Mkatoliki anayepokea rushwa anaikana imani yake-Ask. Kassala amesema

Na Jimmy mahundi, Mtwara
MAkamu wa Rais Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Askofu Flavian Kassala amewataka waamini wa Kanisa Katoliki kuiishi imani yao inayomtaka mkristo kuwajibika kwa uadilifu, kuichukia dhambi yakiwemo masuala ya rushwa.
Amesema hayo wakati wa adhimisho la Misa Takatifu ya Jumapili ya 6 ya Pasaka katika Kanisa Kuu la Kiaskofu la Watakatifu wote la Jimbo Katoliki Mtwara
Ametaja baadhi ya mambo ambayo yamekuwa kikwazo katika imani  ikiwemo, rushwa, udini,ukabila na umaeneo ambayo vyote hivyo vimekuwa sababu ya mateso kwa wanadamu wengi katika nyakati hizi na matokeo yake ni kushuka kwa imani miongoni mwa waamini.
“Haiwezekani jana umepokea rushwa kwa mtu mmoja na leo umekaa karibu naye kanisani halafu wakati wa kutakiana amani mnashikana mikono ya amani!,” amesema Askofu Kassala
Kufuatia hali hiyo amewataka waamini kote nchi kuishi kwa kuzingatia imani yao inayokataza rushwa, chuki, ubaguzi wa dini, rangi, kabila, maeneo nk.
“Imani yetu inasisitiza upendo, msamaha, amani, huruma, uwajibikaji wenye uadilifu nk,” amesema.
Aidha Kassala amewashukuru waamini na wananchi wa mkoa wa Mtwara kwa moyo wao wa upendo na shukrani kwa Mungu kwa kujituma katika maandalizi na kufanikisha maziko ya Marehemu Askofu Mstaafu Gabriel Mmole ambayo yalifanyika Mei 22 mwaka 2019 jimboni humo.
Amewataka wanamtwara kuendeleza ushirikiano na mshikamano kama walivyofanya wakati wa msiba wa Marehemu Askofu Mmole.
“Maaskofu wamefurahishwa na maandalizi walioyakuta wakati wa maziko ya Askofu Mmole na imeonyesha namna wanajimbo kwa kushirikiana na viongozi wa Kanisa wanavyofanya kazi kwa pamoja na huo ni ukomavu wa iamani,”amesema Askofu Kassala ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki Geita.
Kwa upande wake mwenyekiti wa halmashauri walei jimbo la Mtwara Paul werema amewashukuru waamini wote kwa namna walivyojitokeza kwa zaidi ya wiki mbili katika maandalizi na hatimaye kufanikisha maziko ya marehemu Askofu Mmole..
Werema amesisitiza kuendelea na umoja katika mambo mbalimbali ya furaha na huzuni kwa kuwa ni umoja pekee ndio utasaidia kufanikisha kila jambo jimboni humo. 
Hata hivyo mwenyekiti huyo amewataka wanajimbo kuwa tayari kwaajili ya kupokea ugeni wa  kongamono la wawata kutoka majimbo ya kusini, ambalo litafanyika Mtwara mwezi juni na amewaomba akinamama wote kushirikiana katika kufanikisha shughuli hiyo.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU