Chuki na dharau vitalibomoa taifa

ASKOFU Jemsi Almasi wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Masasi amewataka watanzania kuondoa chuki na dharau ambazo zinasababisha mauaji na hofu kwa jamii.
Ameyasema hivi karibuni katika mahubiri yake ya Misa ya Pasaka iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Edward mjini Lindi.
Amesema katika kuadhimisha sikukuu ya Pasaka ya ufufuo wa Bwana Yesu Kristo ambaye alifuta hati ya mashitaka ya dhambi kwa wanadamu ili watu wamrudie Mungu wao, lakini kwa sasa ni tofauti kwani wanadamu wameanza ukengeufu.
Askofu Almasi amesisitiza kuwa taifa la Tanzania lilijengewa misingi ya uvumilivu, utii na upendo ambapo kila mtanzania alifanya kazi kila kona ya nchi bila hofu kwa vile alijiamini kuwa watanzania wote walikuwa ni ndugu.
“Kwa sasa taifa hili limeanza kuingiwa na hofu ya maisha, kila mtu amekuwa hana amani ya kufanya kazi ya kuleta maendeleo jambo ambalo litarudisha nyuma jitihada za kufikia maisha bora,”amesema Almasi
    Askofu huyo amesema matatizo yote yanatokana na chuki na visasi ambapo jambo hili linawasababishia watanzania kutoaminiana hivyo kukosa upendo, uvumilifu na utii jambo ambalo litalibomoa taifa ambalo ni teule.
“Taifa la Tanzania linasafiri kwa nguvu za Mungu kwa kuwa watu wake walikwisha futiwa mashitaka na waasisi wetu, hivyo tuheshimu uhuru wa kila raia kwani ana haki sawa na wewe,”amesema Askofu huyo
Ameongeza kuwa kila kiongozi wa serikali katika taifa hili anao wajibu wa kuheshimu msingi wa katiba ya nchi, katiba ya kila dini, maana ndio misingi ya uongozi ambayo inaondoa chuki na visasi.
“Hata Yesu alimwambia Petro rudisha upanga halani, kwani ukifanya hivyo watu wote wataangamia kwa upanga, hivyo basi  sisi tuseme turudishe mitutu yetu ya bunduki ghalani kwani tumeanza kuangamia kwa mtutu jambo linaloleta hofu kubwa kwa maisha yetu.”
Amehitimisha kuwa utii na upendo ndio silaha pekee ya mafanikio ya amani ya taifa linalohitaji maendeleo kwa wananchi wake.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU