Mfuko wa Graca Machel kuinua elimu Musoma






Na Veronica Modest, Musoma.

SERIKALI Mkoani Mara imewaondoa hofu walimu wanaotarajia kufundisha watoto walio nje ya mfumo wa shule kwa ongezeko la vipindi vingi vya darasani katika mradi wa Graca Machel Trust (GMT) ambao unatekelezwa kwa kushirikiana na Jimbo Katoliki Musoma.

Akizungumza kwenye hafla ya kufunga mafunzo ya walimu 432 yaliyofanyika kwa muda wa mwezi mzima katika kituo cha ufundi cha St Anthony na Chuo cha Maendeleo ya Jamii cha Buhare, kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mara Bw.Method Mkoba amesema kuwa walimu hao hawana budi kuondoa wasiwasi wa kuwa na majukumu makubwa wakati wa kuwafundisha watoto hao, kwa kuwa tayari serikali imekwishaweka mfumo mzuri utakaowasaidia walimu hao kusimamia majukumu yao bila tatizo.

 Mkoba amesema kuwa Serikali Mkoani hapa imeandaa mikataba ya kazi ambayo itawasaidia walimu hao katika kusimamia majukumu yao hasa kwa upande wa vipindi vya darasani, ambavyo awali walikuwa wanafundisha na sasa wameongezewa tena darasa jingine la MEMKWA, ili kuwapunguzia mzigo mkubwa na kwamba walimu wote watakuwa chini ya mwalimu mkuu wa shule husika.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili, baadhi ya walimu walioshiriki mafunzo hayo wamesema kuwa, wanakuwa na hofu hasa upande wa vipindi vya darasani ambavyo sasa vimeongozeka kwa kuwa awali wengine  walikuwa na vipindi vitano kwa siku sawa na vipindi 25 kwa wiki, hivyo huenda darasa moja likakosa vipindi na hata watoto kufeli somo la mwalimu husika, kwa kuwa mwalimu huyo huenda akajikita zaidi upande wa darasa moja na kushindwa kumudu darasa jingine kwa wakati muafaka.


Mmoja wa walimu kutoka wilaya ya Butiama (jina tunalihifadhi) amesema kuwa Bi.Graca Machel ana lengo zuri la kuwasaidia watoto walio nje ya mfumo wa shule, hivyo ili mradi huu uweze kufanikiwa zaidi,  kwanza yawepo  mazingira rafiki ya kuwafundisha watoto kutokana na ukweli kwamba kuna wengine walikuwa tayari wamekwishaolewa wakiwa na umri mdogo na sasa wanataka kurudi shuleni, wengine wanahitaji muda mrefu wa kuelimishwa hasa kwa kwenda taratibu ili wote waelewe, hivyo itawalazimu walimu hao kutumia muda mwingi zaidi katika madarasa hayo ya MEMKWA kuliko kufundisha darasa la kawaida.

Kaimu Afisa Elimu Mkoa wa Mara Elisonguo Mshiu amewaambia walimu walioshiriki mafunzo hayo ya MEMKWA kuwa wameaminiwa na Serikali, hivyo waende wakafikishe kile walichojifunza katika jamii, kwa kufuata maadili ya utumishi wa Umma na hivyo kuleta matokeo chanya kwa watoto hao watakaokwenda kuwafundisha walio nje ya mfumo wa shule.










Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU