Mitandao isiwatenge na Mungu-Askofu Mstaafu awaonya vijana

MWENYEKITI wa jukwaa la Kikristo Tanzania, mkoani Mbeya, Askofu mstaafu John Mwela, amewaonya vijana wa kitanzania kuwa matumizi ya mitandao ya kijamii na kukua kwa sayansi na teknolojia kusiwatenganishe na Mungu.
Askofu Mwela ameyasema hayo wakati akikabidhi  misaada mbalimbali ya vyakula, nguo na mahitaji muhimu ikiwemo vifaa vya shule vilivyochangwa na wasamaria wema wa kikristo na kiislamu jijijini Mbeya na kuwasilishwa kwa Shirika lisilo la kiserikali  la Sauti ya Mama Afrika(SAMAFO) akisema kuwa mitandao ya kijamii imekuwa ikiwaondolea vijana walio wengi hofu ya Mungu na kuiga matendo yasiyompendeza Mungu.
Ametoa wito kwa shirika la Sauti ya Mama Afrika kuendelea kutoa elimu  kwa jamii  hasa vijana na  familia majumbani kuwa wasimsahau Mungu kwani kwa sasa hali imekuwa ni mbaya kwa vijana walio wengi  wamefikia  hatua ya kuona kwamba Mungu yupo katika mitandao wanayoperuzi.
Askofu Mwela  amesema  kwa sasa  dunia  ni kama kijiji  hivyo vijana wanaona Mungu wao yupo katika mitandao ya kijamii na simu hali inayosababisha  dunia kwa sasa kughubikwa  na dhuluma, uhalifu, matumizi hovyo ya silaha na vitendo vya utekaji, hivyo amewaombea kwa Mwenyezi  Mungu awasaidie ili wanapofundisha  katika program zao  wawakumbushe vijana  athari na faida ya mitandao.
“Utandawazi umetandaa kila mahali, kwa hiyo wanawake mnalo jukumu kubwa kwa vijana kuwafahamisha kuwa  matumizi ya mitandao ya kijamii yasiwasahaulishe Mungu wao na yasiwaondolee kutokuwa na hofu na Mungu wao  kwani kwa sasa hofu haipo, wanaona Mungu hayupo,” amesema.
 “Pengine dunia ilivyo sasa katika mtikisiko wa  hali ya kiuchumi, kiutamaduni, kisiasa, kijamii na hali mbalimbali, tungeisikiliza sauti ya Mama pengine yasingetokea yanayotokea, kwa hiyo Sauti ya Mama Afrika  ni msemo mzuri sana. Katika Biblia unaikuta sauti ya Mama Maria kwa mwanawe Yesu iliposikilizwa kilifanyika kitu cha uponyaji,” amefafanua.
Mwenyekiti  huyu ameendelea kufafanua kuwa Sauti ya mama ikisikilizwa katika jamii uponyaji mkubwa unaweza kutokea  akiwasihi  waendelee na msimamo na utamaduni wa kuwatembelea yatima na wahitaji.
Awali Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika lisilo la kiserikali  la Sauti ya Mama Afrika (SAMAFO), Bi.Tabitha Bughali ameiomba  Serikali ya Mkoa wa Mbeya  kupitia idara ya ardhi kuwapatia uwanja  ili waweze kujenga nyumba ya amani kwa ajili ya kuwafanyia ushauri nasaha vijana na kuwasaidia kisheria wanawake wanaofanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Hata  hivyo baadhi ya watoto yatima  wanaolelewa katika kituo cha mafunzo na malezi cha Msamaria Mwema kilichopo kitongoji cha Idiga, Kata ya Songwe viwandani mkoani Mbeya, Emmy Immanuel na Daniel Richard  wametoa angalizo kwa watoto yatima nchini kutokubali kushawishika na makundi yasiyompendeza Mungu huku  mtoto Sharo Edson akiomba  wasamaria wema kuwajengea wigo na kuimarisha ulinzi katika kituo chao.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU