Ask. Kinyaiya:Acheni kuwatafuta masangoma wakati ninyi ni wakristo

Na Rodrick Minja, Dodoma
ASkofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki  Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaiya, amewaonya baadhi ya waamini wenye tabia ya kwenda kwa waganga wa kienyeji kupeleka matatizo yao.
Amewataka  kuachana na imani hiyo mara moja.
Ametoa kauli hiyo  kwenye Ibada ya Misa Takatifu alipokuwa anatoa Sakramenti Takatifu ya Kipaimara  kwa vijana 82 wa Parokia ya Bikira Maria Msaada wa Wakristo  Kizota Jimboni Dodoma.
Askofu Kinyaiya amesema kwa kufanya hivyo muumini anakengeuka na hawezi kuishika imani yake vilivyo kwani atakuwa unatangatanga kiimani.
“Tafadhalini sana ndugu zangu tuachane na imani hizo kwa wale wanaokwenda kwa waganga wa kienyeji, Yesu ndiye kila kitu,”amesema Askofu Mkuu Kinyaiya.
Askofu Kinyaiya, amewaasa vijana waliopokea sakramenti ya kipaimara kuwa askari hodari wa Yesu Kristo kwa kuilinda na kuitetea imani yao.
Aidha amewataka vijana hao kuwa waaminifu na wajiandae kupokea masakramenti mengine yaliyobaki ya ndoa na utawa/ Upadri kwa wale watakaokuwa na wito huo.
Akitoa tafakari ya somo la kwanza kutoka katika kitabu cha mwanzo Askofu Mkuu Beatus Kinyaiya amesema, Mungu aliona mahangaiko ya utupu wa mwanadamu ndio maana alimleta mwanae Yesu Kristo kuja kutusitiri.
Askofu Kinyaiya amekaza na kusema kwa mazingira ya kawaida na ya kimaumbile  utupu haukubaliki, hivyo kutokana na dhambi walizozitenda  Adam na Eva bustani ya Edeni walijikuta wapo utupu na kuanza kuhangaika kujisitiri.
 “Wapendwa Taifa la Mungu ninawaombeni mumkabidhi Mwenyezi Mungu maisha yenu jumla kwani tukimkabidhi hakuna kitakachotuyumbisha katika maisha ya hapa duniani,” Askofu Kinyaiya amesema.
Katika  hatua nyingine amewataka waamini wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma kuhakikisha kuwa wananunua Biblia Takatifu na kuzisoma kwani kupitia Maandiko Matakatifu yaliyopo katika Biblia hizo wataweza kujua habari njema za wokovu.
 “Nawaombeni mnunue biblia na mtenge muda wa kuwashirikisha watoto wenu neno la Mungu” ameongeza  Askofu Kinyaiya.
Aidha amehitimisha homilia yake kwa kuwakemea wale wote wenye tabia ya kudanganyika na mafundisho ya baadhi ya watu wa imani nyingine kwamba watakapokwenda kuombewa na wao watapata ajira, uponyaji, watabarikiwa katika shughuli zao, na wengine hata kuwarubuni kuwauzia maji ya baraka .


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU