“Hakuna mafuta mbadala ya krisma”

ASKOFU wa Jimbo Katoliki Iringa Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amewataka waamini kuwaombea mapadri na hasa katika kipindi hiki ambacho wanaadhimisha miaka 100 tokea wapatikane mapadri wa kwanza Tanzania Bara, ili waweze kuishi katika Roho ya kweli isiyo na uroho na pia kuutendea haki ukuhani kwa kumuakisi Yesu katika yote.
Mhashamu Ngalakumtwa ameyasema hayo mwishoni mwa juma katika misa ya kubariki mafuta (Krisma) ya wagonjwa,wakatekumeni na kuyaweka wakfu mafuta ya Krisma, misa ambayo imefanyika katika Kanisa Kuu la kiaskofu la Moyo Mtakatifu wa Yesu Parokia ya Kihesa.
Amesema kwamba ikiwa makuhani hao watafanya vile anavyotaka Roho Mtakatifu, wanamfanya Kristo atende kama zama hizo na siyo kuhani kumzamisha muamini katika giza.
“Siyo mie kuhani nakuzamisha kwenye giza, nashindwa kuwasaidia wale wenye mioyo mizito hapana, natakiwa niwapatie tumaini jipya, na waliokata tamaa niwaelekeze kwamba kabla hajafa hujaumbika,” amesema Mhashamu Ngalalekumtwa.
Aidha Mhashamu Ngalalekumtwa amekemea baadhi ya waamini wanaosema kwamba kuna mafuta kutoka sehemu fulani au ya Mama Bikira Maria na amesema kuwa huo ni upotoshaji mkubwa.
“Hakuna mafuta yanayotumika katika liturujia zaidi ya haya, huo ni upuuzi mtupu na uhuni, mnakufuru huo ni utapeli wa kiroho.
Tutayaweka wakfu mafuta ya Krisma ambayo yanatumika kwa sakramenti mbalimbali na matumizi mengine kama kuitakatifuza altare, ubatizo, kipaimara, wanapakwa pia mapadri na maaskofu, tutabariki mafuta ya wagonjwa na mafuta ya wakatekumeni.” Ameonya
Aidha katika misa hiyo ambapo makuhani hao walirudia viapo vyao, Mhashamu Ngalalekumtwa amesema kwamba, makuhani wanajazwa Roho kuwasaidia waamini sakramenti ya kiroho wanashirikishwa kazi hiyo nzito na takatifu, hivyo waamini wanapaswa kuwaombea.
“Tumekusanyika kuadhimisha karama zetu na pia kurudia viapo vyetu mbele ya Mungu na Kanisa, tunatoa sadaka za kiroho kwa Mungu, daraja hili lina hadhi na majukumu ya kipeke,” Amefafanua
Misa hiyo imehudhuriwa na mapadri 70 kutoka jimboni Iringa, watawa wa kike na kiume pamoja na waamini wenye mapenzi mema.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU