Wazazi warithisheni watoto elimu-Askofu Nyaisonga asisitiza

Na Thompson Mpanji, Songwe
WAAMINI  wa Kanisa Katoliki  wametakiwa kuwaendeleza watoto wao katika elimu  ikiwemo na wao wenyewe kujiendeleza katika fani mbalimbali  ili waweze kujiajiri  kupitia mafunzo mbalimbali waweze kujitegemea.
 Elimu ndiyo hazina pekee  na urithi mkubwa kwa familia na jamii kwa ujumla katika  maisha ya sasa  na ya baadaye.
Ushauri huo umetolewa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Mbeya,Mhashamu Gervas Nyaisonga  wakati wa homilia yake  katika adhimisho la Ibada ya Misa Takatifu  iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Francisco wa Asiz, Kigango cha Mkwajuni,Parokia ya Mwambani,jimboni humo.
Walioshiriki ibada hiyo licha ya waamini wa parokia hiyo, walishiriki pia Wafanyakazi wa Hospitali ya Mwambani inayomilikiwa na Jimbo Kuu Katoliki la Mbeya, iliyopo katika Kigango hicho ambako Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Mbeya Mhashamu Gervas Nyaiaonga alifanya ziara ya kutembelea Hospitali hiyo.
Katika Homilia yake Askofu Nyaisonga amesema elimu ni hazina kubwa na msingi wa maendeleo katika familia, jamii na taifa kwa ujumla.
“Wazazi na walezi wasomesheni watoto wetu kwani katika maendeleo ya sayansi na teknolojia ni muhimu sana,lakini pia  nanyi mkipata nafasi mjiendeleze kielimu  na katika fani mbalimbali,” amefafanua Askofu Nyaisonga.
Aidha ametoa wito kwa madaktari, wauguzi na wafanyakazi wa fani mbalimbali katika Hospitali  ya Mwambani kuwahudumia  wagonjwa kwa upendo,huruma na unyenyekevu kadri ya weledi wao bila kujali tofauti za kiimani.
Amesema kazi waliyoichagua ni wito na utume wa kujitoa  kuwahudumia wagonjwa na wahitaji mbalimbali, hivyo wanapaswa kufuata nyayo za Muuguzi mwanzilishi Florence Nightingale.
“Muwe watu wa huruma kwa wagonjwa,muwe wapole,wakarimu na wanyenyekevu na lugha itakayoweza kuwatia moyo wagonjwa,” amefafanua.
Hata hivyo amewakumbusha  waamini  na wakristo umuhimu wa kusali na kumuomba Mungu katika maisha yao ya kila siku ili aweze kuwafundisha,kuwaongoza na kuwasaidia katika maisha.
Hospitali  ya Mwambani iliyopo makao  makuu ya Wilaya ya  Songwe,mkoani songwe  inamilikiwa na Kanisa Katoliki Jimbo Kuu Katoliki Mbeya kwa kushirikiana na Serikali.



Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU