Kadinali Pengo aonya waamini wavivu

Na Philipo Josephat Dar Es Salaam
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam Mwadhama Palycarp Kadinali Pengo amewaonya watu mbalimbali wanao watumikisha wenzao katika kufanya kazi kwa manufaa yao huku wao wakiwa mawestarehe.
Kadinali Pengo amesema hayo katika Ibada ya Misa Takatifu ya Mtakatifu Yoseph iliyoandaliwa na wanaume wa katoliki (UWAKA) na kufanyika katika viwanja vya hija Pugu Dar es salaam.
“Wapo watu ambao wamekuwa wakiwatumikisha wenzao kazi ili hali wao wameketi bila hofu yoyote na wakiwa wamesahau sauti ya Mwenyezi Mungu anamtaka kila mmoja kutafuta chakula chake kwa jasho.
Mwenyezi Mungu aliwaambia wazazi wetu kuwa kwa jasho lao watapata chakula, hivyo kila mmoja wetu afanye kazi bila kumtumikisha mwenzake huku tukiendelea kujifunza kwa Mtakatifu Yoseph ambaye licha ya kupewa jukumu la kumtunza Mungu aliendelea na kazi yake ya useremala na pengine tungejiuliza kwa nini hakukaa raha mstarehe badala yake aliendelea na kazi yake,” ameeleza.
Ameongeza kuwa Mtakatifu Yoseph alipopewa jukumu la ulinzi wa mtoto Yesu angeweza kuomba kwa Mwenyezi Mungu amfanyie kitu ili maisha yao ndani ya familia yawe mazuri na aachane na shughuli za useremala.
 Lakini hakufanya hivyo bali anatufundisha kufikiria wengine kwanza kwa kuona ni lipi la manufaa kwao kama Yesu alivyoacha yote na kuwatazama vipofu, viwete, na wakoma kwa kuwapa tumaini ya kutembea tena na kuona tena.
Amesema kila mtu anapaswa ajifunze kupitia kwa mtakatifu Yoseph kufanya kazi hata ile inayodharauliwa kwenye jumuiya ya watu ili itupatie riziki na kuwasaidia wengine wasioweza kufanya kazi.
Aidha Kadinali Pengo amewataka wanaume Katoliki kufanya kazi na kushirikiana kwa pamoja huku wakiisikia sauti ya Mungu kwa majitoleo ya hali na mali katika kukijenga kituo cha Hija Pugu ili kiwe eneo bora Afrika Mashariki kwa watu kufika na kuja kufanya Hija.
Wakati huo huo Padri Raymond Mbaula anayehudumu katika Seminari ya Visiga na Paroko Msaidizi wa Parokia ya Mlandizi kwa pamoja wamewaongoza wanakwaya wa Mtakatifu Yoseph Kigango cha Visiga katika kusherekea somo wa kwaya hiyo sherehe zilizofanyika kigangoni hapo na kuhudhuriwa na kwaya mbalimbali ikiwemo kwaya ya Gabriel Malaika Mkuu kutoka Parokia ya Roho Mtakatifu Segerea sanjari na kwaya za Kristo Mfalme, Mtakatifu Maria na Mtakatifu Sesilia zote kutoka Parokia ya Mlandizi.    


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU