Ushoga siyo haki ni udhalilishaji wa binadamu


Na Pascal Mwanache, Dar es salaam
Katika kuadhimisha miaka 70 ya azimio la ulimwengu la haki za binadamu viongozi wa dini kutoka Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) wamekutana na kuweka wazi kuwa wanalo jukumu la kusimamia haki huku wakibainisha kuwa vitendo vya ushoga vinadhalilisha utu wa mwanadamu.
Akitoa mada katika kongamano hilo Katibu Mkuu wa TEC Padri Dkt. Charles Kitima amesema kuwa katika jamii zote, haki za binadamu zipo hasa katika mila na desturi na kwamba haki za msingi ni stahili za kila binadamu kwa sababu ya utu wake.
“Maandiko Matakatifu yanatambua haki za binadamu kwa mfano haki ya kuwa na familia, kuoa na kuolewa. Ndiyo maana ushoga unapigwa vita. Ndoa iwe na fursa ya kuendeleza ubinadamu. Utaletaje ndoa ambayo haina ya kuzaa” amehoji Padri Kitima.
Aidha amesema kuwa viongozi wa dini hawana budi kupigania na kusimamia haki za wanyonge kama ambavyo wanaendelea kufanya bila woga. Ameongeza kuwa Kanisa Katoliki linahuisha mchango wa kimaadili kwa jamii, na hivyo kuhimiza umuhimu wa kulinda haki za binadamu.
“Tangu mwaka 1997 viongozi wa dini wamepambana na haki katika migodi na kuisaidia serikali. Miaka 20 mmepiga vita na kusimamia haki ya mnyonge mpaka haki ifanyike. Hivyo viongozi wa dini tuna kazi pia ya kulinda haki za umiliki wa ardhi kwa manufaa ya wananchi wote” amesema.
Kwa upande wake Mjumbe wa Baraza la Ulamaa BAKWATA Sheikh Issa Athuman Issa amesema kuwa mwili wa binadamu ni dhamana kutoka Mungu na hivyo haki za binadamu hazina budi ziangaliwe kwenye jicho la kiimani.
“Wengine wanazungumzia kuwa mwili wake ni milki yake na anaweza kuutumia kadiri anayotaka. Vifungu 2 na 3 vinaungana na dharura tano kadiri ya Uislamu: Moja, kuhifadhi dini: kuheshimu yanayorudiwa; Mbili, kuhifadhi nafsi yake na ya wengine “Wewe, usidhuru, na usiwe na sababu ya mwingine kudhurika. Tatu, Kuhifadhi akili: dhidi ya ulevi, madawa ya kulevya. Nne, kuhifadhi nasaba au koo, kwa utaratibu wa kuoana. Kama ushoga hauhifadhi ukoo. Tuliogope na tulilinde sana swala la koo na nasaba. Na tano ni kuhifadhi hadhi ya mtu, nafsi yake” amesema .
Pia aeongeza kuwa msingi wa kwanza ni kumfanya mtu ajitambue thamani yake na hivyo viongozi wa dini wanapaswa wahakikishe kuwa binadamu anatambua thamani yake. “Tuambukize kwa watoto wetu kujitambua kuwa wana thamani kama binadamu” ameeleza.
Akielezea juu ya maadhimisho hayo Askofu wa Jimbo Katoliki Mbinga Mhashamu John Ndimbo amesema kuwa azimio hilo ni chimbuko la viongozi wa dini mbalimbali kukaa pamoja na kutathmini mikakati itakayowawezesha katika kulinda na kutetea haki za binadamu.
“Azimio hili ndani ya miaka 70 limetufanya sisi wa dini mbalimbali tuje pamoja tuzungumze pamoja, tukae pamoja tuangalie watu wetu wanaishi namna gani na wanapata haki zao” amesema.
Naye Sheikh wa Mkoa wa Pwani Sheikh Hamis Mtupa amebainisha kuwa vitendo vya ushoga havipaswi kukingiwa kifua mbele kwa kuwa havikubaliki kwa Mungu na hata kwa jamii.
“Kuna haki nyingine ambazo huwa zinasemwa kuwa ni haki za kibinadamu lakini siyo haki za kibinadamu bali ni haki za kudhalilisha utu wa mwanadamu. Ni kama vile mahusiano ya jinsi moja, wanawake kwa wanawake au wanaume kwa wanaume. Ni jambo ambalo halifai. Ni jambo ambalo tunapaswa kuliondoa kwani linamuudhi Mungu” ameweka wazi.
Kwa upande wake Askofu wa AIC Pwani Askofu  Charles Salala amesema kuwa kitu muhimu ni jinsi ambavyo jamii ya sasa inavyorithisha maadili kwa kizazi kinachofuata.
“Jinsi tunavyoishi sasa ndiyo huamua jinsi kizazi kitakachofuata kitakavyokuwa. Tunahitaji kuwekeza kwa watoto na vijana wetu” amesema.
Maadhimisho hayo yamefanyika Desemba 10 katika ukumbi wa mikutano Golden Tulip jijini Dar es salaam na kuhudhuriwa pia na wadau wa masuala ya haki za binadmu nchini.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU