Ulinzi waimarishwa Dodoma kuelekea sherehe za uhuru

JESHI la Polisi Mkoani Dodoma limeendelea kuimarisha ulinzi kwa kufanya operesheni mbalimbali na misako, katika kuelekea maadhimisho ya miaka 56 ya Uhuru wa Tanganyika, yatakayofanyika mkoani humo Disemba 9 mwaka huu.
Kamanda wa Polisi mkoani Dodoma Kamishna Msaidizi Mwandamizi Gilles Muroto amesema kuwa kwa sasa Mkoa wa Dodoma una wageni wengi waliokuja kwa ajili ya shughuli za sherehe ya uhuru ambazo kitaifa zinafanyika mkoani hapo ambapo wahalifu hutumia nafasi hiyo kufanya vitendo vya kihalifu.
Akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni mkoani Dodoma, Kamanda Muroto ameongeza kuwa kufuatia upekuzi utakaohusisha  nyumba za wageni na doria, jeshi la polisi limefanya kazi nyingine za misako ambapo wamekamata watu watatu wakiwa na meno ya tembo, yenye uzito wa kilogram 16 yaliyokuwa yamebebwa kwenye pikipiki kutoka Kondoa yakipelekwa  Dodoma mjini.
Pia amesema zoezi la kubomoa vibanda vya biashara visivyo rasmi eneo la Railway linaendelea likisimamiwa na vyombo mbalimbali vya ulinzi na usalama na kuwa ubomoaji huo unalenga kupanua ujenzi wa miundombinu ya reli baada ya eneo hilo kuvamiwa na wafanyabiashara ambapo katika zoezi hilo wamekamata watuhumiwa watatu kwa makosa ya wizi wa mali za wafanyabiashara.
“Kufuatia sherehe za maadhimisho ya uhuru wakazi wa mji huu wanapaswa kuwa waadilifu ili kuiendeleza amani ikiwa ni pamoja na kusaidiana na jeshi la polisi kuwafichua wahalifu watakaojitokeza,” amesema.
Sambamba na hayo ametoa tahadhari kwa watu wanaokwenda Dodoma kufanya uhalifu kuwa sehemu hiyo siyo  salama kwao  na kutoa wito kwa wakazi wa Dodoma katika kipindi hiki  kinachoambatana na shamrashamra nyingi wawe watulivu , wafanye shughuli zao kwa kufuata sheria na watumie fursa hiyo kujiletea maendeleo halali na kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama kuwafichua wahalifu wote.
Maadhimisho ya siku ya uhuru wa Tanganyika yanafanyika kitaifa mkoani Dodoma huku Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania John Magufuli akitajwa kuwa mgeni rasmi.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU