‘Jubilei ni azimio la kuanza upya wa maisha, siyo idadi ya miaka’

Na Pascal Mwanache, Imiliwaha
IMEELEZWA kuwa jubilei siyo tu idadi ya miaka fulani, bali ni azimio la kuanza upya wa maisha katika kuelekea ukamilifu na utakatifu. Hayo yamesemwa na Abate wa Abasia ya Hanga-Songea, Abate Octavian Masingo wakati wa Adhimisho la Misa Takatifu ya uzinduzi wa Jubilei ya Miaka 50 ya Shirika la Masista wa Mtakatifu Agnes-Chipole, Nyumba ya Mtakatifu Getrude Imiliwaha.
Akitoa homilia katika adhimisho hilo Abate Octavian amesema kuwa katika kipindi cha jubilei masista hao hawana budi kuweka mikazo na mikakati thabiti kuelekea katika kilele huku mkazo ukiwekwa katika kutathmini hali halisi ya wito wao badala ya kujikita katika kuhangaikia vitu.
“Mnapoizindua jubilei hii mnaazimia kuanza upya maisha yenu ya kiroho. Inawapasa kunuia kuelekea katika utakatifu na ukamilifu” ameeleza.
Aidha ameongeza kuwa maandalizi ya kuelekea kilele cha jubilei hiyo hayapaswi kujikita katika vitu kwani kufanya hivyo ni kupotosha dhamira ya kumshukuru Mungu. Badala yake ameshauri kuwa maandalizi hayo yaendane na uwajibikaji na utendaji mpya katika kumshukuru Mungu.
“Tendo la uzinduzi huashiria shukrani kuelekea katika utimilifu. Mumtegemee Mungu kwa sababu amewabeba na kuwasaidia hata sasa na hata kufikia utimilifu wa maisha yenu na kazi yenu ya uinjilishaji” ameongeza.
Misa ya uzinduzi wa Jubilei hiyo imeongozwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Njombe Mhashamu Alfred Maluma katika nyumba ya Mtakatifu Getrude Imiliwaha.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU