Askofu Kinyaiya aonya vijana juu ya mitandao

Na Mwandishi wetu Dodoma
askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaiya amewataka wazazi na walezi kuwa na jicho la pekee kwa vijana wao ambao wanaishi katika kizazi chenye kasi ya maendeleo ya utandawazi.
Akofu Mkuu Kinyaiya amesema hayo kwenye Ibada ya Misa Takatifu ya Kilele cha Jubilei ya miaka hamsini tangu kutabarukiwa kwa Kanisa la Mtakatifu Paulo wa Msalaba Jimbo Kuu Katoliki Dodoma.
Jubilei hiyo imeenda sambamba na kutoa Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 75.
Askofu Kinyaiya amewataka wazazi na walezi kuwasimamia vijana wao vema katika suala la maadili kwani ulimwengu wa sasa umeghubikwa na utandawazi mkubwa wa teknolojia ambayo kwao wakiitumia vizuri itawasaidia na wakiitumia vibaya itawapoteza.
“Vijana wa sasa wanaishi mitandaoni na wanasikia kelele nyingi. Ni vyema wazazi wakendelea kuwaelekezaa, kuwaonesha mjia sahihi.
Pia kuwaelekeza kujua namna ya kuchuja sauti mbalimbali za mitandao, kuchuja mitindo ya maisha ambayo ni kinyume na maadili yetu,” amesema Askofu Mkuu Kinyaiya.
Pia amewataka vijana 75 ambao wameimarishwa kwa sakramenti ya Kipaimara kuhakikisha kuwa wanakuwa  askari hodari Yesu Kristo katika kulitangaza neno la mungu popote pale watakapokuwepo.
Pia amewataka waimarishwa hao kuhakikisha kuwa wanaisoma biblia ambayo kwayo itakuwa ni nguzo muhimu ya kuwakuza kiimani na kiroho.
Kwa nyakati tofauti, Makamu wa Askofu Mkuu Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Padri Chesco Msaga amesema  kuwa dhambi iliingia ulimwenguni kwa kiburi, kutotii, kutosikiliza sauti ya mwenyezi Mungu na kutosikiliza maagizo yake mwenyezi Mungu.
Hayo ameyaeleza alipokuwa akitoa homilia yake katika Ibada ya Misa Takatifu ya Sikukuu ya Bikira Maria Mkingiwa wa Dhambi ya Asili,ibada iliyokwenda sambamba na wanovisi 10 wa Shirika la Upendo wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili na kuweka  nadhiri  za kwanza ndani ya shirika hilo.
Amewaasa wanovisi hao ambao wameweka nadhiri za kwanza za utawa  kuwa Mungu amewaita kuishi maisha ya useja, na kuweka nadhiri ya ufukara hivyo hawatajilimbikizia mali bali watatumia vyote kwa sifa na utukufu wa mwenyezi Mungu.
Wanovisi  walioweka nadhiri za kwanza ni Agatha Urassa, Alice Kamwara, Editha Yunde, Felista Laurenti, Jonisia Munyi, Mary Okello, Moureen Ogwaro, Veneranda Sangawe, Victoria Richard pamoja na Winny Francis.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU