadili ya viongozi iangalie suala la rushwa kwa mtazamo mpana.
“Wanajaribu kuangalia katika umiliki wa mali, lakini kwa sasa viongozi wana fursa nyingi za kumiliki mali bila kuvunja sheria. Kila kiongozi anayesajili mali zake aeleze amezipata kwa njia gani” amesisitiza.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU