Kongamano la Utoto Mtakatifu (Haki na Amani) kufanyika Juni Zanzibar

Kongamano la utoto Mtakatifu-Watoto wa Haki na Amani linatarajiwa kufanyika Jimboni Zanzibar kuanzia tarehe 8-11 Juni mwaka huu.

Hayo yamesemwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Zanzibar Mhashamu Augustine N.Shao C.S.Sp hivi karibuni ambapo amewaalika waaamini kuwaandaa watoto kwa ajili ya Kongamano hilo.
Askofu Shao amesema Kongamano hili ni sehemu ya Umisionari wa Watoto kwa watoto wenzao  wa Zanzibar na wakristo kwa ujumla.

Katika Kongamano hilo watoto wataonesha vipawa vyao katika kumsifu Mungu, kushirikishana zawadi walizojaliwa na Mwenyezi Mungu katika michezo, sala na kufurahia kwa pamoja kama familia.
Askofu Shao ameomba waamini waungane na watoto hao katika kusali na kuiombea Dunia amani ambayo ni lazima ianzie kwenye familia na kuwa na umoja.

Kauli mbiu ya kongamano hilo ni “UPENDO NA MSAMAHA UHAI WA FAMILIA” ambayo imejikita katika kutafakari nguvu ya msalaba na Neno la Mungu. “Kristo amekuja ili tuwe na uhai tena tuwe nao kamili” (Jn.10:10)

Wakati huohuo, Paroko wa parokia ya Mjini  Unguja, Jimbo Katoliki Zanzibar Padri Richard Haki akishirikiana na Padri Mathias C.S.Sp, wamewaomba waamini wakristo kuwachangia chochote watoto wa Haki  na Amani ili kuweza kufanikisha Kongamano hilo.
Amesema kongamano hilo litawakusanya watoto kutoka Tanzania Bara na visiwani, hivyo wawe na muamko wa kuwachangia watoto hao kwa sababu ni neema kwa Zanzibar kupata nafasi ya kuandaa Kongamano hilo.
Hata hivyo Padri Haki amesema kuwa ndani ya sherehe hizo kutakuwepo na masomo tofauti tofauti ya kumjenga mtoto kiakili hususani katika masuala ya Imani.
Padri Haki  amewasihi wazazi na vijana kuwachangia watoto hao ili kufanikisha zoezi hilo la sherehe ya watoto wa Haki na Amani itakayofanyika mwezi wa sita katika viwanja vya shule ya Francis Maria Libermann Zanzibar.
Naye Padri  Padri Mathias akinukuu injili ya Mathayo 7:7 kuwa “ombeni nanyi mtapewa tafuteni nanyi mtapata” kuwasihi waamini kujitoa kwa kutoa michango na majitoleo yao kwa wakati.
Katika harambee iliyofanyika ndani ya muda mfupi baada ya ibada ya Misa ya Jumapili ya pili ya Pasaka, zilipatikana fedha za kitanzania shilingi 404,000 kutoka kwa waamini wa Kanisa la Minara Miwili.
Mapadri hao waliwashukuru waamini kwa mchango wao walioutoa kwa ajili ya watoto wa haki na amani.
Misa ya Ufunguzi wa Kongamano hilo itaadhimishwa tarehe 9 Juni  na Askofu Augustine Shao na kutakuwa na mada mbalimbali za majiundo katika Imani na kuzidi kutambua upendo wa Mungu kwetu.
Kongamano hilo  la Kanda za Mashariki na Kati linajumuisha majimbo 9 pamoja na Zanzibar yenyewe. Majimbo ya Kanda ya Mashariki ni Jimbo Kuu Dar Es Salaam, Jimbo Katoliki Tanga,  Jimbo Katoliki Morogoro,  Jimbo Katoliki Ifakara, Jimbo Katoliki Mahenge na  Jimbo Katoliki Zanzibar. Majimbo ya Kanda ya Kati ni Jimbo Kuu Dodoma, Jimbo Katoliki Singida na Jimbo Katoliki Kondoa.

Jimbo Katoliki Zanzibar linalojumuisha Visiwa vya Unguja na Pemba, lina Parokia zipatazo 8 na 1 tarajiwa.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU