KARDINALI PENGO APONGEZA JUHUDI ZA ASKOFU SANGU 

n Na Joachim Mahona, Shinyanga.

ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar-es-salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amepongeza juhudi mbalimbali zinazofanywa na Askofu wa Jimbo Katoliki Shinyanga Mhashamu Liberatus Sangu za kulistawisha Jimbo na kutoa huduma mbalimbali za kijamii jimboni humo.
Akizungumza mara baada ya kuongoza misa takatifu ya dominika ya kwanza ya majilio katika Kanisa Kuu la Mama Mwenye Huruma Ngokolo mjini Shinyanga wakati wa kuhitimisha ziara yake ya siku nne aliyoifanya jimboni Shinyanga, Kardinali Pengo amebainisha kuwa amepata faraja kubwa baada ya kutembelea miradi mbalimbali na kuona jinsi Askofu Sangu anavyofanya juhudi kubwa za kulistawisha Jimbo kwa kushirikiana na mapadri na waamini kwa kipindi kifupi tu cha miaka miwili tangu aanze utume wake.
“Narudi Dar-es-Salaam nikiwa naamini kuwa Jimbo hili limepiga hatua kubwa katika hali ya kushangaza, nilikuwa na wasiwasi wakati wa kumwekea mikono siku ile tuliyokuwa tukimweka wakfu kuwa Askofu wa Shinyanga.  Lakini kwa sasa nimefarijika sana kuona akifanya juhudi mbalimbali za kulistawisha Jimbo hili,” Amesema.
Kardinali Pengo ametumia nafasi hiyo kuwataka mapadri wa Jimbo Katoliki Shinyanga kuwa na umoja na kuendelea kushirikiana na Askofu wao ili kazi anazozifanya ziwe za mafanikio.
Katika hatua nyingine Kardinali Pengo amemuomba Askofu Sangu kuhakikisha anafanya juhudi za kuongeza idadi ya parokia mpya ili Jimbo liwe na parokia nyingi zaidi na kwa kuanza aanze  na malengo ya kuwa na parokia 75 kwani kwa sasa Jimbo lina parokia 32 tu.
“Mimi wakati naanza kufanya utume katika Jimbo Kuu Katoliki Dar-es-salaam mwaka 1992, nilikuta kukiwa na parokia ishirini tu (20), lakini niliwatangazia waamini wa Dar-es salaam kuwa lazima tumwongezee wachumba Kristo, maana Kanisa ni mchumba wa Kristo. Kwa hiyo watu walihamasika mpaka sasa tumefanya juhudi na kufikisha parokia 107. Kwa hiyo baba Sangu jitahidi kuongeza parokia nyingi zaidi ya ulizonazo hivi sasa na ikiwezekana ujiwekee malengo ya kawaida ya kufikia parokia 75.”
Kardinali Pengo pia amepongeza wazo la Askofu Sangu la kuanzisha kituo cha kulelea watoto yatima kiitwacho (Bishop Sangu Orphanage Centre) kilichopo katika eneo la Uzunguni mjini Shinyanga. Hatua ambayo imeonesha upendo na ubinadamu kwa watoto hao ambao ni miongoni mwa makundi yaliyoko katika dhiki kubwa na yaliyosahauliwa.
Naye Askofu Sangu amemshukuru Kardinali Pengo kwa ukarimu uliouonyesha kwa kukubali kulitembelea Jimbo Katoliki Shinyanga katika ziara ambayo aliitaja kuwa imewajenga waamini kiimani.  Ametumia nafasi hiyo kumwalika tena katika uzinduzi wa Jubilei ya miaka 25 ya parokia ya Kanisa Kuu la Mama Mwenye Huruma Ngokolo na Jubilei yake ya miaka 25 ya upadri. Uzinduzi ambao unatarajiwa kufanyika mwezi Agosti mwaka 2018.
Ziara ya Kardinali Pengo ya siku 4 katika Jimbo Katoliki Shinyanga ilikuwa mwaliko maalum aliopewa na Askofu Liberatus Sangu ambayo pamoja na mambo mengine ilikuwa na lengo la kuwaimarisha kiimani waamini, kudumisha umoja wa Kanisa na kujenga mahusiano kati ya majimbo mawili ya Shinyanga na Jimbo Kuu Dar-es-salaam.
Akiwa katika ziara hiyo jimboni Shinyanga,  Kardinali Pengo alifanya shughuli mbalimbali za kuweka mawe ya msingi na kubariki mahali ambapo patajengwa  nyumba ya mapadri katika parokia teule ya Lubaga, jengo la kituo cha kulelea watoto yatima ambacho kinatarajiwa kuanzishwa na Askofu Sangu katika eneo la Uzunguni mtaa wa Mitimirefu yalipokuwa makazi ya aliyekuwa Askofu wa tatu wa Jimbo Katoliki Shinyanga  hayati  Aloysius Balina, jengo la hosteli mpya za mapadri zinazoendelea kujengwa katika eneo la Ngokolo mitumbani mjini Shinyanga, jengo la ofisi mpya za parokia  zinazoendelea kujengwa  katika Kanisa Kuu la Mama Mwenye Huruma Ngokolo, kubariki na kufungua kikanisa cha kuabudia Ekaristi takatifu katika parokia ya Ngokolo pamoja na kuwapa  komunyo ya kwanza waamini wapatao 222 katika adhimisho la misa takatifu Dominika ya kwanza ya Majilio iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Ngokolo Desemba 3, 2017.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU