TANZIA


Matukio yaliyojiri katika Adhimisho la Misa Takatifu ya Mazishi ya Padri Filipo Mrope (94) aliyefariki dunia Juni 19 mwaka huu huko kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara iliyoko Ndanda katika Wilaya ya Masasi Mkoani humo.


UMATI wa waombolezaji wamejitokeza kumzika Padri Filipo Mrope (94) aliyefariki dunia Juni 19 mwaka huu huko kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara iliyoko Ndanda katika Wilaya ya Masasi Mkoani humo.

Akitoa salamu zake Askofu Askofu Titus Mdoe wa Jimbo Katoliki Mtwara amemshukuru Mungu kwa kuwapatia zawadi ya Padri huyo na kwa namna ya pekee ameshukuru huduma na utume alioufanya Padri Mrope katika majimbo ya zamani ya Ndanda,Nachingwea na hatimaye Jimbo la Mtwara.

Amesema kuwa kabla ya kuaga dunia aliagana na Padri Mrope ambaye  amewahimiza wakristo Jimboni humo kuzidi kumuomba Mungu kusudi aite vijana wengi ambao wataisikia sauti yake kusudi wawe mapadri na watawa wa kike na kiume ili kukabiliana na changamoto ya ukame wa miito iliyomo Kanisani hivi sasa.

Aidha Askofu Mdoe ametumia fursa hiyo kuwataka Mapadri kuchochea miito kupitia maisha yao na utendaji wa kazi za kueneza Injili; kama Padri Mrope alivyofanya kiasi cha kuwavuta vijana wengi kujiunga na Seminari kupitia maneno na matendo yake katika huduma zake  za Kipadri.

Adhimisho hilo la Misa ya Maziko limehudhuriwa pia na Askofu Mstaafu wa Jimbo Katoliki Mtwara Mhashamu Gabriel Mmole, Maabate Wastaafu wa Ndanda Siegifried OSB na Dionynis OSB, Mapadri toka majimbo ya Dar es Salaam, Lindi, Mtwara, Tunduru-Masasi,na Zanzibar, Watawa wa kike na kiume pamoja na waombolezaji wengine toka sehemu mbalimbali nchini.

Kwenye mahubiri yake, aliyekuwa Naibu wa Askofu Mmole, Padri Galus Chilamula, amesema kama waombolezaji hususan Watawa wa kike na wa kiume wangepata nafasi ya kumwelezea Padri Mrope, wangesimulia jinsi walivyonufaika naye kwa huduma zake mbalimbali kwa njia ya ushauri na mafundisho yake aliyoyatoa wakati wa mafungo na nyakati zingine enzi za uhai wake.


Kuhusu mwaka wa Yubilei ya Huruma ya Mungu, Padri Chilamula amewahimiza waamini kutumia fursa iliyotolewa na Kanisa kwa kujipatanisha na Mungu kwa njia ya kupokea Sakramenti mbalimbali, hususani ya Upatanisho ,kusudi kuifaidi huruma na wema wa Mungu ambao hauna mipaka. Kwa namna ya pekee amewakumbusha wote kuzingatia miito waliyopewa na Mungu na kuitumia kwa manufaa ya Kanisa na hata jamii inayowazunguka.

Naye  Kiongozi (Priori) wa Nyumba ya Watawa wa Mtakatifu Benedikto Ndanda, Padri Silvanus Kessy, kwa niaba ya Abate Plasido OSB amewapa pole wote waliopatwa na majonzi kutokana na kifo cha Padri Mrope. Amesema kuwa licha ya Padri huyo kuwa muungamishi wao,kuna mambo ambayo wamejifunza katika kipindi chote cha miaka 30 aliyoishi kati ya Wanajumuiya hao.

Mambo hayo ni mapenzi yake ya maisha ya sala, kujali muda na kupenda mazoezi ya mwili, kwani mara nyingi alitembea kwa miguu katika huduma zake za Kichungaji alizotoa jirani na ilipo Nyumba ya Watawa hao.

Naye Meneja wa Duka la Vitabu Ndanda ,Padri Sebald OSB alivionesha vitabu mbalimbali ikiwemo Agano Jipya ambayo ilitafsiriwa kwa  Kiswahili na Padri Mrope,na kwamba alikuwa bingwa wa lugha za Kilatini, Kiingereza na Kiswahili.

Wengine waliotoa salamu za rambirambi ni Askofu James Almas wa Dayosisi ya Anglikana Masasi, Naibu wa Askofu wa Lindi, Padri Angelus Chitanda na Mwakilishi wa Askofu wa Jimbo la Tunduru Masasi Padri Herman Mchopa.

HISTORIA YA PADRI MROPE
Akiwa mtoto wa nane kati ya watoto 10 wa Familia ya Mzee Mikael Humkamaru Mrope na Bi Melania, amezaliwa Kijiji cha Chigugu Masasi Juni 6,1922,na baada ya miaka 12 alibatizwa.

Elimu; Alianza Elimu ya Msingi Kijijini kwake Chigugu mwaka 1931-1937,na mwaka 1938 hadi 1941 alisoma Shule ya Walimu-TTC huko Ndanda.Katika kipindi hicho Filipo alisikia wito wa Upadri akapelekwa Seminari ndogo ya Kigonsera Ruvuma pamoja na wenzake Klement Mapua, Xaver Chinyang’anya,na Paulinus Nnembuka.

Kutokana na sababu mbalimbali vijana wawili walitoka Seminari,wakabakia Paulinus na Filipo ambao kwa miaka 1942-1946 waliongezewa madarasa ili waweze kumudu masomo ya Falsafa na Teolojia.


Baada ya kumaliza masomo hayo,mwaka 1946/47,mwaka 1948  walijiunga na Seminari Kuu Peramiho kwa ajili ya masomo ya Teolojia. Iikuwa tarehe 26 Oktoba 1955,ambapo Mhashamu Askofu Victor Haelg OSB, wa Jimbo la Ndanda wakati huo,aliwapa Daraja takatifu ya Upadre kwenye Kanisa Kuu la Ndanda.

UCHUNGAJI:Mwaka 1956 Padre Mrope alikuwa Paroko Msaidizi Parokia ya Nkowe na miaka sita alipelekwa Seminari Ndogo ya Namupa kuwa Mwalimu.Katika kipindi cha mwaka 1963-1964 aliazimwa na Uongozi wa Jimbo la Nachingwea wakati huo akawa Katibu wa Elimu wa shule za Jimbo hilo,na baada ya mwaka mmoja alirudi Jimboni Ndanda na kuendelea kuwa Katibu wa Elimu wa Jimbo hilo.

Mwaka uliofuata alifanywa Paroko wa Parokia ya Malolo na mwaka 1967 akahamia Newala ambako alikuwa Paroko Msaidizi. Mwaka 1968-1976 alikuwa Paroko kwenye Parokia za Lukuledi, Nachingwea, Liwale na Migongo Masasi. Katika kipindi hicho Padri Mrope alichaguliwa kuwa Makmu wa Askofu wa Jimbo la Nachingwea wakati huo Askofu Arnold Cotey SDS.

1968-1998 Padri Mrope alikuwa Mjumbe wa Liturujia Kitaifa akiungana na mabingwa wengine wa Kilatini walitafsiri Sala za Misa Takatifu katika lugha ya Kiswahili. Wajumbe wengine walikuwa Askofu Joseph Sipendi wa Jimbo la Moshi, Padri John Kabeya wa Jimbo la Tabora na Padri Stephen Mlunde wa Jimbo la Dodoma.

Baada ya kazi hiyo kukamilika Padri Mrope 1976-1979 alirudi Mtwara na akafanywa Paroko wa Rondo. Mwaka 1979-1982 Paroko Nanganga. Mwaka 1982-1988 Paroko Namupa sanjari na kuwa Baba wa Roho katika Seminari ndogo ya Namupa.

Mwaka 1981-1982 Padri Filipo pamoja na Padri Valerian Fataki wa Dar Es Salaam walifanya tafsiri ya Sala za Misa Takatifu huko Mafinga Iringa.
Mwaka 1988 Padri Mrope alikuwa Baba wa Roho wa Masista Wabenediktini wa Bikira Maria Msaada wa Wakristo Ndanda hadi alipostaafu kutokana na uzee.

Pamoja na mambo mengine Padri Mrope atakumbukwa na wengi kutokana na upole wake, unyenyekevu wake,ucheshi wake na kwamba alikuwa Mwanasanaa aliyebobea. Na katika matukio mbalimbali aliwavunja watu mbavu kwa vibweka na vichekesho vyake vilivyotumbuiza watu.

 Na Anthony Chilumba, Ndanda






Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU