‘Wanaovaa rozari bila kusali wanakufuru’

θ  Wamo wasanii, waamini na wanaoning’iniza kwenye magari

WAAMINI nchini wametakiwa kutumia vizuri visakramenti ikiwemo Rozari Takatifu ili waweze kuimarika kiimani. Rai hiyo imetolewa kwa nyakati tofauti na Askofu wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Desderius Rwoma na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Padri Raymo nd Saba, ambapo wote wamekemea tabia ya watu kuvaa rozari bila kusali.
Akiongoza Misa Takatifu ya ufunguzi wa Kongamano la TYCS Kitaifa Askofu Rwoma amesema kuwa rozari siyo pambo la kuvaliwa au kuwekwa ndani, bali inamtaka muumini kuitumia kwa kusali na kuimarika kiroho.
Aidha Askofu Rwoma amekemea tabia ya wasanii kuvaa rozari katika kazi zao huku matendo wanayofanya katika nyimbo zao au filamu kutoendana na uwepo wa rozari hizo.
“Unakuta wasanii wanavaa rozari kwenye nyimbo zao lakini yanayotendeka humo hayafanani kabisa. Tumieni visakramenti hivi vizuri, mnaovaa rozari mkumbuke kwamba siyo pambo hilo. Rozari iwasaidie kumpenda Bikira Maria na kuimarika kiimani” ameasa Askofu Rwoma.
Kwa upande wake Padri Raymond Saba amesema kuwa kitendo cha kuvaa rozari bila kusali au kuning’iniza kwenye magari bila kusali ni ushirikina. Amewaasa waamini kusali rozari kila siku siyo kusali kwa kibiashara, yaani kusali wakati wa shida pekee.
“Kama unavaa rozari au unatundika kwenye gari bila kusali, huo ni ushirikina. Rozari kazi yake ni kusali kila siku, siyo kusali kibiashara yaani kusali kwa nipe nikupe, kusali pale tu unapokua na shida. Daima mdumu katika kusali rozari” ameeleza Padri Saba.
Mwezi Mei na Oktoba kila mwaka waamini wakatoliki wanaalikwa kusali rozari kwa ajili ya nia mbalimbali, lakini daima sala ya rozari inapaswa kusaliwa kila siku na kila wakati.

Comments

  1. Asante sana Baba Padri Raymond Saba na Baba Askofu Rwamo.

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU